Weka Akili Yako Ikiwa Imekazwa juu ya Mambo Yaliyo Juu
1 Ikieleza juu ya kizazi kinachotuzunguka na mtazamo wacho kuelekea wakati ujao, makala moja katika The New York Times la Desemba 31, 1994, ilisema hivi: “[Watu] wanahofia wakati ujao. Wanauhofia kwa habari ya kazi, kwa habari ya maradhi, kwa habari ya uchumi, kwa habari ya hali za ulimwengu.” Kokote tutazamapo, kuna hisia ya kukosa uhakika juu ya maisha. Huduma yetu tukiwa Mashahidi wa Yehova hutufanya tukutane kila siku na watu wanaohisi hivyo. Ingawa twakabili matatizo ayo hayo wanayokabili, imani na uhakika wetu katika ahadi zilizo hakika za Neno la Mungu hutuwezesha kuwa na mtazamo ulio tofauti sana juu ya maisha na wakati ujao wa wanadamu.—Isa. 65:13, 14, 17.
2 Maoni yetu mazuri na mtazamo wetu wenye tumaini lililo hakika hufanya watu wengi wenye mioyo ya haki wasikilize ujumbe tunaowaletea. Watu wengi mmoja-mmoja wanaohisi mshuko-moyo na kulemewa huliona kuwa jambo lenye kufariji kuongea nasi. Wengine hukubali kujifunza Biblia pamoja nasi, kwa sababu wanapenda kile wanachosikia. Hata hivyo, nyakati nyingine, huenda watu wakataka kwanza kuongea juu ya matatizo yao ya kibinafsi. Ingawa wakati fulani waweza kutumiwa katika kusikiliza mahangaiko ya mtu ya kibinafsi, hatupaswi kusahau lengo letu, ambalo ni kufundisha watu zile kweli chanya za Neno la Mungu.
3 Twataka kuwa wenye huruma kuelekea wale ambao wamelemewa. Yesu aliweka kielelezo aliposema, kama ilivyorekodiwa kwenye Mathayo 11:28: “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa.” Twataka kuwatia watu moyo kwa namna iyo hiyo. Hata hivyo, ebu ona umalizio wa mstari 28 (NW), Yesu alisema hivi: “Nitawaburudisha nyinyi.” Hiyo yapaswa iwe shabaha yetu. Twafanya hivyo kwa kushiriki zile ahadi zenye kuburudisha kutoka Neno la Mungu. Kuwa msikilizaji mzuri kwaonyesha kupendezwa na kuhangaika kwetu kibinafsi na ni muhimu ili tutimize utume wetu wa kuhubiri habari njema ya Ufalme, tukisaidia wengine kung’amua kwamba Ufalme ndio dawa pekee ya hakika kwa matatizo yote ya wanadamu.—Mt. 24:14.
4 Kazi yetu si ile ya wanatiba stadi. Badala ya hivyo, ni kama vile mtume Paulo alivyoeleza, kama ilivyoonyeshwa kwenye 1 Timotheo 4:6, ni huduma ambayo hukazia “mafundisho mazuri,” mafundisho yanayopatikana katika Neno la Mungu. Wale wenye matatizo ya kibinafsi au ya kihisiamoyo wahitaji kutiwa moyo wamtegemee Yehova. Uwafundishe kuweka “akili [zao] zikiwa zimekazwa juu ya mambo yaliyo juu”—mambo yanayohusiana na tumaini la Ufalme. (Kol. 3:2, NW) Watu wakikazia uangalifu Neno la Mungu, wao waweza kujengwa kupitia uvutano walo wenye nguvu maishani mwao.—Ebr. 4:12.
5 Kwa hiyo mradi wetu ni kusaidia watu wakaze fikira zao juu ya mambo yaliyo ‘ya uadilifu, safi kiadili, ya kupendeka, na ya kustahiki sifa.’ (Flp. 4:8, NW) Wakikaza uangalifu juu ya tumaini la Ufalme, watabarikiwa katika njia ileile tunayobarikiwa. Wao pia watakuwa na shangwe inayotokana na kujua kwamba hatimaye Yehova atasuluhisha matatizo yao yote kupitia Ufalme wake.—Zab. 145:16.