Mwapaswa Kuwa Watu wa Namna Gani?
1 Siku ya kutozwa hesabu yakaribia kwa wanadamu wote. Biblia huiita “siku ya Yehova.” Ni wakati ambapo hukumu ya kimungu itatekelezwa dhidi ya waovu; pia ni wakati wa ukombozi kwa waadilifu. Watu wote walio hai wakati huo watatozwa hesabu ya jinsi walivyoishi maisha yao. Akiwa na hilo akilini, Petro atokeza swali hili lenye kuchunguza: “Mwapaswa kuwa watu wa namna gani”? Yeye akazia umaana wa ‘matendo matakatifu ya mwenendo, vitendo vya ujitoaji kimungu, na kuiweka akilini siku ya Yehova,’ na vilevile uhitaji wa kuwa ‘bila doa, bila waa, na katika amani.’—2 Pet. 3:11-14, NW.
2 Matendo Matakatifu ya Mwenendo na Vitendo vya Ujitoaji Kimungu: Matendo matakatifu hutia ndani kazi zenye kielelezo kizuri ambazo huheshimu kanuni za Biblia. (Tito 2:7, 8) Mkristo apaswa kuepuka mwenendo wa kilimwengu ambao husukumwa na ubinafsi, na tamaa za kimwili.—Rum. 13:11, 14.
3 “Ujitoaji kimungu” wafafanuliwa kuwa “ujihusishaji wa kibinafsi pamoja na Mungu, utokanao na moyo unaochochewa na uthamini wenye kina kirefu kwa sifa zake zenye kuvutia.” Bidii yetu katika huduma ni njia yenye kutokeza tunayoonyesha sifa hii. Mtazamo wetu katika kuhubiri ni zaidi ya wajibu tu; huo hutokana na upendo wenye kina kirefu zaidi kwa Yehova. (Mk. 12:29, 30) Tukichochewa na upendo kama huo, twaona huduma yetu kuwa wonyesho wa maana wa ujitoaji kimungu wetu. Kwa kuwa ujitoaji wetu wapaswa uwe wa daima, ushiriki wetu katika kuhubiri wapaswa kuwa wenye kudumu. Wapaswa kuwa sehemu muhimu ya ratiba ya utendaji wetu wa kila juma.—Ebr. 13:15.
4 Kuendelea “kukumbuka” siku ya Yehova kwamaanisha kuiweka mbele ya mawazo yetu ya kila siku, bila kuiondoa kamwe akilini na kuitupilia mbali iwe isiyo ya maana sana. Humaanisha kuweka masilahi ya Ufalme kwanza maishani mwetu.—Mt. 6:33.
5 Bila Doa, Bila Waa, na Katika Amani: Tukiwa sehemu ya umati mkubwa, ‘tumefua mavazi yetu, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo.’ (Ufu. 7:14) Basi kuwa bila “doa” humaanisha, kwamba ni lazima kwa uimara tulinde maisha yetu yaliyo safi na wakfu dhidi ya kuchafuliwa na vitu visivyo safi vya ulimwengu. Twajiweka wenyewe tukiwa “bila waa” kwa kukataa kuruhusu ufuatiaji wa vitu vya kimwili visivyo vya kimungu uharibu utu wetu wa Kikristo. (Yak. 1:27; 1 Yoh. 2:15-17) Twaonyesha kwamba twaishi “katika amani” kwa kuonyesha “amani ya Mungu” katika kushughulika kwetu pamoja na wengine.—Flp. 4:7; Rum. 12:18; 14:19.
6 Tukilinda kwa mafanikio dhidi ya kuchafuliwa kwa kilimwengu, ‘hatutafuatisha namna ya mfumo huu wa mambo,’ ambao umelaaniwa na Yehova. Badala yake, kazi zetu nzuri zitasaidia wengine waone tofauti “kati ya yeye amtumikiaye Mungu na yeye asiyemtumikia.”—Rum. 12:2, NW; Mal. 3:18.
7 Baadaye mwakani tutahudhuria “Wasifaji Wenye Shangwe” Mkusanyiko wa Wilaya, na bila shaka chakula cha kiroho chenye kuburudisha kitazidisha tamaa yetu ya kuonyesha ujitoaji kimungu wetu. Wengi walio wapya wanashiriki tamaa hii. Twaweza kuwa baraka kwa kuwasaidia kushiriki katika utumishi wa shambani wakati wa Agosti.
8 Jina la Yehova latukuzwa, kutaniko laimarishwa, na wengine wananufaishwa tunapodumisha “matendo mazuri.” (1 Pet. 2:12) Sikuzote na tuwe namna ya mtu huyo.