Kusanyiko la Wilaya la Mashahidi wa Yehova la 2006 la “Ukombozi Unakaribia”
1 Mfalme Hezekia wa Yuda la kale alitumia wakimbiaji kupeleka barua za kuwaita watu wakusanyike pamoja Yerusalemu. (2 Nya. 30:6, 13) Itikio la watu lilionyesha mtazamo wao kuelekea ibada ya kweli. (2 Nya. 30:10-12) Miezi michache ijayo, watumishi wa Yehova watakuwa na fursa kama hiyo ya kuonyesha uthamini wao wa kutoka moyoni kwa tukio la pekee la kukusanyika pamoja ili kumwabudu Yehova. Barua ya kuwaalika mhudhurie Kusanyiko la Wilaya la “Ukombozi Unakaribia” imetumwa katika kutaniko lenu. Utaitikiaje mwaliko huo?
2 Fanya Mipango Sasa: Ili tunufaike kabisa na programu ya kiroho ambayo inatayarishwa, tunahitaji kuhudhuria programu yote. Anza kufanya mipango yoyote inayohitajiwa sasa ili wewe pamoja na familia yako mhudhurie siku zote tatu. (Met. 21:5) Huenda matayarisho hayo yakatia ndani kumwomba mwajiri wako ruhusa, kuzungumzia mipango yako na mwenzi asiyeamini, kufanya mipango ya mahali pa kulala, na kusaidia wanafunzi wa Biblia wahudhurie siku zote. Usiahirishe mambo hayo muhimu hadi dakika ya mwisho. Badala yake, sali kwa Yehova kuhusu mambo hayo, ukitumaini kwamba ‘yeye mwenyewe atatenda.’—Zab. 37:5.
3 Tengenezo la Yehova limejitahidi ili kuhakikisha kwamba kutakuwa na vyumba vya kulala vya kutosha kwenye kila mji au jiji la kusanyiko. Kuthamini jitihada za ndugu zetu waliofanya kazi kwa bidii ili kusaidia kufanya mipango hiyo, kuwafikiria ndugu na dada wenzetu watakaohudhuria kusanyiko, na kuheshimu utaratibu wa kitheokrasi kunapaswa kutuchochea tufuate kikamili mwongozo ambao umetolewa katika makala hii.—1 Kor. 13:5; 1 The. 5:12, 13; Ebr. 13:17.
4 Kuhifadhi Vyumba vya Hoteli: Ikiwa utakaa hotelini, Idara ya Mahali pa Kulala inaweza kukusaidia kupata hoteli inayofaa kwenye mji au jiji la kusanyiko. Tafadhali andikia Idara ya Mahali pa Kulala mapema na kutaja pesa ambazo ungependa kulipa kwa mtu mmoja kila siku. Ushirikiano wako utakusaidia kupata hoteli karibu na jiji la kusanyiko kwa bei nafuu.—1 Kor. 14:40.
5 Unapaswa kuhifadhi tu vyumba vya hoteli utakavyotumia wakati wa kusanyiko. Hatungependa hoteli ihifadhi vyumba kwa wajumbe wa kusanyiko ambao hawatavitumia. Kila chumba kinapaswa kuhifadhiwa kwa jina la mtu mmoja kati ya wale watakaokitumia.
6 Ili kuhakikisha kwamba chumba chako hakitapewa mtu mwingine, huenda ukahitajiwa kulipa ada ya kukihifadhi. Iwapo ada itahitajika, Idara ya Mahali pa Kulala itawasiliana nawe.
7 Mahitaji ya Pekee: Methali 3:27 inasema: “Usiwanyime watu mema wanayostahili, mkono wako ukiwa na uwezo wa kuyafanya.” Unawezaje kuwafanyia wengine mema wakati wa kusanyiko? Huenda wahubiri walio wazee kwa umri, walio wagonjwa, walio katika utumishi wa wakati wote, na wengine wakahitaji usafiri au mahali pa kulala. Watu wa ukoo ndio wenye daraka kuu la kushughulikia mahitaji ya watu hao. (1 Tim. 5:4) Ikiwa hawawezi kufanya hivyo, waamini wenzao wanaweza kusaidia. (Gal. 6:10) Waangalizi wa mafunzo ya kitabu wanapaswa kuhakikisha kwamba wenye mahitaji ya pekee katika kikundi chao wamefanya mipango hususa mapema kabla ya kusanyiko.
