Aprili 6, 1996: Itikio Zuri Ajabu!
Kwenye Huduma ya Ufalme Yetu ya Februari 1996 uangalifu ulielekezwa kwenye siku ya pekee ya magazeti iliyopangiwa Jumamosi, Aprili 6. Wito ulitolewa kwa watangazaji wote katika Afrika Mashariki washiriki kikamili katika siku hii ya pekee ya magazeti. Tulipoikaribia siku hiyo mtu aliweza kuhisi mchachawo na idili ikienea makutanikoni. Akina ndugu walipanga mambo ya kibinafsi na utendaji ili kuhakikisha watashiriki katika sehemu fulani ya utendaji wa magazeti wakati wa siku hiyo.
Matokeo yalikuwa mazuri ajabu! Katika nchi zote kulikuwa na ongezeko katika maangusho ya magazeti wakati wa Aprili kuanzia asilimia 85 katika Kenya hadi zaidi ya asilimia 100 katika nchi nyinginezo. Katika Kenya tuliangusha jumla ya magazeti 83,175. Hii ni idadi ya juu zaidi kwa mwezi moja katika historia ya kazi hii katika Kenya. Vema! Maangusho ya mwezi huo katika Rwanda yalishinda mwaka uliopita kwa asilimia 30; katika Tanzania karibu maradufu ya Aprili 1995, na katika Uganda karibu mara nne kuliko Aprili mwaka mmoja uliopita. Bora kama nini! Jumla ya magazeti 144,938 yaliangushwa katika nchi zote wakati wa mwezi huo. Kwa kweli ni kazi iliyofanywa vema kama nini, wapiga-mbiu wa Ufalme!
Makutaniko mengi yalimaliza ugavi wayo wa kawaida wa magazeti pamoja na matoleo mengine ya zamani ambayo yalikuwa yamerundamana katika akiba ya kutaniko. Makutaniko jirani yalisaidiwa kugawanya ugavi wao. Kwa hiyo, sasa huu huenda ukawa wakati mzuri kwa wazee kupitia agizo la magazeti la kutaniko ili kujua kama kuna magazeti ya kutosha ya kutumia katika huduma na kwa ajili ya funzo. Makutaniko yatapanga angalau siku moja ya magazeti kwa juma iwe ni nyumba hadi nyumba, sokoni, katika eneo la biashara au ushahidi wa barabarani. Ndugu wapendwa, endeleeni kutumia vizuri magazeti yetu yenye kuokoa uhai ambayo ni kama ‘hekima ipazayo sauti yake katika njia kuu.’—Mit. 1:20.