Sanduku La Swali
◼ Twaweza kufanya nini ili kufanya mikutano yetu iwe yenye matokeo?
Huenda wengine wakaelekea kuhisi kwamba wazee na watumishi wa huduma ndio tu wenye daraka la kufanikisha mikutano ya kutaniko kwa sababu wao ndio huiongoza na kushughulikia sehemu karibu zote. Kwa kweli, sisi sote twaweza kuchangia kibinafsi mikutano yenye kupendeza na yenye manufaa. Twaweza kusaidia kufanya mikutano iwe yenye matokeo kwa njia kumi zifuatazo:
Tayarisha Kimbele. Tunapojitayarisha vema, mikutano huvuta upendezi wetu. Sote tufanyapo hivi, mikutano inakuwa yenye uchangamfu na yenye kujenga zaidi. Hudhuria kwa ukawaida. Wahudhuriaji wengi hutia moyo kila mmoja aliyepo, wakiimarisha uthamini kuhusu umaana wa kuhudhuria. Fika kwa wakati. Tuketipo kabla ya programu kuanza, twaweza kujiunga katika wimbo na sala ya kufungua na kupokea manufaa kamili kutokana na mkutano. Njoo ukiwa na vifaa. Kwa kuleta Biblia zetu na kichapo au vichapo vinavyotumiwa mkutanoni, twaweza kufuata na kuelewa vizuri yale yanayozungumzwa. Epuka vikengeusha-fikira. Labda twaweza kusikiliza vizuri tuketipo mbele. Kunong’onezana na kwenda msalani mara nyingi kwaweza kufanya tukose kukaza fikira na tuzuie wengine pia. Shiriki. Wengi wetu wanaponyoosha mikono na kutoa maelezo, wengi wanatiwa moyo na kujengwa na maelezo ya imani. Toa maelezo mafupi. Kufanya hivi huwapa wengi iwezekanavyo fursa ya kushiriki. Imetupasa tutegemeze maelezo yetu mafupi juu ya somo linalozungumzwa tu. Timiza migawo. Tukiwa wanafunzi katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi au washiriki katika Mkutano wa Utumishi, na tujitayarishe vizuri, tufanye mazoezi ya maonyesho kimbele, na tusikose kutimiza migawo yetu. Pongeza walioshiriki. Waambie wengine jinsi jitihada zao zinavyothaminiwa. Kufanya hivyo huwajenga na kuwachochea wafanye vizuri zaidi wakati ujao. Tianeni moyo. Salamu zenye fadhili na mazungumzo yenye kujenga kabla na baada ya mikutano huongezea upendezi na manufaa tuwezazo kupata kutokana na kuhudhuria mikutano.