Mkusanyiko wa Wilaya wa 2002 wa “Watangazaji wa Ufalme Wenye Bidii” wa Mashahidi wa Yehova
1 “Nalifurahi waliponiambia, na twende nyumbani kwa BWANA.” (Zab. 122:1) Unapochunguza maneno ya mtunga-zaburi, ona jinsi (1) alivyohisi alipoalikwa kumwabudu Yehova, (2) mashirika mazuri aliyokuwa nayo, ambao pia walipendezwa sana na ibada ya kweli, na (3) mipango ambayo ilifanywa ili kualika watu, kuwakusanya, na kufunga safari kwenda kwenye nyumba ya Mungu.
2 Je, maneno ya mtunga-zaburi hayaonyeshi hisia zetu wenyewe tunaposikia kwamba mipango ya mkusanyiko wetu unaofuata inafanywa? Tunajawa na hamu tunapokumbuka shangwe za mikusanyiko iliyopita na tazamio la kuwapo tena kwenye mkusanyiko wa pekee pamoja na waabudu wenzetu wanaompenda Yehova. Mipango imefanywa kuwe na Mikusanyiko ya Wilaya ya siku tatu ya 2002 ya “Watangazaji wa Ufalme Wenye Bidii.” Sasa ndio wakati wa kufanya mipango yetu ya kuhudhuria mkusanyiko ili tunufaike kabisa kutokana na karamu ya kiroho inayotungojea.
3 “Msimamizi-nyumba mwaminifu, mwenye busara,” ameanza kutayarisha chakula cha kiroho cha wakati unaofaa kitakachoandaliwa mkusanyikoni. (Luka 12:42) Kila kutaniko litajulishwa ni mkusanyiko upi ambao litahudhuria ili kusiwe na watu wengi kupita kiasi kwenye kila mkusanyiko. Kuongezea, ndugu wengi wanapanga idara mbalimbali za mkusanyiko ili “mambo yote yatukie kwa adabu na kwa mpango.” (1 Kor. 14:40) Kwa kuwa mambo mengi tayari yamepangwa, sisi twaweza kufanya nini ili tujitayarishe kwenda mkusanyikoni?
4 Panga Sasa Kuhudhuria Siku Zote Tatu: Je, wahitaji kuomba ruhusu kutoka kwa mwajiri wako ili uhudhurie siku zote za mkusanyiko? Yehova anaelewa kwamba waajiri fulani ni “wagumu kupendeza.” (1 Pet. 2:18) Lakini mikusanyiko yetu ni ya maana sana, nasi tungependa kujitahidi sana ili tuhudhurie programu yote. Mfikie Yehova kwa sala kuhusu jambo hilo, ukitafuta mwongozo upate matokeo mazuri.—Neh. 2:4.
5 Tafuta Mahali pa Kulala Mapema: Iwe utakaa shuleni, kwenye bweni au hotelini, huu ndio wakati wa kuhesabu gharama na kuanza kuweka kando fedha za mambo hayo. (Luka 14:28) Ukipanga kukaa hotelini na unataka msaada wa Idara ya Mahali pa Kulala, tafadhali andikia Idara ya Mahali pa Kulala ya mkusanyiko utakaohudhuria mapema iwezekanavyo. Unaweza kuandika kupitia ofisi. Huenda ukahitajiwa kulipa amana.
6 Chunguza Hali ya Kutaniko Lenu: Ikiwa tunajua kwamba ndugu au dada ana uhitaji wa kimwili ambao huenda ukafanya iwe vigumu kuhudhuria mkusanyiko, je, tunaweza ‘kupanuka’ katika upendo wetu na kuwasaidia? (2 Kor. 6:12, 13; Kum. 15:7) Hiyo ndiyo roho ambayo Paulo alitia moyo watu wawe nayo kwenye 2 Wakorintho 8:14. Kwa nini usiwaalike watu kama hao wasafiri pamoja nawe mkusanyikoni? Ikiwa ni mapainia, yaelekea watakuwa na mambo mengi yaliyoonwa watakayosimulia safarini. Ikiwa ni ndugu au dada wazee, huenda wakawa na historia nzuri sana ya kitheokrasi ambayo hukujua mbeleni. Je, kushirikiana na ndugu na dada hawa hakutakuwa na matokeo mazuri kwako na kwa familia yako? Watathamini roho yako ya ukarimu na Yehova atakuthawabisha.—Mit. 28:27; Mt. 10:42.
