“Msaada Katika Wakati Ufaao”
1 Inaburudisha kama nini kupokea msaada hasa wakati tunapouhitaji! (Ebr. 4:16) Kwenye “Wajumbe wa Amani ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya, tulipata shangwe tulipopewa maandalizi mawili ya pekee ya msaada katika wakati ufaao hasa.
2 Kitabu kipya, Siri ya Kupata Furaha ya Familia, kilikuja katika wakati ufaao. Hicho hukazia mambo manne muhimu yanayoendeleza maisha ya familia yenye furaha: (1) Kujidhibiti, (2) utambuaji wa ukichwa, (3) mawasiliano mazuri, na (4) upendo. Onyo la upole linalotolewa katika kitabu Furaha ya Familia litasaidia familia zote zinazolitumia kupata amani ya kimungu. Wekeni kando wakati mkisome kitabu hicho kipya na kujifunza pamoja katika familia. Fahamu vizuri sehemu zacho ili uweze kukitumia kwa matokeo unapokitoa kwa watu wote.
3 Ile broshua mpya, Mungu Anataka Tufanye Nini?, imekuja kwa wakati unaofaa ili kusaidia kuharakisha kazi ya kufanya wanafunzi. Ingawa yaweza kutumiwa hasa kusaidia watu wenye uwezo mdogo wa kusoma, watu walio wazima wengi na watoto wachanga wenye elimu pia watanufaika kutokana na maelezo yayo sahili ya mafundisho ya msingi ya Biblia. Huenda ikawa ndilo jambo linalohitajiwa hasa kuanzisha funzo ambalo ni hatua ya kuelekea kitabu Ujuzi. Andalizi hili kwa hakika litasaidia wengi zaidi wathamini jinsi wanavyoweza kubarikiwa sana kwa kufanya yale ambayo Mungu anataka.
4 Daudi alionyesha vizuri maelekeo yetu alipojulisha wazi kwamba ‘hakupungukiwa na kitu, nafsi yake ilihuishwa, na kikombe chake kilifurika!’ (Zab. 23:1, 3, 5) Twatazamia kwa shangwe kupeleka msaada huu mzuri ajabu wa kiroho kwa wengine wengi wanaotamani kwa unyoofu kujua na kumtumikia Mungu wa kweli, Yehova.