Heshimu Sana Jina Tukufu la Yehova
1 Shetani aliharibu jina la Mungu alipowachochea wazazi wetu wa kwanza wafanye dhambi. Ibilisi alidokeza kwamba Yehova alimdanganya Adamu. (Mwa. 3:1-5) Kwa kuwa jina la Mungu linahusiana na uwezo wake wa kutimiza neno lake, dai la Shetani lilikuwa uchongezi mbaya sana. Kwa kutimiza kusudi lake hatua kwa hatua, Yehova ameondolea jina lake shutuma na kulifanya liwe tukufu.—Isa. 63:12-14.
2 Sisi ndio watu ambao Yehova ‘amewaita kwa jina lake.’ (Mdo. 15:14, 17) Hiyo hutupa fursa ya kuonyesha jinsi tunavyohisi kuhusu kutakaswa kwa jina hilo. Twaliona jina la Yehova kuwa tukufu sana, kwa kuwa hilo huwakilisha kila kitu chema, chenye fadhili, upendo, rehema, na uadilifu. Tunajawa na kicho kwa ukuu wa jina tukufu la Mungu. (Zab. 8:1; 99:3; 148:13) Hilo litusukume tufanye nini?
3 Takasa Jina la Mungu: Jina la Mungu tayari ni tukufu zaidi. Lakini kwa mwenendo wetu safi na kuhubiri Ufalme, twaweza kuonyesha kwamba twaliheshimu sana jina la Mungu. Acheni tupaze sauti tukisema: “Mshukuruni BWANA, liitieni jina lake; yatangazeni matendo yake kati ya mataifa, litajeni jina lake kuwa limetukuka.” (Isa. 12:4) Twaweza kufanyaje hivyo?
4 Twaweza kutumia kila fursa ili kutangaza jina la Yehova na yote ambayo jina hilo lamaanisha. Iwe ni rasmi au kivivi hivi, nyumba hadi nyumba au duka hadi duka, barabarani au kwa kutumia simu, kazi yetu ya kuhubiri humheshimu Yehova. Tunapokuta watu wenye kupendezwa ambao wanasikiliza, twapaswa kufanya mipango hususa ya kuwarudia na kuwafundisha mengi zaidi juu ya Yehova. Hilo lamaanisha kwamba tutimize ahadi zetu za kuwarudia bila kukosa na kudumu katika jitihada zetu za kuanzisha mafunzo ya Biblia ya nyumbani. Kwa furaha, kila mwaka mamia ya maelfu ya watu wanapata kujua, kustahi, na kutakasa jina tukufu la Yehova.
5 Kushiriki kwetu kwa moyo wote katika kazi ya kulitakasa jina la Mungu huonyesha wazi msimamo wetu kuhusu lile suala ambalo Shetani alitokeza katika Edeni. Hii ndiyo kazi njema na yenye kuheshimika zaidi tunayoweza kufanya. Na tuliheshimu zaidi na kulisifu kwa bidii jina tukufu la Yehova!—1 Nya. 29:13.