Tumia Broshua Mbalimbali Katika Huduma Yako
1 Leo watu wanapendezwa na mada mbalimbali. Unapojihusisha na utumishi wa shambani wakati wa Julai, unaweza kuwa na broshua kadhaa tofauti katika lugha mbalimbali, ukitumia moja hususa itakayovutia watu katika eneo. Pengine utataka kujaribu mojapo utoaji huu mbalimbali:
2 Kwa kutoa broshua “Serikali Itakayoleta Paradiso,” unaweza kuuliza:
◼ “Wafikiri ulimwengu ungefananaje ikiwa Mungu pekee ndiye angekuwa mtawala? [Ruhusu itikio.] Kutwaa kwa Mungu utawala wa dunia ndilo hasa tunaloomba tunaposali ile Sala ya Bwana au Baba Yetu, ambayo Yesu Kristo alitufundisha. [Fungua ukurasa 3, na usome fungu la kwanza, linalonukuu Mathayo 6:10.] Ikiwa ungependa kuishi katika ulimwengu kama huo, unapaswa kusoma broshua hii.” Iache.
3 “Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa” yaweza kutolewa kwa njia hii:
◼ “Je, wafikiri siku itafika wakati wowote ambapo hakuna hata mmoja wetu atakapopoteza mpendwa katika kifo? [Ruhusu itikio.] Broshua hii iliyoandikwa vizuri imefariji mamilioni kwa ahadi yenye uhakika ya Biblia kwamba siku hiyo inakuja wakati ujao karibuni. [Fungua ukurasa 5, na usome fungu la tano, ukitia ndani 1 Wakorintho 15:21, 22. Kisha fungua kielezi kwenye ukurasa 30.] Hapa mchoraji ametilia mkazo shangwe tunayoweza kuona tukikaribisha wapendwa wetu waliokufa katika ufufuo. Lakini mandhari hiyo ya furaha itatendeka wapi? Broshua hii itakuonyesha jibu la Biblia kwa swali hilo.” Broshua ikikubaliwa, unaweza kuongezea: “Ningependa kurudi baadaye ili tuzungumzie mada hii zaidi.”
4 Unaweza kutoa broshua “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya,” kwa kutumia mfikio huu wa moja kwa moja ili kuanzisha funzo la Biblia:
◼ “Watu wengi wana maswali kuhusu Biblia. Huenda umejiuliza kuhusu jibu la mojapo maswali haya. [Fungua ukurasa 30.] Swali hili la mwisho limechochea kupendezwa kwa wengi: ‘Unaweza kujitayarishaje kuja kupata uzima wa milele katika Paradiso?’” Ukizungumzia mafungu 57-58 kwenye kurasa 29-30 na usome Ufunuo 21:3, 4, utakuwa umeweka msingi wa kuanza funzo la Biblia. Malizia kwa kuacha broshua na kupanga ziara ya kurudia utakapoweza kuzungumza juu ya maswali yale mengine.
5 Unaweza kutaka kujaribu utoaji huu sahili ukiwa na broshua “Jina la Mungu Litakaloendelea Milele”:
◼ “Mojapo mambo ya kwanza niliyojifunza katika Biblia lilikuwa jina la Mungu. Je, wewe walijua? [Ruhusu itikio.] Acha nikuonyeshe. Liko hapa katika Biblia kwenye Zaburi 83:18. [Soma.] Broshua hii yaonyesha jinsi jina la Mungu, Yehova, lipatikanavyo katika lugha nyingi tofauti. [Onyesha sanduku kwenye ukurasa 8.] Ikiwa ungependa kujifunza zaidi kuhusu Yehova na makusudi yake, unapaswa kusoma broshua hii.” Mpe mwenye nyumba hiyo broshua.
6 Tukiwa na broshua hizo mbalimbali za kutumia, kwa hakika tumetayarishwa vema ‘kuwahubiri wanyenyekevu habari njema.’—Isa. 61:1.