Wanatakwa—Mapainia-Wasaidizi 2,500
Je, Waweza Kuwa Painia-Msaidizi Katika Machi? Aprili? Mei?
1 “Wahubiri 1,000 Watakwa” hicho kilikuwa kichwa cha makala iliyochapishwa katika toleo (la Kiingereza) la Mnara wa Mlinzi la Aprili 1881. Ilikuwa na ombi kwa wanaume na wanawake wote walio wakfu, “ambao Bwana amewapa ujuzi juu ya kweli Yake,” watumie wakati wowote walio nao kushiriki katika kueneza kweli za Biblia. Wale ambao wangeweza kutoa nusu ya wakati wao au zaidi kwa kazi ya Bwana walitiwa moyo wajitolee wawe waeneza-evanjeli makolpota, yaani, watangulizi wa mapainia wa leo.
2 Ijapokuwa nyakati zimebadilika tangu miaka ya 1800, jambo moja ladumu kuwa lilelile—watumishi wa Mungu walio wakfu wanataka kuendelea kutumia wakati mwingi iwezekanavyo katika kueneza habari njema. Kutumikia wakiwa mapainia-wasaidizi husaidia watangazaji wa kutaniko kuboresha matokeo yao wanapotoa jitihada ya ziada katika huduma ya Ufalme.—Kol. 4:17; 2 Tim. 4:5.
3 Tangu mwanzo wayo, upainia msaidizi umefurahiwa na mamia ya maelfu ya ndugu na dada. Idili ya sehemu hii ya huduma ya painia iliongezeka kwa kadiri ya kwamba jumla ya mapainia-wasaidizi 2,175 ilifikiwa katika nchi zilizo chini ya ofisi yetu ya tawi. Jumla ya vilele vya mapainia-wasaidizi katika kila nchi iliyo chini ya ofisi yetu ya tawi ni: Kenya: 954; Rwanda: 566; Sudan: 96; Tanzania: 412 na Uganda: 147. Kukiwa na ongezeko hilo zuri katika watangazaji chini ya ofisi yetu ya tawi, twahisi kwamba mradi wa mapainia-wasaidizi 2,500 wakati wa masika ya 1997 utawezekana.
4 Twakutia moyo uwe na mradi wa upainia msaidizi mwezi mmoja au zaidi miezi ya Machi, Aprili, na Mei. Kwa nini tutie ndani Machi? Kwa sababu mwaka huu Ukumbusho wa kifo cha Kristo utakuwa Jumapili, Machi 23. Hakuna njia bora zaidi tunayoweza kutumia majuma yanayotangulia Ukumbusho kuliko kushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri Ufalme ambayo Bwana wetu na Mwokozi, Yesu Kristo, alianzisha. Tunapotoa ushahidi mwingi sana katika Machi, twaweza kualika watu wengi wenye kupendezwa wajiunge nasi kuadhimisha kifo cha Kristo. Pia Machi utakuwa mwezi wa pekee kwa kuwa, kwa mara ya kwanza, tutakuwa tukitoa kitabu kipya, Siri ya Kupata Furaha ya Familia. Kwa kuongezea, mwezi wa Machi huwa na Jumamosi tano na Jumapili tano, zikiruhusu utendaji wa mwisho-juma mwingi katika utumishi wa shambani. Bila shaka, wakati wa miezi ya Aprili na Mei, jitihada ya kuendelea katika huduma itaturuhusu kufuatia kupendezwa kulikopatikana na kuanzisha mafunzo mapya ya Biblia nyumbani, tukitumia broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? Pia tutatimiza eneo letu kikamili, hasa kwenye miisho-juma, tukiwa na matoleo ya karibuni ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!
5 Ni Nani Anayestahili Kuwa Painia-Msaidizi?: Tumefanywa Tengenezo Tutimize Huduma Yetu, ukurasa wa 113, chaeleza: “Hata uwe una hali gani za kibinafsi, kama umebatizwa, una hali nzuri ya kiadili, unaweza kufanya mpango utimize takwa la kutumia kila mwezi saa 60 katika huduma ya shambani na unaamini ungeweza kutumika kuwa painia-msaidizi mwezi mmoja au zaidi, wazee wa kutaniko watafurahi kufikiria ombi lako la pendeleo hili la utumishi.” Je, waweza kupanga ufurahie pendeleo hili Machi? Aprili? Mei?