7 Ijapokuwa wale wenye mahitaji ya pekee wanatunzwa na watu wao wa ukoo walio Wakristo, wazee na wengine katika kutaniko ambao wanajua mahitaji yao wanaweza kuwasaidia kwa upendo kufanya mipango hiyo. (1 Tim. 5:4) Fomu za Ombi la Mahali pa Kulala kwa Wenye Mahitaji ya Pekee zinapopelekewa Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko, halmashauri yapaswa kuchunguza sifa za kila mmoja aliyejaza ombi hilo kabla ya kuzituma kwenye Idara ya Mahali pa Kulala. Tumeni fomu zilizokubaliwa kwenye Idara ya Mahali pa Kulala ya mkusanyiko.
8 Jitolee kwa Hiari: Wakati wa mkusanyiko, mamia ya wenye kujitolea husaidia kufanya mambo yaende kwa utaratibu katika idara mbalimbali. Wakaribishaji kwenye mahali pa mkusanyiko na kwenye maegesho ya magari wanatoa mwelekezo wa kuketi nao wanachunga magari yetu siku yote. Idara ya Usafi ina pendeleo la kuendeleza sifa yetu ya usafi, ikiacha mahali petu pa ibada pa muda pakiwa safi kuliko tulivyopakuta. Je, twaweza kusaidia idara hizo au nyinginezo ambazo zaweza kuhitaji msaada wetu? Je, utajitolea kusaidia “kwa nia moja” na ndugu zako?—Sef. 3:9.
9 Je, Kweli Watu Huona Tunayofanya? Wakati wa mkusanyiko wa wilaya mwaka uliopita, mwanamume mmoja aliyekuwa ameacha kujifunza na Mashahidi wa Yehova zaidi ya miaka 20 iliyopita alikuwa akifanya kazi katika hoteli moja. Aliwaambia Mashahidi fulani kwamba sasa alikuwa anafikiria kurudia funzo lake la Biblia na kuhudhuria mikutano. Kwa nini? Kwa sababu ya jinsi alivyotendewa kwa upendo siku hizo ambazo Mashahidi walikuwa kwenye hoteli hiyo.
10 Msimamizi wa uwanja mmoja wa michezo aliwaambia hivi ndugu zetu: “Kikundi chenu ndicho kikundi bora zaidi ambacho hutumia uwanja wetu. Watu wenu wana subira sana, ni wapole na sikuzote huacha mahali hapa pakiwa safi kuliko walivyopakuta.” Baba yetu wa kimbingu hufurahi kama nini anapotuona tukifuata ushauri wa Yesu: “Acheni nuru yenu ing’ae mbele ya watu, ili wapate kuona kazi zenu bora na kumpa utukufu Baba yenu aliye katika mbingu”!—Mt. 5:16.
11 Na tuige mtazamo wa Mfalme Daudi, ambaye kwa shangwe alitarajia kwenda kwenye nyumba ya ibada ya Yehova. Mikusanyiko yetu ya wilaya ni chanzo muhimu cha chakula cha kiroho na fursa ya pekee ya ushirika wenye upendo. Kwa hiyo, twakualika kwa moyo mchangamfu uanze kufanya mipango yako ya kuhudhuria vipindi vyote vya siku zote tatu vya mkusanyiko wa Wilaya wa mwaka huu wa “Watangazaji wa Ufalme Wenye Bidii”!
[Sanduku katika ukurasa wa 3]
Saa za Programu
Ijumaa na Jumamosi
3:30 asubuhi – 11:00 jioni
Jumapili
3:30 asubuhi – 10:00 jioni