Kujulisha Jina la Yehova Katika Dunia Yote
1 Yesu alipowatuma wanafunzi wake wawe mashahidi “hadi sehemu ya mbali sana ya dunia,” alikuwa tayari amewawekea kielelezo cha kufuata. (Mdo. 1:8) Wakati wowote na mahali popote alipopata watu, alizungumza nao kuhusu kusudi la Mungu kwa wanadamu. Kwa kumwiga Yesu, jamii ya mtumwa mwaminifu inatumia njia mbalimbali kufanya jina la Yehova ‘lijulikane katika dunia yote.’—Isa. 12:4, 5.
2 Yaliyofanywa Siku za Zamani: Katika miaka iliyopita mahubiri yalichapishwa katika magazeti; ile “Photo-Drama of Creation” ilitolewa na kuonyeshwa kwa mamilioni; magari yenye vikuza-sauti yalitumiwa; kinanda cha gramafoni kilitumiwa sana na kwa muda fulani redio—yote hayo yalitumiwa ili kuhubiri habari njema. Bila shaka, mkazo umetiliwa katika kukutana na watu kibinafsi ili upendezi wowote unaoonyeshwa uweze kufuatiwa. Kwa sababu hiyo, huduma ya nyumba hadi nyumba imekuwa njia yenye matokeo sana katika kufanya jina la Yehova lijulikane kila mahali.—Mdo. 5:42.
3 Yanayofanywa Katika Siku Yetu: Kadiri nyakati zinavyoendelea kubadilika ulimwengu nao wasonga kwa kasi sana, na katika mahali pengi watu hawapatikani sana nyumbani. Wachache wana mwelekeo wa kutumia wakati wakisoma na kutafakari juu ya mambo ya kiroho. Kwa hiyo, ni lazima huduma yetu ibadilikane ili kufaa hali. Kwa kuongezea kuendelea kumaliza eneo kwa kuhubiri nyumba hadi nyumba, tumetiwa moyo kwenda mahali watu walipo na ‘kuwa tayari sikuzote’ kutetea tumaini tulilo nalo. (1 Pet. 3:15) Hilo lamaanisha kujitahidi kuwahubiria wafanyakazi wenzetu, wanashule wenzetu, watu barabarani, na katika bustani au katika maegesho ya magari, duka hadi duka na mahali pengine popote ambapo watu waweza kupatikana. Tukiwa na utegemezo wa Yehova kazi yetu itafanikiwa sana. Je, wewe unashiriki kuwafikia watu popote walipo?
4 Acheni sisi sote binafsi tutumie kila njia tuwezayo ili kufanya jina la Yehova lijulikane katika eneo letu. Tunaweza kupata uradhi katika kutimiza kikamili huduma yetu, tukitarajia Yehova awavute wenye mioyo minyoofu.—Yoh. 6:44.