Je, Unatumia Broshua Anataka Kuanzisha Mafunzo?
1 Je, umetambua kwamba ukizungumza na mtu kwa ukawaida kuhusu Biblia na kufuata utaratibu fulani ukitumia mojawapo ya vichapo vinavyopendekezwa, hata ikiwa ni kwa muda mfupi, unaongoza funzo la Biblia? Ndiyo, hata kama unafanya hivyo ukiwa umesimama mlangoni au kwenye simu. Kwa nini usijitahidi kuanzisha funzo la Biblia ukitumia broshua Anataka mwezi wa Mei na Juni?
2 Jitayarishe Ili Upate Matokeo Mazuri: Unapotoa broshua Anataka, fikiria vizuri kile unachotaka kuzungumzia. Ikiwa unafanya ziara ya kurudia, fikiria yale mliyozungumzia wakati uliopita. Jiulize hivi: ‘Ni mafungu gani katika broshua hii ninayoweza kukazia ili kuendeleza mazungumzo yatakayoelekeza kwenye funzo la Biblia?’ Ikiwa unaenda nyumba kwa nyumba, fikiria mambo yatakayompendeza kijana, mtu mzee, mwanamume, au mwanamke. Zungumzia habari kuu za broshua hiyo, na uchague somo litakaloamsha upendezi wao. Baada ya kuchagua utangulizi utakaotumia, jizoeze mara kadhaa. Hiyo ndiyo mojawapo ya njia za kufanikiwa.
3 Nyongeza ya Huduma Yetu ya Ufalme ya Januari 2002 ina madokezo manane yanayopatikana chini ya kichwa “Madokezo ya Namna ya Kutoa Broshua Anataka.” Sanduku linalosema “Njia ya Moja kwa Moja” laonyesha jinsi ya kutumia broshua hii kuanzisha mafunzo. Unaweza kutumia dokezo la kwanza ifuatavyo:
◼ “Je, unajua kwamba kwa dakika chache tu, unaweza kupata jibu la swali muhimu katika Biblia? Kwa mfano, kwa nini kuna dini nyingi sana zinazodai kuwa za Kikristo? Je, umewahi kujiuliza jambo hilo?” Baada ya mtu huyo kujibu, fungua somo la 13 na mzungumzie mafungu mawili ya kwanza. Wakati ukiruhusu, soma na kuzungumzia andiko moja au mawili. Kisha soma swali la mwisho lililo juu ya ukurasa huo, na useme: “Sehemu inayobaki ya somo hili yakazia mambo matano yanayoitambulisha dini ya kweli. Ningependa kurudi ili tuyachunguze pamoja.”
4 Endelea Kujitahidi: Tumia kila fursa kuanzisha funzo la Biblia ukitumia broshua Anataka. Omba baraka za Yehova. (Mt. 21:22) Ukiendelea kujitahidi, unaweza kupata shangwe ya kusaidia mtu akubali habari njema!