6 Mtazamo chanya kwa upande wa mabaraza ya wazee pamoja na uungaji-mkono wa moyo wote wa watangazaji wengine bila shaka utafanya itikio la mwito huu wa mapainia 2,500 kuwa wenye mafanikio makubwa. (Ebr. 13:7) Vichwa vyote vya familia vyatiwa moyo kuhakikisha ni wangapi katika nyumba zao wanaoweza kujiunga na vikundi vya mapainia-wasaidizi mwezi mmoja au zaidi kati ya ile inayokuja.—Zab. 148:12, 13; linganisha Matendo 21:8, 9.
7 Usifikie haraka mkataa kwamba huwezi kufanya upainia msaidizi kwa sababu ya kazi yako ya wakati wote, ratiba ya shule, madaraka ya familia, au wajibu mwingine mbalimbali wa Kimaandiko. Kwa wengine huenda isiwezekane kushiriki; hata hivyo, wakiwa na mpango mzuri na baraka za Yehova, wanaweza kufanikiwa. (Zab. 37:5; Mit. 16:3) Acha tamaa ya kushiriki katika utumishi wa painia iongoze hali zako; usiache hali zako ziongoze tamaa yako ya kupainia. (Mit. 13:19a) Kwa sababu hiyo, wakiwa na upendo mwingi kwa Yehova na kwa wanadamu wenzao, wengi wameweza kurekebisha kawaida yao ya maisha ya kila juma ili wapanue huduma yao mwezi mmoja baada ya muda fulani. (Luka 10:27, 28) Baraka nyingi zawangoja wale wanaojikakamua wenyewe kisulubu katika utumishi wa Ufalme.—1 Tim. 4:10.
8 Yanayotimizwa na Upainia Msaidizi: Jitihada ya nafsi yote inayofanywa na maelfu ya watumishi wa Mungu ili wafanye upainia msaidizi hutokeza sifa kubwa kwa Yehova. Wapiga-mbiu wa Ufalme hawa wanapojikakamua kueneza habari njema kwa watu wengi zaidi, wanavutwa karibu zaidi na Yehova kibinafsi kwa sababu wanajifunza kumtegemea zaidi ili wapate roho na baraka yake.
9 Kuwa na mapainia-wasaidizi, wa kawaida, na wa pekee miongoni mwetu hutokeza roho mpya yenye uhai katika kutaniko. Idili yao ni yenye kuambukiza wanapoongea kuhusu mambo yao yaliyoonwa shambani. Jambo hili huchochea wengine wachunguze tena mambo yao ya kutangulizwa na uwezekano wa ushiriki ulioongezeka katika kazi ya maana sana ya huduma. Dada aliyebatizwa akiwa na umri wa miaka 70 alianza mara moja kufanya upainia msaidizi kwa kuendelea. Miaka kadhaa baadaye, alipoulizwa kwa nini katika umri wake, bado alikuwa akijikakamua hivyo katika huduma akiwa painia-msaidizi kila mwezi, alisema alikuwa akihisi kana kwamba miaka ya kwanza 70 ya maisha yake ilikuwa imepotezwa bure, na kwamba hakutaka kupoteza miaka yake yoyote ya maisha iliyobaki!
10 Kila mshiriki wa kazi ya upainia msaidizi husitawisha stadi iliyoboreshwa katika huduma. Shahidi mmoja mchanga alikubali hivi: ‘Katika utoto wangu wa mapema nilikuwa naandamana na wazazi wangu katika utendaji wao wa kuhubiri. Utumishi wa shambani ulikuwa wenye kufurahisha kwelikweli. Hata hivyo, nilikuja kugundua kwamba nilikuwa tofauti na wengine shuleni. Kisha ikawa vigumu kwangu kuongea na wanafunzi wenzangu juu ya kweli. Nilipokuwa nikihubiri nyumba hadi nyumba, nilianza kuogopa kukutana na mtu ninayemjua shuleni. Kwa upande wangu nafikiri tatizo lilikuwa kuhofu mwanadamu. [Mit. 29:25] Nilipomaliza shule, niliamua kujaribu kupainia kwa muda. Tokeo likawa, kuhubiri kulinipendeza kuliko wakati mwingine wowote. Sikukuona kuwa utendaji wa kujifurahisha, wala mzigo mzito. Kwa kuona wanafunzi wangu wa Biblia wakifanya maendeleo katika kweli, nilifurahia uradhi mkubwa kwa ithibati ya kwamba Yehova Mungu alikuwa akitegemeza jitihada zangu.’ Kijana huyu aliendelea kutumikia akiwa painia wa kawaida.
