Rudi kwa Shangwe ili Kusaidia Wenye Kupendezwa
1 Kila mtu anayeshiriki katika kazi ya nyumba kwa nyumba anatamani kusaidia watu wanaopendezwa. Kwa kutoa msaada huo, tunapata shangwe yenye kina na kuridhika. (Linganisha Zaburi. 126:5, 6.) Hilo lataka tuwe tumejitayarisha.
2 Kujitayarisha kwaanza na kuweka habari yenye kina katika rekodi ya nyumba kwa nyumba. Andika habari mliyozungumzia kwenye ziara ya kwanza na itikio la mwenye nyumba. Huenda hata ukataka kuandika jinsi ungependa kuanza mazungumzo unaporudi.
3 Kwa mfano, ikiwa ulirejezea ile Sala ya Bwana mara ya kwanza, ungeweza kusema kifupi hivi:
◼ “Katika ziara yangu iliyopita, tulizungumzia jinsi mapenzi ya Mungu yatakavyofanywa duniani na kwamba amani itaonekana katika sehemu zote za maisha. Kuhusiana na jambo hilo, tafadhali angalia broshua hii Serikali Itakayoleta Paradiso, inavyosema kuhusu baraka nyinginezo ambazo Ufalme wa Mungu utaletea ainabinadamu.”
4 Ikiwa mtu alielekea kutoamini Mungu, sema hivi:
◼ “Nilipokuwa hapa wakati uliopita, tulikuwa tukiongea jambo ambalo Paulo alitaja katika Waebrania 3:4, akitoa sababu za kiakili za kuamua kwamba lazima kuwe na Mfanyi wa vitu vyote mwenye weledi.” Soma andiko hilo tena na uelekeze kwenye kurasa 4 hadi 9 za broshua Je! Kweli Mungu Anatujali?, ukianzia pale utoaji wako wa kwanza ulipoachia. Uliza swali halafu usome fungu, ukiruhusu mwenye nyumba ajibu swali. Ikifaa, mkaribishe achukue broshua yake na mwangalie habari hiyo pamoja.
5 Ikiwa mwenye kurudiwa ni kijana, unaweza kurejezea ile trakti Je! Ulimwengu Huu Utaokoka? na urudie linalotajwa kwenye ukurasa wa 6. Mwulize mwenye nyumba ikiwa anatamani kuishi kwenye paradiso yenye kupendeza duniani. Ili kusaidia kuimarisha kupendezwa kwake, unaweza kumwuliza atoe maelezo yake kuhusu picha yenye kutia moyo au jambo fulani katika gazeti unalotumia.
6 Mfikio huuhuu wa kimsingi waweza kutumiwa pamoja na makala ambayo huenda ikawa ulizungumzia katika Mnara wa Mlinzi au Amkeni! Rejezea makala iliyoonyeshwa kwenye ziara yako ya kwanza na utaje jambo jingine la kupendeza katika makala hiyohiyo au moja katika makala nyingine uliyo nayo. Ikiwezekana, someni andiko pamoja na umuulize mwenye nyumba atoe maelezo yake.
7 Weka akilini mradi wako wa kuanzisha funzo la Biblia. Kwa kawaida huchukua ziara kadhaa ili kusitawisha kupendezwa kwa kadiri hiyo. Onyesha kuhangaikia kwako binafsi mwenye nyumba kwa kurudi upesi iwezekanavyo.
8 Habari njema tunazotangaza hutokeza shangwe kubwa. (Lk. 2:10) Wenye kupendezwa wanapoitikia kutokana na jitihada zetu, hiyo kwa hakika ni sababu ya kushangilia. (Flp. 4:1) Acheni tupate shangwe hiyo kwa kurudi ili kuwasaidia wenye kupendezwa tunaowapata shambani.