Roho ya Yehova Iko Nasi
1 Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tuna mgawo mkubwa. Yesu alisema: “Katika mataifa yote lazima habari njema ihubiriwe kwanza.” (Mr. 13:10) Kwa maoni ya kibinadamu, mgawo huo ungeonekana mgumu, lakini sivyo ilivyo. Twategemezwa na kani yenye nguvu zaidi ulimwenguni pote—roho ya Mungu.—Mt. 19:26.
2 Uthibitisho wa Karne ya Kwanza: Akiutumia unabii wa Isaya kujihusu, Yesu alisema: “Roho ya Yehova iko juu yangu, . . . kutangaza habari njema.” (Luka 4:17, 18) Kabla ya kupaa mbinguni, aliwaambia wafuasi wake kwamba wao vilevile wangepata nguvu kutokana na roho takatifu ili kutoa ushahidi “hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.” Baada ya hapo, Filipo alielekezwa na roho takatifu amhubirie yule Mwethiopia aliyekuwa ofisa wa nyumba ya mfalme, roho ilimtuma Petro kwa ofisa Mroma, nayo ilimtuma Paulo na Barnaba kuyahubiria mataifa ya Wasio Wayahudi. Ni nani ambaye angewazia kwamba watu kutoka malezi hayo wangeikubali kweli? Lakini waliikubali.—Mdo. 1:8; 8:29-38; 10:19, 20, 44-48; 13:2-4, 46-48.
3 Uthibitisho wa Siku ya Kisasa: Kitabu cha Ufunuo hukazia kuhusika kwa roho takatifu katika kazi ya kuhubiri ya leo kwa kusema hivi: “Na roho na bibi-arusi hufuliza kusema: “Njoo!” . . . Acha yeyote atakaye achukue maji ya uhai bure.” (Ufu. 22:17) Roho imechochea jamii ya bibi-arusi wa Kristo na “kondoo wengine” walio waandamani wao wahubirie watu wote habari njema. (Yn. 10:16) Twapaswa kuwa wajasiri katika kuhubiri kwetu, bila kusita kuhubiria watu wa aina zote, tukiwa na uhakika sikuzote kwamba roho ya Mungu itatusaidia. Kichapo 1998 Yearbook chaandaa uthibitisho wenye kusadikisha wa kwamba roho ya Mungu yaendelea kuwa na watumishi wake. Tazama matokeo! Katika miaka miwili ya utumishi iliyopita, wastani wa watu zaidi ya 1,000 walibatizwa kila siku.
4 Uwe na hakika ya kwamba roho ya Mungu itaendelea kuwa nasi tuhubiripo ujumbe wa Ufalme kwa kadiri anayotaka Yehova. Ujuzi huu wapaswa kututia moyo na kutuchochea tuendelee kujikakamua wenyewe katika kazi ya maana zaidi ya Ufalme.—1 Tim. 4:10.