8 Fomu za Ombi la Mahali pa Kulala kwa Wenye Mahitaji ya Pekee zinapatikana tu kwa ajili ya wahubiri ambao mahitaji yao ya mahali pa kulala hayawezi kushughulikiwa na watu wa familia zao au kutaniko. Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko inapaswa kuchunguza sifa za mhubiri, wakitumia miongozo kwenye fomu hiyo. Ni wahubiri wenye msimamo mzuri tu pamoja na watoto wao wenye tabia nzuri wanaoweza kufaidika na mpango huo.
9 Kuhudhuria Kusanyiko Lingine: Ili kuhakikisha kwamba hakuna upungufu wa viti, vichapo, mahali pa kulala, na kadhalika, wahubiri wanatiwa moyo wahudhurie kusanyiko ambalo kutaniko lao limepangiwa. Ikiwa utalazimika kuhudhuria kusanyiko lingine kwa sababu ya hali, tafadhali mwone mwandishi wa kutaniko lenu.
10 Wafanyakazi wa Kujitolea: Bila shaka wote watakaohudhuria kusanyiko watapata shangwe nyingi na kunufaika na chakula cha kiroho na fursa za kujengana. Tutakuwa wenye furaha hata zaidi ikiwa tutajitolea kusaidia kazi ambayo lazima ifanywe ili kufanikisha kusanyiko. (Mdo. 20:35) Hivi karibuni, Halmashauri za Kusanyiko zitawaalika watu wajitolee kusaidia. Je, unaweza kujitolea?—Zab. 110:3.
11 Mvulana mmoja mwenye umri wa miaka mitano alisema hivi alipokuwa akihudhuria kusanyiko la wilaya: “Kati ya mambo ninayofurahia zaidi katika ibada ya Yehova ni kuhudhuria kusanyiko la wilaya.” Maelezo hayo ya kutoka moyoni hutusaidia sote tutambue furaha ambayo sisi hupata tunapohudhuria kusanyiko la wilaya kila mwaka. Ni kama vile mtunga-zaburi alivyoimba: “Siku moja katika nyua zako ni bora kuliko siku elfu moja kwingineko.” (Zab. 84:10) Kupitia wimbo, Daudi alionyesha tamaa yake ya ‘kukaa katika nyumba ya Yehova siku zote za maisha yake, ili aweze kulitazama kwa uthamini hekalu la Yehova.’ (Zab. 27:4) Daudi alifurahi sana kuwa miongoni mwa waabudu wa Yehova. Na tuonyeshe uthamini kama huo kwa ajili ya ibada ya kweli kwa kuhudhuria siku zote tatu za Kusanyiko la Wilaya la “Ukombozi Unakaribia.”
[Maswali ya Funzo]
1. Watu wa Mungu walionyeshaje uthamini wao kwa ibada ya kweli nyakati za kale, nasi tuna fursa gani kama hizo leo?
2. Tunaweza kufanya nini sasa ili tunufaike kabisa na kusanyiko?
3. Kwa nini tunapaswa kufuata mipango iliyofanywa ya mahali pa kulala?
4-6. Tunapaswa kukumbuka mambo gani muhimu tunapotaka kuhifadhiwa chumba cha hoteli, na kwa nini?
7, 8. Watu walio na mahitaji ya pekee wanaweza kushughulikiwaje?
9. (a) Kwa nini tuhudhurie kusanyiko ambalo kutaniko letu limepangiwa? (b) Unapaswa kuchukua hatua gani ikiwa utalazimika kuhudhuria kusanyiko lingine kwa sababu ya hali?
10. Tunaweza kuchangia shangwe ya kusanyiko lijalo katika njia ipi?
11. Wewe huthamini nini kuhusu kusanyiko la wilaya la kila mwaka, na unapaswa kuazimia nini?
[Sanduku katika ukurasa wa 3]
Saa za Programu
Ijumaa na Jumamosi
3:30 asubuhi - 11:05 jioni
Jumapili
3:30 asubuhi - 10:10 jioni