Tembea kwa Imani
1 Mamilioni ya watu hukazia maisha zao juu ya mali zao za kimwili, wakitumaini kipumbavu nguvu zenye kudanganya za utajiri. (Mt. 13:22) Wao hujifunza somo gumu mali zao zinapopotea au zinapoibwa au zinapokuwa bila faida kubwa. Twahimizwa tutafute mwendo wenye hekima, tushindanie hazina za kiroho. (Mt. 6:19, 20) Hili hutia ndani ‘kutembea kwa imani.’—2 Kor. 5:7, NW.
2 Neno “imani” latafsiriwa kutoka neno la Kigiriki ambalo hutoa wazo la uhakika, itibari, sadikisho imara. Kutembea kwa imani humaanisha kukabili hali ngumu tukiwa na uhakika katika Mungu, tukitumaini uwezo wake wa kuongoza hatua zetu na utayari wake wa kutimiza mahitaji yetu. Yesu aliweka kielelezo kikamilifu; alikaza fikira juu ya mambo yaliyokuwa ya maana kwelikweli. (Ebr. 12:2) Vivyo hivyo, sisi twahitaji kukaza mioyo yetu juu ya mambo yasiyoonekana, ya kiroho. (2 Kor. 4:18) Lazima sikuzote tuwe tukikumbuka kwamba uhai wetu wa sasa hauna uhakika na kukiri utegemeo wetu wote kwa Yehova.
3 Lazima tuwe na usadikisho imara kwamba Yehova anatuongoza kupitia tengenezo lake lionekanalo chini ya mwelekezo wa “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Mt. 24:45-47) Twaonyesha imani yetu ‘tunapowatii wenye kuongoza’ kutanikoni. (Ebr. 13:17) Kufanya kazi kwa unyenyekevu tukishirikiana na mpango wa kitheokrasi huonyesha itibari yetu katika Yehova. (1 Pet. 5:6) Twapaswa kuchochewa kuunga mkono kwa moyo wote kazi ambayo tengenezo limepewa liifanye. Kufanya hivi kutatuvuta karibu na ndugu zetu kwa kifungo chenye nguvu cha upendo na muungano.—1 Kor. 1:10.
4 Jinsi ya Kuimarisha Imani: Hatupaswi kuruhusu imani yetu iwe bila maendeleo. Twahitaji kujitahidi sana ili tuiimarishe. Ukawaida katika funzo, sala, na hudhurio la mikutano utatusaidia tuimarishe imani yetu ili iweze kushinda jaribio lolote kwa msaada wa Yehova. (Efe. 6:16) Je, umesitawisha kawaida nzuri ya usomaji wa Biblia wa kila siku na utayarishaji kwa ajili ya mikutano? Je, sikuzote wewe hutafakari yale unayojifunza, na kumfikia Yehova kwa sala? Je, ni zoea lako kuhudhuria mikutano yote na kuishiriki fursa itokeapo?—Ebr. 10:23-25.
5 Imani yenye nguvu huthibitishwa na matendo mema. (Yak. 2:26) Njia moja bora zaidi ya kuonyesha imani yetu ni kwa kutangaza tumaini letu kwa wengine. Je, wewe hutafuta fursa za kushiriki habari njema? Je, hali zako zaweza kurekebishwa ili zikuwezeshe kufanya mengi zaidi katika huduma? Je, wewe hutumia madokezo tunayopokea ili kuboresha na kuifanya huduma yetu iwe yenye matokeo? Je, wewe huweka miradi ya kibinafsi ya kiroho na kujitahidi kuifikia?
6 Yesu alionya juu ya kujiingiza kupita kiasi katika mambo ya kila siku ya maisha na kuruhusu mapendezi ya kimwili au ya ubinafsi yafifishe mtazamo wetu wa kiroho. (Luka 21:34-36) Twapaswa kuangalia sana jinsi tunavyotembea ili kuepuka kuharibikiwa imani yetu. (Efe. 5:15; 1 Tim. 1:19) Sisi sote twatumaini kwamba hatimaye tutaweza kutangaza kwamba ‘tumepiga vita vilivyo vizuri, mwendo tumeumaliza, Imani tumeilinda.’—2 Tim. 4:7.