Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • km 11/98 kur. 3-6
  • Uwe Mwenye Matokeo Katika Huduma Yako

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uwe Mwenye Matokeo Katika Huduma Yako
  • Huduma Yetu ya Ufalme—1998
  • Habari Zinazolingana
  • Njia za Kuhubiri Habari Njema
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
  • Toa Uangalifu Daima kwa Fundisho Lako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Je, Utanufaika kwa Kuwa na Eneo la Kibinafsi?
    Huduma ya Ufalme—2013
  • Tumia Wakati Wako kwa Matokeo
    Huduma Yetu ya Ufalme—1999
Pata Habari Zaidi
Huduma Yetu ya Ufalme—1998
km 11/98 kur. 3-6

Uwe Mwenye Matokeo Katika Huduma Yako

1 Anga latiwa giza, sauti yenye kutia hofu yaongezeka hadi kuwa mngurumo wenye kishindo. Moshi ulio kama wingu washuka. Kuna nini? Jeshi la mamilioni ya nzige wanaokuja kuleta ukiwa kamili nchini! Mandhari hiyo iliyofafanuliwa na nabii Yoeli inatimizwa leo katika kazi ya kuhubiri ya watumishi wa Mungu watiwa-mafuta na waandamani wao, umati mkubwa.

2 Gazeti Mnara wa Mlinzi la Mei 1, 1998, ukurasa wa 11, fungu la 19, lilisema: “Jeshi la nzige wa Mungu wa siku ya kisasa wametoa ushahidi kamili katika ‘mji’ wa Jumuiya ya Wakristo. (Yoe. 2:9) . . . Wangali wanapanda vizuizi vyote na kuingia mamilioni ya makao, kuwafikia watu barabarani, kusema nao kwenye simu, na kuwafikia katika njia yoyote iwezekanayo, wajulishapo rasmi ujumbe wa Yehova.” Je, si pendeleo kubwa kushiriki katika kazi hii ya kuagizwa na Mungu?

3 Tofauti na nzige halisi, ambao lengo lao hasa ni kujilisha, sisi tukiwa watumishi wa Yehova tunahangaikia sana maisha ya wale tunaohubiria. Twataka kusaidia wengine wajifunze kweli tukufu zilizo katika Neno la Mungu na kuchochewa kuchukua hatua itakayoongoza kwenye wokovu wao wa milele. (Yn. 17:3; 1 Tim. 4:16) Kwa sababu hiyo, twataka kuwa wenye matokeo katika njia tunayotimiza huduma yetu. Iwe twatumia njia yoyote ile ya kuhubiri, twapaswa kuchunguza kama twaitimiza katika njia na wakati utakaoleta matokeo mazuri zaidi. Kwa kuwa “mandhari ya ulimwengu huu inabadilika,” ni vema kuchanganua njia zetu na mfikio wetu kuhakikisha kwamba twakabiliana na ugumu wa kuwa wenye matokeo iwezekanavyo.—1 Kor. 7:31.

4 Ijapokuwa twajitahidi kufikia watu katika njia mbalimbali, mahubiri ya nyumba hadi nyumba yangali nguzo ya huduma yetu. Je, mara nyingi wewe hupata kwamba watu hawako nyumbani au wanalala unapozuru? Yatamausha kama nini, kwa kuwa huwezi kushiriki ujumbe wa habari njema nao! Waweza kukabilianaje na ugumu huu?

5 Uwe Mwenye Kubadilikana na Mwenye Kusababu: Katika Israeli ya karne ya kwanza, wavuvi walivua usiku. Kwa nini usiku? Ingawa huo haukuwa wakati uliowafaa, ulikuwa wakati mzuri zaidi kushika samaki wengi zaidi. Ulikuwa wakati wenye matokeo zaidi. Katika kueleza juu ya zoea hili, gazeti Mnara wa Mlinzi la Juni 15, 1992, lilisema: “Sisi pia twapaswa kuchunguza eneo letu ili twende kuvua, wakati ambao, kwa kweli, watu walio wengi wamo nyumbani na wangeitikia.” Kuchunguza kwa uangalifu mazoea ya kijamii kumeonyesha kwamba katika jumuiya nyingi za viungani na maeneo ya makazi, labda watu wako nyumbani tunapoenda mapema Jumamosi na Jumapili asubuhi, lakini huenda wasitupokee wakati huo. Ikiwa eneo lenu liko hivyo, je, waweza kurekebisha saa za ziara zako hadi baadaye asubuhi au hata alasiri? Hiyo ni njia ifaayo ya kuongeza matokeo ya huduma yetu na vilevile kuonyesha twawajali jirani zetu, ambao ni uthibitisho wa upendo wa Ukristo wa kweli.—Mt. 7:12.

