Ni Vizuri Kama Nini Kuhudhuria Sikuzote!
1 Kwa miongo kadhaa katika Ulaya Mashariki, wengi kati ya ndugu zetu wapendwa walipigwa marufuku wasiweze kuhudhuria mikutano hadharani. Ebu wazia shangwe yao marufuku zilipoondolewa nao wangeweza kukutana pamoja kwa uhuru!
2 Mwangalizi wa mzunguko mmoja aliandika hivi kuhusu ziara yake katika kutaniko moja: “Jumanne jioni, mara tu ziara yangu ilipoanza, mfumo wa kupasha joto uliharibika. Nje, halihewa ilibaki katika kiwango cha kuganda, na ndani, ilikuwa digrii 5 Selsiasi hivi. Akina ndugu waliketi wakiwa wamevalia makoti yao, vitambaa vya shingoni, kofia, na buti. Hakuna mtu aliyeweza kufuatisha Biblia, kwa kuwa haikuwezekana kufungua kurasa. Nikisimama jukwaani nikiwa nimevalia suti yangu, nilikuwa nimeganda kabisa, na kila mara nilipoongea, ningeweza kuona mvuke wangu. Lakini jambo lililonivutia ni kwamba sikusikia mtu hata mmoja aliyelalamika. Ndugu wote walisema jinsi ilivyopendeza na ilivyokuwa vizuri kuhudhuria!” Ndugu hao hawakufikiria hata kukosa mkutano huo!
3 Je, Hivyo Ndivyo Tunavyohisi? Je, twathamini sana fursa ya kukutana kwa uhuru kwenye mikutano yetu ya kila juma? Au sisi hukosa kuithamini mikutano hali zinapokuwa si nzuri? Kuhudhuria mikutano kwa ukawaida huenda kusiwe rahisi, na huenda kukawa na nyakati ambazo tuna sababu za maana za kutohudhuria. Ingawa hivyo, usisahau kamwe kwamba, kuna watu miongoni mwetu ambao licha ya uzee, matatizo mabaya sana ya afya, vizuizi vya kimwili, ratiba ya kazi yenye kutumia nguvu nyingi, na madaraka mengine mazito huona umaana wa mikutano nao huhudhuria karibu sikuzote. Hivyo ni vielelezo bora kwetu kama nini kufuata!—Linganisha Luka 2:37.
4 Na tuifanye iwe desturi yetu kutegemeza ibada ya kweli kwa kuhudhuria mikutano ya Kikristo, kuanzia na kikundi kidogo cha funzo la kitabu hadi mkusanyiko mkubwa. Kwa nini tuchukulie kwa uzito kuhudhuria vikusanyiko hivi? Kwa sababu ni amri ya Mungu kwamba tukutane pamoja. Lakini kuna sababu nyinginezo za maana. Sisi sote twahitaji maagizo ya kimungu na msaada wa roho takatifu, ambayo hupatikana kwenye mikutano. (Mt. 18:20) Twajengwa kwa badilishano la kitia-moyo tunaposhiriki na ndugu zetu.—Ebr. 10:24, 25.
5 Wakati wa mgeuko-umbo, Petro alisema, “Mfunzi, ni vizuri kwetu kuwa hapa.” (Luka 9:33) Twapaswa kuhisi vivyo hivyo kuhusu mikutano yetu yote ya Kikristo. Kwa kweli, ni vizuri kama nini kuhudhuria sikuzote!