Kuanzisha Mafunzo Katika Broshua Anataka
1 Ripoti kutoka ulimwenguni pote zaonyesha kwamba broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? ni kifaa chenye nguvu sana cha kufundishia watu kweli. Maelfu ya mafunzo ya Biblia sasa yanaanzishwa kila juma kwa kutumia broshua hii. Je, umefanikiwa kuanzisha na kuongoza funzo la Biblia katika broshua Anataka?
2 Ijapokuwa wengi wanaona ikiwa rahisi kuangusha broshua hiyo, wengine huona vigumu kujua la kusema ili kuanzisha funzo. Ni njia gani ambazo wengine wameona zikiwa zenye matokeo katika kuanzisha mafunzo ya Biblia kwa kutumia broshua Anataka? Madokezo yafuatayo yapaswa kutusaidia.
3 Onyesha Jinsi Funzo Lifanywavyo: Tunapofanya ziara ya kwanza au ziara ya kurudia, badala ya kumtolea mwenye nyumba funzo la Biblia tu, twaweza kuonyesha jinsi funzo la Biblia litakavyoongozwa. Kufanya hivyo kutaelekea kuondoa fumbo na wasiwasi wenye kuendelea ambao wenye nyumba wengi huuhusianisha na neno “funzo.” Mara tujuapo jinsi ya kulionyesha, tutaona kwamba tukitumia utangulizi sahili, twaweza kuanzisha funzo.
4 Utayarishaji Ndilo Jambo la Msingi: Shauku ya kuanzisha mafunzo ya Biblia yahusiana moja kwa moja na jinsi ambavyo tumejitayarisha vizuri. Kutayarisha mapema kutatusaidia tushinde kusitasita kokote ambako huenda tukawa nako katika kushiriki kazi ya kuongoza funzo la Biblia. Kwa kujizoeza utoaji wetu mara kadhaa, tutaufanya uwe wa namna ya maongezi zaidi, na kuweza kujieleza wenyewe kwa njia ya kiasili na kwa maneno yetu wenyewe. Hiyo itatusaidia tustarehe na pia tumfanye mwenye nyumba astarehe vilevile.
5 Unapofanya mazoezi, itasaidia kuhesabu wakati ili umjulishe mwenye nyumba utachukua muda gani kumwonyesha jinsi ya kujifunza. Baada ya kujijulisha, ndugu mmoja husema: “Nimepitia hapa ili nikuonyeshe programu yetu ya funzo la Biblia bila malipo. Huchukua muda wa dakika tano hivi kuionyesha. Je, una dakika tano?” Somo la 1 la broshua Anataka laweza kuonyeshwa kwa dakika tano hivi. Bila shaka, ni maandiko yaliyoteuliwa tu yanayoweza kusomwa kwa muda huu wa wakati, lakini kwa kumaliza somo la kwanza kwa dakika chache, mwenye nyumba ataweza kupata funzo lake la kwanza. Kisha mjulishe utakaporudi mjifunze somo la 2, utatumia dakika 15 tu.
6 Utoaji ufuatao umethibitika kuwa wenye matokeo:
◼ “Ningependa kukuonyesha njia sahili sana, hata iliyofupishwa, mtaala wa kujifunza Biblia nyumbani kwa kutumia broshua hii Mungu Anataka Tufanye Nini? Wengi wameona kwamba kwa dakika chache tu kama vile 15 kila juma kwa majuma 16, wanaweza kupata majibu yenye kuridhisha ya Kimaandiko kwa maswali haya ya Biblia ya maana.” Mwonyeshe kifupi yaliyomo. Ukifungua Somo la 1, sema: “Ukitupatia dakika tano hivi, tungependa kukuonyesha jinsi ambavyo hufanywa. Somo la 1 lina kichwa ‘Jinsi Unavyoweza Kujua Yale Ambayo Mungu Anataka.’” Kisha soma yale maswali matatu, na ueleze juu ya namba zilizo katika vifungo vya mraba. Soma fungu la 1, na umwonyeshe mwenye nyumba jinsi ya kupata jibu. Huenda mwenye nyumba akaombwa kusoma fungu la 2. Kisha sema: “Ukitegemea habari hii, ungejibuje swali hili? [Soma swali hilo tena na umruhusu mwenye nyumba atoe maelezo.] Utaona kwamba kuna maandiko yanayoambatanishwa na kila fungu. Hayo huelekeza fikira zetu kwenye jibu la Biblia kwa maswali haya. Kwa kielelezo, acha tusome 2 Timotheo 3:16, 17, tuone kama linaunga mkono jibu ulilotoa kuhusu mtungaji wa Biblia.” Baada ya kusoma fungu la 3, ukifikiria swali hilo na kusoma Yohana 17:3, vuta uangalifu wa mwenye nyumba kuelekea ujuzi ambao amepata kwa kupitia Somo la 1. Kufikia hapa waweza kufungua Somo la 2 na kusoma swali la mwisho, “Ni njia gani mbili ambazo twaweza kujifunza kumhusu Mungu?” Kisha uliza: “Ni lini utakapokuwa na dakika 15 hivi ili tuweze kujifunza Somo la 2 na kupata jibu?”
7 Ni jambo la maana kufanya mazungumzo yawe sahili na umpongeze mwenye nyumba inapowezekana. Unapopangia ziara nyingine, badala ya kuuliza kama angetaka kuendelea, mtie moyo tu afuate utaratibu huohuo kwa somo linalofuata. Mjulishe kwamba unatazamia kwa hamu kurudi. Wahubiri wengine wamejitolea kufanya somo moja kupitia simu kama ilikuwa vigumu kupanga wakati. Pia waweza kumtia moyo mwanafunzi aiweke broshua yake mahali salama, panapofaa, ili aweze kuipata kwa urahisi unaporudi.
8 Azimia: Ijapokuwa msingi wa mafanikio ni utayarishaji, lazima tuazimie kuliendeleza. Kufundisha somo moja kwa dakika chache kwaweza kuwa jambo gumu, kwa hiyo, azimia kujizoeza utoaji huo mara nyingi iwezekanavyo ili ufanye funzo hilo kwa ufasaha. Jaribu kumwonyesha jinsi ya kujifunza, mtu yeyote unayempata mlangoni, kivivi hivi, na kutoa ushahidi kupitia simu. Ikiwa unaona ugumu kuanzisha funzo la Biblia, usivunjike moyo. Mafanikio katika kuanzisha mafunzo ya Biblia huhitaji azimio na tamaa ya moyo mweupe ya kuwajulisha wengine kweli.—Gal. 6:9.
9 Kwa kutumia madokezo haya, wewe pia waweza kuwa na pendeleo la kumsaidia mtu fulani aingie kwenye barabara iongozayo kwenye uhai, kwa kuanzisha na kuongoza funzo la Biblia katika broshua Anataka.—Mt. 7:14.