Iweni Wafundishaji wa Neno la Mungu —Mkitumia Broshua
1 Kila mtumishi wa Yehova aliyejiweka wakfu ana daraka la kushiriki katika kazi ya kufundisha wengine Neno la Mungu. Uzito wa daraka hili huwa wazi tukithamini kwamba ndiye mwenye mamlaka yote mbinguni na duniani ambaye ametupatia agizo la ‘kuwafanya mataifa yote kuwa wanafunzi, . . . na kuwafundisha.’ (Mt. 28:18-20) Kwa hiyo, kushiriki kuhubiri habari njema kwatutaka tuwe wafundishaji!—2 Tim. 2:2.
2 Wakati wa Agosti tunaweza kutumia stadi zetu za kufundisha tutoapo broshua. Twaweza kutwaa baadhi ya mawazo yenye kupendeza ya Kimaandiko kutoka kwayo na kutayarisha maelezo machache yatakayotusaidia tuanzishe mazungumzo.
3 Unapotoa broshua “Je! Kweli Mungu Anatujali?” waweza kusema:
◼ “Tumetembelea wengi wa majirani wako na kupata kwamba wanahangaishwa na ongezeko la ghafula la uhalifu, uharamia, na ujeuri. Kulingana na maoni yako, kwa nini jambo hili limekuwa tatizo? [Ruhusu itikio.] Ni jambo lenye kupendeza zaidi kwetu kwamba Biblia ilitabiri hili lingetukia. [Soma 2 Timotheo 3:1-3.] Ona kwamba jambo hili lingetokea ‘siku za mwisho.’ Yamaanisha kwamba jambo fulani liko karibu kufikia mwisho. Unafikiri hilo ni nini?” Ruhusu itikio. Fungua ukurasa 22, onyesha kielezi, na uzungumzie andiko moja au mawili yaliyonukuliwa kwenye ukurasa huo. Fanya mipango ya kurudi baadaye ili ueleze ni kwa nini twaamini baraka hizi ziko karibu.
4 Huenda ukataka kutumia mfikio huu unapotoa broshua “Ni Nini Lililo Kusudi la Uhai?—Wewe Waweza Kulipataje?”:
◼ “Watu wengi huona ugumu katika kujaribu kupata kusudi halisi la kuishi. Ijapokuwa wachache hufurahia furaha iliyo na mipaka, walio wengi huishi maisha yaliyojaa matamauko na kuteseka. Unafikiri hivi ndivyo Mungu alivyokusudia tuishi? [Ruhusu itikio.] Biblia huonyesha kwamba Mungu ataka tuishi katika ulimwengu kama huu.” Onyesha kielezi kwenye ukurasa 21, kisha ufungue kurasa 25 na 26, mafungu 4-6, na ueleze kile ameahidi. Tokeza swali hili kwa ajili ya mazungumzo unaporudi: “Twaweza kuwaje na uhakika kwamba Mungu atatimiza ahadi zake?”
5 Waweza kutoa broshua “Furahia Milele Maisha Duniani!” kwa kuonyesha picha kamili iliyo mbele na nyuma ya majalada na kuuliza:
◼ “Je, ungependa kuishi katika ulimwengu kama huu uliojaa watu wenye furaha? [Ruhusu itikio.] Biblia hutuambia kwamba Mungu hupenda watu naye ataka waishi milele kwa furaha kwenye dunia hii.” Fungua picha namba 49, na usome mojapo Maandiko yaliyowekwa kando. Kisha, onyesha picha namba 50, na ueleze jambo ambalo lazima tufanye ikiwa twataka kuishi katika Paradiso hii. Jitolee urudi mzungumze ni kwa nini imani katika Yesu Kristo ni muhimu sana.
6 Yehova anapendezwa tufanyapo ‘maendeleo yetu yawe dhahiri kwa kufundisha kwetu.’ (1 Tim. 4:15, 16) Broshua zetu zaweza kuwa msaada kwetu kwelikweli katika jitihada za kusaidia wale wanaotamani kusikia “habari njema ya mambo mema.”—Isa. 52:7.