Mkusanyiko wa Wilaya wa 2001 wa “Walimu wa Neno la Mungu” wa Mashahidi wa Yehova
1 Nabii Isaya alimtaja Yehova kuwa Mfunzi Mtukufu, ambaye kama baba, husihi hivi: “Njia ni hii, ifuateni.” (Isa. 30:20, 21) Lakini twasikiaje maneno ya Yehova yanayosemwa kwa faida yetu? Yehova husema na watu wake kupitia Biblia na vilevile vichapo vinavyotegemea Biblia, mikutano, matukio ya mzunguko, na mikusanyiko ya wilaya inayoandaliwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45) Twaweza kumshukuru Yehova kwamba anaendelea kutuelekeza katika njia ambayo twapaswa kutembea.
2 Kila mwaka mkusanyiko wa wilaya hutupatia fursa ya kukusanyika na waamini wenzetu na kusikiliza kwa makini maagizo ya Yehova. Mwaka jana, watu 58,592 walihudhuria mikusanyiko yenye kuburudisha kiroho ya “Watekelezaji wa Neno la Mungu.” Mwaka wa 2001, Mikusanyiko ya Wilaya ya “Walimu wa Neno la Mungu” ya siku tatu itafanywa. Twajua kwamba unaitazamia na unafanya mipango ya kuhudhuria, kwa hiyo twatoa habari ifuatayo ili kukusaidia.
3 Kufanya Mipango ya Mahali Pako pa Kulala: Kila mwaka tunafurahi kuwaarifu jinsi mnavyoweza kufanya mipango ya mahali pa kulala wakati wa mkusanyiko, na twathamini sana ushirikiano wenu kuhusu maagizo haya. Idara ya kwenu ya Mahali pa Kulala sikuzote huwa tayari kutosheleza mahitaji yoyote ya mahali pa kulala. Tafadhali fuateni kwa uangalifu maagizo yanayotolewa na idara hii kuhusu mahali popote pa kulala palipoandaliwa. Kwa sababu ya kanuni za moto na usalama, wale wanaolala katika madarasa au mabweni ya shule hawapaswi kupikia humo.
4 Hoteli zapatikana katika majiji na miji mingi ya mkusanyiko. Kama ungependa Idara ya Mahali pa Kulala ikutafutie mahali pa kulala hotelini, tafadhali andikia idara hii mapema ukionyesha kiasi cha pesa unachotaka kulipa kwa mtu mmoja kwa siku.
5 Ukiomba Idara ya Mahali pa Kulala ikuhifadhie chumba, tafadhali usibadilishe mpango huo na kwenda kwenye hoteli nyingine. Kufuata mwelekezo huu hutupatia fursa ya kuonyesha upendo wetu kwa ndugu zetu Wakristo na kuepuka mtazamo wa “mimi kwanza” ambao umeenea sana ulimwenguni leo.—1 Kor. 10:24.
6 Kuweka Amana Katika Hoteli, na Kushughulikia Matatizo ya Hoteli: Ili kuhakikisha unahifadhiwa chumba, hoteli kadhaa hutaka amana ilipwe kwa kila chumba unachohifadhi. Bila amana, hoteli ina haki ya kumpa mtu mwingine chumba chako. Ikiwa ndivyo ilivyo, Idara ya Mahali pa Kulala itakujulisha utaratibu wa kulipa amana. Ukipata magumu yoyote kabla na baada ya mkusanyiko, unaweza kujulisha Idara ya Mahali pa Kulala. Tatizo likitokea wakati wa mkusanyiko, wapaswa kwenda haraka iwezekanavyo kwenye Idara ya Mahali pa Kulala ya mkusanyiko ili ndugu hao wakusaidie kabla ya kuondoka hotelini.
7 Kutunza Walio na Mahitaji ya Pekee: Wazee-wazee, wadhaifu, watumishi wa wakati wote, au wengine huenda wakahitaji msaada ili wahudhurie mkusanyiko. Watu wa jamaa, wazee, na wengine katika kutaniko ambao wanajua hali za pekee za wale walio na mahitaji ya pekee wanaweza kufanya mipango inayohitajiwa kwa upendo. Familia na kutaniko halipasi kuachia wale wanaopanga mambo ya mkusanyiko daraka hilo. (1 Tim. 5:4) Fomu ya Sosaiti ya Ombi la Mahali pa Kulala kwa Wenye Mahitaji ya Pekee huonyesha matakwa yanayohitajiwa ili kujaza fomu hiyo. Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko yapasa kuchunguza sifa za kila mtu anayetoa ombi kabla ya kupeleka fomu hiyo kwenye Idara ya Mahali pa Kulala. Mwandishi wa kutaniko apaswa kuandika namba yake ya simu, ikiwa anayo, kwenye fomu hiyo ili Idara ya Mahali pa Kulala iweze kuwasiliana naye kama kuna maswali yoyote. Maombi yaliyokubaliwa yapasa kutumwa kwenye ofisi ya mkusanyiko.
8 Kuhudhuria Mkusanyiko Mwingine: Kama wahitaji kuhudhuria mkusanyiko katika sehemu nyingine, nawe wahitaji mahali pa kulala kupitia Idara ya Mahali pa Kulala, tafadhali andika mapema. Idara ya Mahali pa Kulala imepata magumu, msaada wa mahali pa kulala unapoombwa wakati huohuo.
9 Wafanyakazi wa Hoteli Wanawaonaje Mashahidi wa Yehova? Baada ya kueleza juu ya tabia nzuri ya watu wa Yehova, meneja mkuu wa hoteli moja huko Midwest, Marekani alisema: “Ninapoona Mashahidi wa Yehova wakiingia Alhamisi, ‘mimi huondoka’ hadi Jumatatu asubuhi. Najua kwamba hakutakuwa na matatizo yoyote makubwa. Inafurahisha sikuzote kuwa na watu wenu hapa.” Mwuzaji wa hoteli hiyo alisema hivi kwa mshangao: “Hiki ni kikundi kizuri ajabu! Kila mtu alikuwa akisema, ‘Asante.’” Je, huoni fahari kusikia ndugu zetu wakisifiwa kwa njia hiyo? Hebu wazia jinsi Yehova anavyofurahi anapotuona tukitenda kwa njia inayoletea jina lake sifa!
10 Umalizio: Wakati wa kuhudhuria mkusanyiko wako wa wilaya ukaribiapo, toa sala kwa Yehova ili uweze kuhudhuria vipindi vyote vya siku zote tatu na unufaike zaidi na programu hiyo. Je, tayari umeomba ruhusa ya siku tatu kazini ili uhudhurie siku zote za mkusanyiko huu uliopangia? Ikiwa hujafanya hivyo, fanya hivyo upesi iwezekanavyo. Maombi ya dakika ya mwisho kutoka kazini mara nyingi hayaruhusiwi. Mtumwa mwaminifu na mwenye busara amepanga Mkusanyiko wa Wilaya wa “Walimu wa Neno la Mungu” wa mwaka huu ili tupate maagizo ya kiroho na kujenga imani yetu. Kwa hiyo anza kufanya mipango yako sasa uhudhurie, ukifuata sihi ya mtunga-zaburi: “Mhimidini Mungu katika mikutano”!—Zab. 68:26.
[Sanduku katika ukurasa wa 3]
Saa za Programu
Ijumaa na Jumamosi
3:30 asubuhi – 11:00 jioni
Jumapili
3:30 asubuhi – 10:00 jioni