6 Kwenye Wafilipi 4:5, mtume Paulo atukumbusha kwamba twapaswa ‘kuacha hali yetu ya kukubali sababu ijulikane kwa watu wote.’ Kupatana na mwelekezo huu uliopuliziwa, twataka kuwa wenye usawaziko na wenye kukubali sababu katika njia zetu tunapotimiza mgawo wetu wa kuhubiri kwa bidii na uchangamfu. Hatutaki ‘kuepuka kufundisha hadharani na nyumba hadi nyumba,’ bali twataka kuhakikisha kwamba twatimiza huduma yetu ya nyumba hadi nyumba nyakati zifaazo na zenye matokeo. (Mdo. 20:20) Kama wale wavuvi katika Israeli ya karne ya kwanza, twahangaishwa na ‘kuvua’ nyakati tunazoweza kuwa wenye matokeo zaidi, si nyakati tunazoona kuwa zafaa zaidi kwetu wenyewe.

7 Ni marekebisho gani yawezayo kufanywa? Mara nyingi, mikutano ya utumishi wa shambani hufanywa saa 3:00 asubuhi au hata mapema zaidi ya hapo Jumamosi na Jumapili, kisha kikundi huanza bila kukawia kuhubiri mlango hadi mlango katika eneo. Hata hivyo, katika maeneo kadhaa, mabaraza mengine ya wazee yamepanga kikundi kishiriki katika aina nyingine za huduma, kama vile kutoa ushahidi barabarani, eneo la biashara, au ziara za kurudia, kabla ya kwenda mlango hadi mlango kwenye maeneo ya wakazi. Saa 4:00 hivi asubuhi, kikundi huenda moja kwa moja kuhubiri mlango hadi mlango mpaka mapema alasiri. Katika maeneo mengine, mapema alasiri badala ya asubuhi, huenda ukawa wakati mzuri kukutana kwa ajili ya utumishi. Marekebisho hayo yanaweza kuchangia ongezeko la matokeo katika mahubiri ya mlango hadi mlango.

8 Uwe na Ufahamu na Mwenye Busara: Tunapowafikia watu mlango hadi mlango, twakutana na maitikio mbalimbali kwa ujumbe wetu. Wenye nyumba fulani hutupokea, wengine huwa na ubaridi, na huenda wachache wakawa wenye kubishana au wachokozi. Kuhusu hao wa mwisho, kwenye ukurasa wa 7 wa kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko, twakumbushwa kwamba hatujaribu ‘kupata ushindi katika kubishana na watu wasioonyesha staha kuelekea ukweli.’ Ikiwa mwenye nyumba ni mwenye uhasama, ni vema kuondoka. Hatupaswi kamwe kupingana na watu kwa kusisitiza wazungumze nasi au wakubali maoni yetu. Hatulazimishi watu kusikia ujumbe wetu. Hilo halingekuwa kukubali sababu na kufanya hivyo kungeweza kusababisha matatizo kwa Mashahidi wengine na kazi hii kwa ujumla.

9 Kabla ya kuanza kulihubiri eneo, ni jambo la hekima kuchunguza kadi ya eneo kwa ajili ya taarifa za nyumba ambazo wakazi wametuambia tusiwatembelee. Ikiwa kuna nyumba kama hizo, kila mhubiri anayehubiri kwenye mtaa huo apaswa kuambiwa mahali ambapo hapaswi kwenda. Mtu yeyote hapaswi kujiamulia mwenyewe kuzuru nyumba hizo bila kuelekezwa na mwangalizi wa utumishi afanye hivyo.—Ona Huduma ya Ufalme Yetu ya 1994, Sanduku la Swali.

10 Twaweza kuongeza matokeo yetu kwa kuwa wenye ufahamu tunapohubiri nyumba hadi nyumba. Uwe mwenye kuangalia kwa makini unapokaribia nyumba. Je, pazia zote au visitiri vyote vimefungwa? Je, hakuna sauti yoyote au shughuli zozote? Hilo huenda likaonyesha kwamba wenyewe wamelala. Yamkini, tutakuwa na mazungumzo yenye matokeo zaidi na mwenye nyumba tukirudi baadaye. Labda itafaa kuipita nyumba hii wakati huu, tukiiandika nyumba hiyo. Unaweza kuangalia nyumba hiyo tena kabla ya kuondoka kwenye eneo hilo au urudi tena saa nyingine.