11 Kulingana na maoni yanayofaa, wakati wengi watumikiapo wakiwa mapainia-wasaidizi katika kutaniko, matokeo huwa kuhubiriwa kikamili kwa eneo. Ndugu anayeshughulikia kutoa mgawo wa maeneo anaweza kuwaomba mapainia-wasaidizi msaada wao katika kuhubiri sehemu zisizohubiriwa mara nyingi. Kubeba chakula cha mchana na kuwa shambani siku nzima kutafanya iwezekane kuhubiri hata kona za mbali za eneo.
12 Wazee Wahitaji Kufanya Matayarisho ya Mapema: Katika miezi yote mitatu ifuatayo, mipango yapasa kufanywa ili kuratibu aina tofauti za utendaji wa kutoa ushahidi nyakati mbalimbali za juma, kutia ndani baadaye alasiri na mapema jioni, ili wengi iwezekanavyo waweze kushiriki. Pamoja na mahubiri ya kawaida ya nyumba hadi nyumba, tia ndani nyakati za kutoa ushahidi barabarani, kuhubiri maeneo ya biashara, na kurudia wasiokuwapo nyumbani. Kwa kufanya hivyo, wazee wanasaidia wale wanaopainia kushiriki utumishi wa shambani na kutaniko wakati itakapowezekana na kuwafaa zaidi mapainia. Kutaniko lapasa lijulishwe vizuri mipango yote ya utumishi wa shambani. Kuongozwa kwa mikutano ya utumishi kwapasa kuwe na mpango mzuri. Kwa kuongezea, eneo la kutosha lapaswa kuwapo na magazeti ya kutosha na fasihi nyingine ziagizwe bila kukawia.
13 Panga Ratiba Yako ya Kibinafsi ya Utumishi: Ndugu mmoja, ambaye hapo mwanzoni alikuwa mwenye kuogopa kufanya upainia msaidizi, alisema: “Kwa kweli ni rahisi zaidi kuliko nilivyofikiri itakuwa. Inahitaji ratiba nzuri tu.” Kwenye ukurasa wa nyuma wa nyongeza hii, je, waona mfano wa ratiba ya painia-msaidizi ambayo ingekuwa yenye kutumika kwako? Saa 15 kila juma kwa huduma ndio wakati unaohitajiwa tu kwa mapainia-wasaidizi.
14 Ili watumikie wakiwa mapainia-wasaidizi, wake-nyumbani na wafanyakazi wa zamu ya jioni hadi saa sita za usiku mara nyingi wanaweza kuratibu asubuhi zao kwa utumishi wa shambani. Wanashule na wanaofanya zamu ya usiku hadi asubuhi kwa ujumla wanaweza kufanya kazi ya kuhubiri baadaye alasiri. Wafanyakazi wa muda wote wa kazi ya kuajiriwa wameona ikiwezekana ama kuchukua pumziko la siku moja ya juma ama kutumia miisho-juma katika huduma, na kuongezea kutoa ushahidi jioni. Wengi ambao utumishi wao wa shambani ni wa miisho-juma tu huchagua miezi ambayo ina miisho-juma mitano kamili. Mwaka huu, ndivyo ilivyo na Machi, na vilevile Agosti na Novemba. Ukitumia ratiba isiyoandikwa kitu na nafasi kwenye ukurasa wa 6 ambayo imetolewa kuwa mwongozo, wazia kwa uangalifu na kwa sala kuhusu ratiba ya kibinafsi itakayokuwa yenye kutumika kwa hali yako mwenyewe.
15 Manufaa moja ya uandalizi wa painia-msaidizi ni hali yake ya kubadilikana. Unaweza kuchagua miezi ambayo utapainia, nawe waweza kutumikia mara nyingi unavyotaka. Ikiwa ungependa kufanya upainia msaidizi kwa kuendelea lakini huwezi kufanya hivyo, je, umefikiria kuhusu kujiandikisha kila baada ya mwezi mmoja kwa mwaka mzima? Kwa upande mwingine, wengine wanaweza kutumikia wakiwa mapainia-wasaidizi kwa kuendelea kwa vipindi virefu vya wakati.
