Kwenda Sambamba na Ongezeko la Kitheokrasi
1 Katika siku za Nehemia, kulikuwa na uhitaji wa ujenzi kwa sababu kuta za kinga za Yerusalemu zilikuwa zimeharibika. Nehemia alitoa uongozi wenye kukata maneno, na watu waliitikia kwa kusema, “Haya! na tuondoke tukajenge.”—Neh. 2:18.
2 Hali kadhalika leo, watu wa Yehova wanaitikia uhitaji wa kujenga na kurekebisha Majumba ya Ufalme. Majumba ya Ufalme mengi yanahitaji kurekebishwa na kudumishwa vizuri zaidi, na majumba mengi mapya yahitaji kujengwa ili kuupa nafasi upanuzi wa haraka wa tengenezo la Yehova. Sawa na vile Nehemia alivyopanga kazi ya kujenga upya kuta za Yerusalemu, ndivyo “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” amepanga kuwe na programu ya ujenzi leo.—Mt. 24:45.
3 Sosaiti yaendelea kuyapa makutaniko mikopo ili kuyasaidia kujenga Majumba ya Ufalme. Michango ya ukarimu ya akina ndugu imewezesha Sosaiti igawie makutaniko yenye uhitaji mkubwa fedha. Itikio hili la kutegemeza ongezeko la kitheokrasi limekuwa lenye kutia moyo sana.—1 The. 4:9, 10.
4 Halmashauri za Ujenzi za Kimkoa pia zimepata baraka za Yehova. Kwa sasa, kuna Halmashauri za Ujenzi za Kimkoa saba zinazofanya kazi katika Afrika Mashariki. Miradi mingi inayohusu ujenzi wa Majumba ya Ufalme mapya au urekebishaji wa majengo yaliyopo tayari, kwa sasa inaendelezwa.
5 Akina ndugu wanaofanya kazi katika Halmashauri za Ujenzi za Kimkoa wanapasa kupongezwa kwa jitihada zao za bidii katika kukabiliana na uhitaji unaoongezeka wa Majumba ya Ufalme. Sosaiti imeandaa mwongozo ili kusaidia kupitia ramani za ujenzi. Hivyo, halmashauri hizi ndizo zinazofaa kusaidia wazee katika kuchora ramani ya Jumba la Ufalme ambalo litakuwa la kiasi na lenye kutumika na ambalo litafanya rasilimali zilizotolewa zitumiwe kwa hekima. Itakuwa vizuri mabaraza ya wazee kufikiria mambo kwa uangalifu, wakinufaika kikamili kutokana na mambo yaliyoonwa na wazee wazoefu waliowekwa kutumikia kwenye Halmashauri za Ujenzi za Kimkoa.—Luka 14:28-30.
6 Kuna Mengi Zaidi ya Kufanya: Ijapokuwa Majumba ya Ufalme mengi yamejengwa tayari, bado kuna mengi ya kutimizwa ili kwenda sambamba na ongezeko la kitheokrasi. Tayari kuna makutaniko mawili au matatu yanayokutania ndani ya baadhi ya Majumba ya Ufalme yaliyojengwa hivi karibuni. Hii yamaanisha kwamba upesi jumba jingine litahitajiwa ili kukabiliana na ukuzi katika maeneo hayo.
7 Ni jambo la Kimaandiko kutoa utegemezo wa kifedha. Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “mchango” humaanisha “fungu takatifu.” (Kut. 25:2, NW Reference Bible, kielezi-chini) Wakristo hutamani ifaavyo kuchangia wakati, nishati, na mali za kimwili ili kuendeleza masilahi za Ufalme. Hatumtajirishi Yehova kwa michango yetu tunayotoa kwa kazi yake, bali katika njia hii twaonyesha kwamba twampenda, naye hubariki wale ambao hutoa michango kwa hiari.—1 Nya. 29:14-17; Mit. 3:9.
8 Kwenye 2 Wakorintho 8:12 Paulo aliandika hivi: “Kwa maana ikiwa utayari upo kwanza, hukubalika hasa kulingana na alicho nacho mtu, si kulingana na kile ambacho mtu hana.” Wote wanaweza kutiwa moyo waweke kando kitu fulani kwa ukawaida kulingana na uwezo na tamaa yao. (Linganisha 1 Wakorintho 16:1-4.) Tertullian aliandika hivi kuhusu kutaniko la Kikristo la mapema: “Kila mtu mara moja kwa mwezi huleta sarafu za kiasi—au wakati wowote apendapo, na ikiwa tu anataka, na kama anaweza; kwa maana hakuna anayelazimishwa; ni toleo la hiari.” Tofauti na dini nyingi leo zinazopitisha sahani ya kuchangisha ili kudai michango, matoleo yote ya kimwili katika kutaniko la Kikristo yanatolewa kwa hiari kutoka moyoni. (2 Kor. 9:7) Kuhusu hilo Huduma ya Ufalme Yetu ya Desemba 1989 ilieleza hivi: “[Makutaniko] na mizunguko mingi imesaidia kwa ukawaida kwa kupitisha maazimio yanayotoa idhini fedha zichangwe kwa Sosaiti.” Hata ingawa kutaniko hufuata utaratibu huu sanduku la mchango la Hazina ya Jumba la Ufalme lililowekwa mahali pafaapo katika Jumba la Ufalme litawezesha watu mmoja-mmoja wanaotaka kufanya hivyo wachangie hazina hiyo kwa hiari. Hata hivyo, hatupaswi kufuata njia zisizo za kitheokrasi kutoa michango ya fedha, kama vile kufanya ukaguzi au ukusanyaji kwa kutumia kitabu cha kuandikia au njia yoyote ile ambayo yaweza kuwafanya wahubiri wahisi wamelazimishwa kutoa michango kwa ajili ya kazi ya Ufalme.
9 Twatumaini kwamba akina ndugu watachochewa kutoa michango kwa hiari kupatana na maandiko, na Yehova kwa kweli ameendelea kubariki roho ya hiari tunayoona miongoni mwa watu wake.—Zab. 110:3.