11 Huenda bado pindi fulani tukamwamsha mtu bila kukusudia au kumsumbua kwa njia fulani. Huenda akaonekana amechokozeka au amekasirika. Tuitikieje? Mithali 17:27 hushauri hivi: “Mwenye roho ya utulivu ana busara.” Ingawa hatuombi radhi kwa ajili ya huduma yetu, kwa hakika twaweza kuonyesha jinsi tunavyosikitika kwamba tumeenda wakati usiofaa. Kwa upole twaweza kuuliza kama wakati mwingine ungefaa zaidi na kuahidi kurudi. Wonyesho mnyofu wa kujali kibinafsi kwa sauti pole mara nyingi humtuliza mtu kama huyo. (Mit. 15:1) Mwenye nyumba akitujulisha kwamba yeye hufanya kazi usiku kwa ukawaida, taarifa yaweza kuhusianishwa na kadi ya eneo ili ziara zijazo zifanywe saa inayofaa.

12 Ufahamu wafaa pia tunapojitahidi kuhubiri eneo letu kikamili. Kwa kuwa watu wengi hawako nyumbani tunapoenda mara ya kwanza, twahitaji kufanya jitihada za ziada kuwafikia ili kushiriki nao ujumbe wa wokovu. (Rom. 10:13) Wahubiri fulani hurudi kwenye nyumba hiyo baadaye katika siku ili kujaribu kupata watu nyumbani. Jirani hawakosi kuona jambo hilo. Hata hivyo, tungependa kuepuka kuonekana kusikofaa kwamba Mashahidi wa Yehova ‘sikuzote hutembea’ katika eneo lao. Hilo laweza kuepukwaje?

13 Tumia ufahamu. Unaporudi tena mahali ambapo hapakuwa na watu nyumbani, je, kuna dalili yoyote kwamba pana mtu nyumbani sasa? Ikiwa mtu hawezi kufikiwa baada ya majaribio kadha kufanywa saa tofauti-tofauti za siku, kama vile jioni, huenda ikawezekana kumfikia mwenye nyumba kupitia simu. Kama sivyo, trakti au kikaratasi cha ukaribishaji chaweza kuachwa kwa busara mlangoni, hasa ikiwa eneo lahubiriwa mara nyingi kwa kiasi. Huenda mtu huyo akafikiwa wakati unaofuata eneo lihubiriwapo.

14 Twapaswa kuepuka kumweka mwenye nyumba katika mazungumzo marefu mlangoni ikiwa hali ya hewa ni mbaya mno. Ukialikwa ndani, uwe mwangalifu usichafue sakafu. Tumia ufahamu unapokabiliwa na mbwa anayebweka. Unapohubiri majengo ya vyumba vya kupangisha, fleti, au nyumba zinazopakana na hizo, zungumza kwa sauti ya chini na uepuke kupiga kelele ambazo husumbua wapangaji na kujulisha kuwapo kwako pale.

15 Uwe Mwenye Utaratibu na Heshima: Tukiwa na mpango mzuri twaweza kuepuka kufanyiza vikundi vikubwa, vinavyoonekana waziwazi vinavyokusanyika katika eneo. Baadhi ya wenye nyumba wanaweza kutishika kwa sababu ya kikundi kikubwa cha wahubiri wanaokusanyika mbele ya nyumba yao. Hatutaki kuwafanya wafikiri kwamba “tunavamia” maeneo yao ya makazi. Yafaa zaidi kufanya mipango ya kuhubiri eneo mahali pa kukutania kwa ajili ya utumishi wa shambani. Vikundi vidogo vya wahubiri, kama vile familia, haviogofyi wenye nyumba navyo havichukui wakati mwingi kuvipanga eneo linapohubiriwa.

16 Utaratibu hutaka wazazi wasimamie mwenendo wa watoto wao wanapolihubiri eneo. Watoto wapaswa kujiendesha vizuri wanapoandamana na watu wazima mlangoni. Vijana hawapaswi kuruhusiwa kucheza au kuzurura-zurura, wakivuta uangalifu usiofaa wa wakazi au wapita-njia.

