Je, Utakuwapo?
1 Shahidi mmoja wa muda mrefu alisema hivi: “Ukikosa siku ya kwanza ya kusanyiko, tayari unakuwa umekosa mengi sana!” Kwa nini alihisi hivyo? Kwa sababu siku ya kwanza ndiyo mwanzo wa karamu nono ya kiroho ambayo tunaandaliwa na tengenezo la Yehova. (Isa. 25:6) Tunapokuwapo kuanzia mwanzo, hiyo huonyesha kwamba twakubaliana na maneno ya mtunga-zaburi aliyesema: “Nilifurahi waliponiambia, na twende nyumbani kwa BWANA.”— Zab. 122:1.
2 Hata hivyo, mwaka jana katika baadhi ya mikusanyiko ya wilaya ya “Neno la Mungu la Kiunabii,” siku ya Ijumaa hudhurio lilikuwa chini kidogo kuliko Jumamosi na Jumapili. Hii yamaanisha kwamba asilimia kubwa ya ndugu na dada zetu walikosa kusikiliza sehemu za kusanyiko ambazo zilitoa habari muhimu kuhusu neno la kiunabii. Wao pia walipoteza ushirika wenye kupendeza pamoja na waamini wenzi.
3 Usiruhusu Kazi ya Kimwili Iingilie Kati: Hangaiko kuhusu kuhatarisha kazi ya kuajiriwa laweza kuwa ndiyo sababu iliyowafanya wengine wasihudhurie siku ya Ijumaa. Hata hivyo, Mashahidi wengi wamepata kwamba waajiri wao wako tayari kushirikiana nao katika jambo hili ikiwa tu wanaomba ruhusa mapema. Mwajiri mmoja alivutiwa sana na jinsi dada mmoja painia alivyoazimia kuhudhuria mikutano yote ya kutaniko na makusanyiko hivi kwamba mwajiri huyo alitumia siku nzima katika kusanyiko ambalo dada huyo alihudhuria!
4 Usidhanie kwamba mwajiri wako hatakupa ruhusa, au kukata kauli kwamba kukosa siku moja ya kusanyiko si kitu. Ukiwa na usadikisho wenye kuhisiwa moyoni jitayarishe kumwonyesha mwajiri wako kupitia Maandiko sababu kwa nini kuhudhuria kusanyiko ni sehemu muhimu ya ibada yako. (Ebr. 10:24, 25) Kisha weka tumaini lako katika ahadi za Yehova, ukitambua kwamba chochote utakachohitaji kimwili atakuandalia ukiweka mahitaji ya kiroho kwanza maishani.—Mt. 6:33; Ebr. 13:5, 6.
5 Jambo muhimu ni kuthamini “mambo yaliyo ya maana zaidi.” (Flp. 1:10, 11; Zab. 27:4) Hilo hutusukuma tufanye mipango ili tunufaike kikamili kutokana na uandalizi huu muhimu kutoka kwa Yehova. Anza kufanya mipango yako kamili sasa, na uazimie kwamba utakuwapo siku zote tatu!