Makusanyiko ya Wilaya ya Mashahidi wa Yehova ya 2004 ya “Tembea Pamoja na Mungu”
1 Ni nini kinachofanya makusanyiko yetu ya wilaya ya kila mwaka yakuvutie? Je, ni hotuba zenye kujenga na drama tunayotayarishiwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”? (Mt. 24:45-47) Je, ni vichapo vipya vyenye chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa? Je, ni kusikia ndugu na dada wakieleza jinsi Biblia imeboresha maisha yao? Je, ni ripoti zinazoonyesha jinsi kazi ya kuhubiri Ufalme inavyoendelea katika nchi nyingine? Je, ni kushirikiana na waamini wenzetu wenye umri mbalimbali? Sababu hizo na nyingine nyingi hufanya tutazamie makusanyiko yetu kwa hamu.
2 Hudhuria Siku Zote Tatu: Yehova aliamuru hivi kupitia Musa: “Wakutanishe watu . . . ili wasikilize na ili wajifunze.” (Kum. 31:12) Kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara, Yehova ametutayarishia programu ya pekee yenye kuelimisha kila siku ya kusanyiko. Tunataka kuwepo ili kupokea mafundisho hayo yote kwa kuwa Yehova anatufundisha ili ‘tujifaidi wenyewe.’ (Isa. 48:17) Ikiwa unahitaji kuomba ruhusa kazini, sali kwa Yehova, kisha uombe ruhusa kama Nehemia alivyofanya kwa ujasiri. (Neh. 1:11; 2:4) Pia, lingekuwa jambo la fadhili kuwajulisha watu wa familia ambao si waamini mipango yako ya kusanyiko mapema iwezekanavyo.
3 Mahali pa Kulala: Mipango inayofaa tayari imefanywa ili kuwe na mahali pa kulala katika kila mji au jiji la kusanyiko. Ushirikiano wenu mzuri utawawezesha ndugu wa kwenu wakisaidiana na ofisi ya tawi kufanya mipango ya mahali pa kulala. Tafadhali fikiria mapema mahali ambapo wewe na familia yako mngependa kukaa ili uweze kutoa habari hizo zinapohitajiwa. Ikiwa ungependa kukaa hotelini, ijulishe Idara ya Mahali pa Kulala pesa unazoweza kumlipia kila mmoja katika familia yako kwa siku moja. Kufanya hivyo kutaisaidia idara hiyo kupata hoteli iliyo karibu na mahali pa kusanyiko kwa bei nafuu kila mwaka.
4 Mahitaji ya Pekee: Mtume Paulo aliyakumbusha makutaniko huko Galatia ‘yawatendee wote mema, na hasa wale ambao katika imani ni jamaa zao.’ (Gal. 6:10) Huenda ndugu na dada wazee, wagonjwa, wazazi wasio na wenzi, na wale walio katika utumishi wa wakati wote wasikuombe msaada, lakini pengine wanahitaji kushinda magumu fulani ili kuhudhuria kusanyiko. Je, unaweza ‘kuwatendea mema’ na kuwasaidia? Wazee kutanikoni na watu wa ukoo walio Wakristo wanapaswa hasa kuzingatia hali za watu hao.
5 Mhubiri akijaza fomu ya Maombi ya Walio na Mahitaji ya Pekee, Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko ichunguze fomu hiyo kulingana na maagizo yaliyomo. Wanapaswa kuona ikiwa wanaweza kushughulikia mahitaji hayo. Ni wahubiri tu wenye msimamo mzuri pamoja na watoto wao wenye tabia nzuri wanaoweza kufaidika na mpango huo. Idara ya Mahali pa Kulala itawasiliana na mwandishi wa kutaniko ikiwa kuna maswali yoyote kuhusu ombi la mahitaji ya pekee.
6 Kuhudhuria Kusanyiko Lingine: Huenda hali zako zikakulazimu kuhudhuria kusanyiko lingine badala ya lile ambalo kutaniko lenu limepangiwa. Tafadhali mwone mwandishi wa kutaniko lenu ikiwa unahitaji habari kuhusu kusanyiko lingine. Ikiwa ungependa mahali pa kulala, tafadhali iandikie Idara ya Mahali pa Kulala ya kusanyiko hilo na uwajulishe ungependa kulala mahali pa aina gani.
7 Katika kusanyiko moja la watu wa Yehova lililofanywa miaka 2,500 hivi iliyopita, Ezra na Walawi wenzake walisoma Neno la Mungu na kuwafafanulia watu waliokusanyika. Ikawaje? Andiko la Nehemia 8:12 linatuambia kwamba ‘watu wote walienda zao wakishangilia sana, kwa maana walikuwa wameelewa maneno ambayo walijulishwa.’ Je, hatushukuru kwamba, kama Ezra na Walawi, jamii ya mtumwa iliyotiwa mafuta inatumia Neno la Mungu, inalifafanua na kutuonyesha jinsi ya kulifuata maishani? Kwa kufanya hivyo, jamii hiyo inamwiga Yehova katika kuwajali na kuwapenda kikweli watu Wake wote. Azimia kuhudhuria siku zote tatu za Kusanyiko la Wilaya la “Tembea Pamoja na Mungu”!
[Sanduku katika ukurasa wa 3]
Saa za Programu
Ijumaa na Jumamosi
3:30 asubuhi – 11:10 jioni
Jumapili
3:30 asubuhi – 10:05 jioni
[Sanduku katika ukurasa wa 4]
Jinsi Unavyoweza Kuunga Mkono Mipango ya Mahali pa Kulala
◼ Fuata sheria za kuzuia moto.
◼ Hifadhi tu vyumba ambavyo utatumia.
◼ Uwe tayari kulipa ada ya kuhifadhi chumba hotelini ikiwa utaombwa kufanya hivyo. La sivyo, huenda mtu mwingine akapewa chumba hicho.
◼ Kaa kwenye chumba ulichohifadhi kwanza.
◼ Usipike kwenye chumba ikiwa huruhusiwi kufanya hivyo.