16 Utayarishaji kwa Ajili ya Upainia wa Wakati Wote: Wengi ambao wana roho ya upainia wangependa kutumikia wakiwa mapainia wa kawaida, lakini wanajiuliza kama wana wakati, hali au nguvu za kufanya hivyo. Bila shaka walio wengi kati ya wale ambao sasa ni mapainia wa kawaida kwanza walifanya upainia msaidizi kuwa utayarishaji wa kazi ya wakati wote. Kwa kuongezea saa moja tu katika ratiba ya painia-msaidizi kila siku, au siku moja kamili kila juma, inawezekana kutimiza ratiba ya painia wa kawaida. Ili uone kama hilo lawezekana kwako, kwa nini usitumie saa 90 kwenye huduma ya upainia msaidizi ya mwezi mmoja au zaidi? Kwa wakati uleule, utakuwa ukisitawisha ziara za kurudia na mafunzo ya Biblia, ambayo yatakuruhusu ufurahie huduma ya painia iliyo na usawaziko.
17 Dada mmoja alifurahia miaka sita ya upainia msaidizi wa kuendelea. Wakati huo wote ulikuwa mradi wake kuingia utumishi wa painia wa kawaida. Akiwa na lengo hilo, alijaribu kazi za kuajiriwa nne akitumaini kutafuta hali itakayomwezesha kufikia takwa la saa 90 za mapainia wa kawaida. Kila mwezi alichora ratiba moja au mbili ili ahesabu kama itawezekana. Lakini katika kuzichunguza, aliona haikuwezekana kwake kufanya huduma ya wakati wote. Hata hivyo, aliendelea kumwomba Yehova mwelekezo wake. Kisha siku moja alipokuwa akijitayarisha kwa Mkutano wa Utumishi, alisoma makala katika Huduma ya Ufalme Yetu ya Septemba 1991 iliyosema: “Badala ya kukazia isivyostahili takwa la saa, kwa nini tusikazie fikira zetu juu ya kuongeza fursa za kushiriki kazi ya kukusanya? (Yn. 4:35, 36)” Yeye asimulia: “Niliisoma sentensi hiyo kwa kurudia mara tano au sita, nami nilikuwa na hakika hili lilikuwa jibu la Yehova. Wakati huo niliamua kuingia utumishi wa painia wa kawaida.” Ijapokuwa kazi yake ya kuajiriwa isiyo ya wakati wote haikuwa nzuri zaidi, alipeleka ombi lake la painia wa kawaida. Juma moja baadaye ratiba yake ilibadilishwa, naye akapewa saa za kazi ambazo zilimfaa hasa. Yeye alimalizia hivi, “Je, huu ni mkono wa Yehova, au sio?,” naye akaongezea: “Unapomwomba Yehova mwongozo na kuupokea, usiukimbie—ukubali.” Ikiwa ni tamaa yako kufanya upainia wa kawaida, labda mwishoni mwa miezi mitatu ya upainia msaidizi mwezi huu wa Machi, Aprili, na Mei, utasadikishwa kwamba wewe pia unaweza kufanikiwa katika huduma ya wakati wote.
18 Tuna uhakika kwamba Yehova atabariki bidii na atategemeza jitihada za watu wake wanapohubiri habari njema za wokovu wakati wa kipindi cha utendaji huu wa pekee wa masika. (Isa. 52:7; Rom. 10:15) Je, utaitikia mwito wa mapainia-wasaidizi 2,500 kwa kushiriki mwezi wa Machi? Aprili? Mei?
[Sanduku katika ukurasa wa 3]
Jinsi ya Kufanikiwa Ukiwa Painia-Msaidizi
■ Uwe na uhakika kwamba utafanikiwa
■ Sali kwa Yehova abariki jitihada zako
■ Alika mtangazaji mwingine apainie pamoja nawe
■ Panga ratiba ya utumishi inayofaa
■ Agiza magazeti ya kutosha
■ Unga mkono mipango ya utumishi ya kutaniko
■ Tafuta fursa za kutoa ushahidi wa vivi hivi