Kufundisha kwa Kutumia Broshua Habari Njema
1. Ni nini kusudi la broshua Habari Njema?
1 Kama ilivyoelezwa katika makala ya Huduma Yetu ya Ufalme ya Julai, broshua Habari Njema Kutoka kwa Mungu! ni mojawapo ya kifaa muhimu tunachotumia kufundishia. Maandiko yaliyoonyeshwa, hayajanukuliwa ili wanafunzi wafurahie kujifunza moja kwa moja kutoka kwenye Biblia. Ingawa machapisho yetu mengi yameandikwa kwa njia ambayo msomaji anaweza kujifunza mwenyewe, broshua hii imekusudiwa kutumiwa kwa njia ya mazungumzo yanayoongozwa na mwalimu. Kwa hiyo, tunapomwachia mwanafunzi broshua hiyo, tunapaswa kumwonyesha funzo linavyoongozwa ili aone jinsi kujifunza habari njema za Biblia kunavyosisimua.—Mt. 13:44.
2. Tunawezaje kutumia broshua Habari Njema katika ziara ya kwanza?
2 Katika Ziara ya Kwanza: Unaweza kusema hivi: “Nimekutembelea kwa sababu watu wengi wana wasiwasi kuhusu wakati ujao. Je, unafikiri kuna wakati hali zitakuwa bora? [Mruhusu ajibu.] Biblia ina habari njema zinazoweza kutupa tumaini. Haya ni baadhi ya maswali ambayo Biblia inajibu.” Mpe mwenye nyumba broshua, na umwombe achague swali moja katika ukurasa wa nyuma. Kisha mwonyeshe jinsi funzo linavyoongozwa ukitumia fungu la kwanza katika somo alilochagua. Njia nyingine ni kumwomba mwenye nyumba achague swali linalomvutia katika somo ulilochagua, na kisha umwonyeshe jinsi broshua hiyo inavyoweza kumsaidia kupata jibu la Biblia. Ikiwa kuna video katika Tovuti ya jw.org inayohusiana na somo hilo, unaweza kumwonyesha mwenye nyumba.
3. Eleza jinsi unavyoweza kuongoza funzo kwa kutumia broshua Habari Njema.
3 Jinsi ya Kuongoza Funzo: (1) Soma swali lenye wino mzito ili kumsaidia mwenye nyumba akazie fikira wazo kuu. (2) Soma fungu. (3) Soma maandiko yenye maandishi yaliyolazwa, na uulize maswali kwa njia ya busara ili kumsaidia mwenye nyumba aone jinsi maandiko yanavyojibu swali la fungu hilo. (4) Ikiwa kuna fungu lingine chini ya swali hilo, rudia hatua ya 2 na ya 3. Ikiwa kuna video inayohusiana na swali hilo na bado hujamwonyesha mwenye nyumba, mwonyeshe mnapozungumzia fungu hilo. (5) Mwishowe, mwombe mwenye nyumba ajibu swali la fungu hilo ili uone kama ameelewa.
4. Ni nini kitakachotusaidia kutumia kwa ustadi kifaa hiki chenye thamani?
4 Elewa vizuri jinsi ya kutumia kifaa hiki chenye thamani. Tumia kifaa hiki katika kila pindi inayofaa. Kabla ya kuanza funzo, mfikirie mwanafunzi wako na njia nzuri ya kujadiliana naye kwa kutumia maandiko yaliyo katika somo hilo. (Met. 15:28; Mdo. 17:2, 3) Kadiri ustadi na uzoefu wako unavyoongezeka, ndivyo utakavyofurahia zaidi kutumia kifaa hiki kuwafundishia watu kweli!