Kusitawisha Kupendezwa na Ujumbe wa Ufalme
1 Wakati fulani umepita—labda siku moja au mbili, labda juma moja—tangu uliposema mara ya mwisho na mtu aliyependezwa na ujumbe wa Ufalme. Iwe alikubali fasihi ya Biblia au la, ni jambo la maana kusitawisha kupendezwa kokote haraka iwezekanavyo.
2 Pitia maandishi uliyoandika kwa uangalifu baada ya ziara ya kwanza. Halafu, unapotayarisha mkoba wako wa kutoa ushahidi, hakikisha unatia ndani nakala ya fasihi uliyoangusha ili uirejezee wakati wa ziara ya kurudia.
Ikiwa uliangusha broshua “Tazama!” huenda ukasema:
◼ “Ninafurahi kukuona tena. Tulipozungumza wakati uliopita, nilikuonyesha jalada la broshua hii, na tukasoma andiko la Biblia ili kuthibitisha kwamba, kupitia Ufalme wake, Mungu ataandaa makao na kazi kwa kila mtu. Lakini Mungu ameahidi pia kukomesha magonjwa, uzee, na hata kifo. Je! unaona hilo kuwa jambo gumu kusadiki? [Ruhusu itikio la mwenye nyumba.] Ona jambo hili katika fungu la 4 la broshua niliyokuachia.” Soma fungu hilo, na zungumzia andiko moja au mawili kati ya yale yaliyoorodheshwa chini ya ukurasa. Funzo la Biblia linaanzishwa!
3 Ili kutayarisha njia kwa ajili ya ziara itakayofuata, ungeweza kumalizia mazungumzo kwa kusema:
◼ “Bila shaka, kila kitu tulichozungumzia kimo katika Biblia, lakini watu wengi wanajiuliza kama wanaweza kusadiki kweli kweli yale Biblia isemayo. Nikija wakati huo mwingine, ningependa kuchukua dakika chache kuzungumzia jambo hilo na wewe.” Unaporudi kusitawisha kupendezwa, endelea na mazungumzo kutoka kichwa kidogo “Kitabu Kinachoeleza Paradiso,” kuanzia fungu la 5 la broshua hiyo.
4 Katika Maeneo Ambamo Fasihi Chache Zinaangushwa: Utoaji huohuo waweza kutumiwa tunapowazuru watu walioonyesha kupendezwa kiasi fulani lakini hawakuchukua fasihi. Huenda ukarejezea broshua uliyotoa mlipokuwa na mazungumzo wakati uliopita. Huenda ikahitajiwa kufanya ziara za mara kwa mara ukitumia Biblia na nakala yako ya kibinafsi ya broshua hiyo kabla mwenye nyumba hajakubali kupata broshua. Ikiwa uliangusha magazeti ya karibuni, rejezea vichwa vinavyolingana katika broshua “Tazama!” unaporudi kusitawisha kupendezwa.
5 Ziara nzuri za kurudia zinazoongoza kwenye funzo la Biblia katika broshua Serikali zaweza kutayarishwa kwa kutumia habari katika kurasa 282-4 za kitabu Kutoa Sababu. Au funzo la Biblia laweza kuanzishwa kwa kuuliza swali: “Je! ulijua kwamba Biblia hutoa matumaini mawili? Moja yayo ni kuishi duniani milele. Broshua hii inaeleza jinsi hilo litakavyowezekana.” Halafu fungua ukurasa 15 wa broshua hiyo, na usome maandiko matatu yaliyoonyeshwa.
6 Ikiwa umeangusha magazeti mawili, kitabu, au broshua au umekuwa tu na mazungumzo ya Biblia yenye kupendeza na mtu fulani, una jukumu la kusitawisha kupendezwa. Tunawatia moyo nyote kuweka kando wakati fulani katika Julai ili kushiriki katika kazi hiyo ya kuokoa uhai.—1 Tim. 4:16.