17 Usawaziko wahitajiwa pia, kuhusu wakati wa kupumzika. Huduma ya Ufalme Yetu ya Juni 1995, ukurasa wa 7, ilisema: “Tunapokuwa katika utumishi wa shambani, twaweza kupoteza wakati mwingi tukinywa kahawa. Ingawa hivyo, wengi hupendelea kuendelea kuhubiria watu na kujinyima kushirikiana na akina ndugu kunywa kahawa wakati ambao umewekwa kando kwa ajili ya huduma.” Ijapokuwa kutua ili kupata viburudisho ni uamuzi wa kibinafsi, imeonekana kwamba nyakati nyingine, vikundi vikubwa vya akina ndugu na dada hukutana kwenye mkahawa. Mbali na wakati mwingi utakaotumiwa kuwatumikia, kuwa kwa umati huko kwaweza kuogofya wateja wale wengine. Nyakati nyingine, mambo yaliyoonwa asubuhi katika utumishi wa shambani huzungumzwa kwa sauti kubwa, na hilo laweza kuondoa heshima ya huduma yetu na kuharibu matokeo yake. Wahubiri wakiwa na ufahamu wanaweza kuepuka kujaza kupita kiasi duka hilo na kutumia wakati wa huduma isivyofaa.

18 Wengi wamepata matokeo mazuri kwa kufikia watu kokote ambako huenda wakapatikana—barabarani, kwenye maegesho ya magari, na mahali kwingineko kwa umma. Hapa pia, twataka kutoa ushahidi mzuri, si kwa maneno yetu tu bali pia kwa kukubali sababu. Wahubiri katika kila kutaniko wapaswa kuhakikisha wanastahi mipaka ya maeneo yao ili wasizidi waendao kwa miguu katika sehemu za kibiashara, miingilio ya maduka, na vijia au wafanyakazi katika biashara, kama vile kwenye vituo vya petroli, ambavyo hufunguliwa muda wa saa 24. Ili kuhakikisha kwamba twatimiza huduma yetu kwa utaratibu, kwa njia ya heshima, tutahubiri tu katika eneo letu tulilogawiwa isipokuwa mipango hususa iwe imefanywa kupitia Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko, ya kuwasaidia.—Linganisha 2 Wakorintho 10:13-15.

19 Makutaniko kadhaa yaliyo na sehemu nyingi ambapo kutoa ushahidi hadharani kwaweza kufanywa yamepanga sehemu hizo ziwe maeneo. Kadi ya eneo hupewa mhubiri mmoja-mmoja au kikundi. Hilo hufanya eneo litimizwe kwa matokeo na hulinda dhidi ya wahubiri wengi kuhubiri sehemu ileile wakati huohuo, kupatana na kanuni iliyo kwenye 1 Wakorintho 14:40: “Lakini acheni mambo yote yatukie kwa adabu na kwa mpango.”

20 Sura yetu sikuzote yapaswa kuwa yenye adhama na kuwakilisha wahudumu wanaoitwa kwa jina la Yehova. Ndivyo inavyopaswa kuwa na vifaa tunavyotumia. Mikoba ya vitabu iliyozeeka na Biblia zilizojikunja au zilizochafuka hukengeusha watu kutoka katika ujumbe wa Ufalme. Imesemwa kwamba mavazi na mapambo “ni njia ya kuwasiliana kwa haraka ambayo huwapa watu wanaotuzunguka habari inayoonyesha wewe ni nani na jinsi ulivyo na vile unavyofaa katika utaratibu wa mambo.” Kwa sababu hiyo, sura yetu haipaswi kuwa ya kizembe au isiyo nadhifu, wala kung’ara mno au wenye madoido mengi, bali sikuzote ‘istahili habari njema.’—Flp. 1:27; linganisha 1 Timotheo 2:9, 10.

21 Kwenye 1 Wakorintho 9:26, mtume Paulo asema hivi: “Jinsi ninavyokimbia si bila uhakika; jinsi ninavyoelekeza ngumi zangu ni ili nisiwe nikipiga hewa.” Kwa kumwiga Paulo, twaazimia kuwa na huduma yenye matokeo. Tunaposhiriki katika kazi ya kutoa ushahidi tukiwa sehemu ya “jeshi la nzige” la Yehova leo, na tutumie kukubali sababu kwa Kikristo na ufahamu katika kupelekea wote katika eneo letu ujumbe wa wokovu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki