Makusanyiko ya 2003 ya Wilaya ya Mashahidi wa Yehova ya “Mtukuzeni Mungu”
1 Yehova aliamuru hivi kupitia nabii wake mwaminifu Isaya: “Nisikilizeni mimi, enyi watu wangu; nisikieni, taifa langu.” (Isa. 51:4) Katika wakati huu wa mwisho unaoendelea kuwa mgumu, je, hatukubali kwamba kusikiliza amri za Yehova ni jambo la maana zaidi? Mojawapo ya njia ambazo ‘tunamsikiliza’ Yehova ni kutii amri yake ya kukutana ili kumwabudu. Kwa kweli sisi hutazamia kwa hamu sana fursa za pekee za kuwa na makusanyiko yetu ya wilaya! Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova limepanga tena makusanyiko mengi ya wilaya yatakayofanywa katika eneo letu mwaka wa 2003.
2 Kama ilivyoonyeshwa katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 2002, makusanyiko ya kimataifa yatafanywa katika majiji yaliyoteuliwa, huku wajumbe wakihudhuria kutoka ulimwenguni pote. Kwa kuwa ni majiji machache yatakayokuwa na makusanyiko ya kimataifa, ni makutaniko yaliyoagizwa kwenda kwenye makusanyiko hayo yatakayoweza kuhudhuria tu. Kama tulivyojulishwa mapema, tumealikwa kutuma wajumbe kwenye makusanyiko ya kimataifa yaliyopangwa kufanywa Afrika Kusini. Lakini ushirika huo wa kimataifa utahisiwa katika makusanyiko yote ya wilaya. Kutakuwapo na mishonari katika makusanyiko mengi, na kutakuwapo na fursa ya kusikia baadhi ya mambo yao yaliyoonwa. Twaweza kufanya nini ili tunufaike kabisa na mipango inayofanywa sasa kwa ajili ya makusanyiko yetu?
3 Hudhuria Kila Siku: Ili tunufaike kabisa na mafundisho yatokayo kwa mtumwa mwaminifu na mwenye busara, twataka kuhakikisha kwamba tunahudhuria programu yote ya kusanyiko. (Mt. 24:45) Je, wahitaji kumwomba mwajiri wako ruhusa ya kuhudhuria siku zote za kusanyiko? Kabla ya Nehemia kumwomba Mfalme Artashasta ruhusa ya kwenda Yerusalemu kujenga kuta, ‘alimwomba Mungu wa mbinguni.’ (Neh. 2:4) Vivyo hivyo wapaswa kumwomba Yehova akupe ujasiri wa kumwomba ruhusa mwajiri wako ili uhudhurie siku zote tatu za kusanyiko. Vipi mwajiri wako akisitasita kukupa ruhusa? Labda atakubali ukimweleza kwamba mafundisho tunayopokea kwenye makusanyiko yetu hutusaidia kuwa wanyofu, wenye bidii na wafanyakazi wenye kutumainika. Kwa kuongezea, kama tuna washiriki wa familia wasioamini, lingekuwa jambo lenye upendo kuwajulisha mipango yetu ya kusanyiko mapema iwezekanavyo.
4 Shirikiana na Idara ya Mahali pa Kulala: Idara ya Mahali pa Kulala itashughulikia mahali pa kulala mapema vya kutosha. Ikiwa ungependa kukaa hotelini tafadhali andikia idara hiyo mapema ukionyesha ni pesa ngapi unazoweza kulipa na kwa siku ngapi. Ili uhakikishe kwamba umewekewa nafasi, huenda ukahitaji kulipa pesa za kushikilia nafasi. Ikiwa jambo hilo latakikana, jitayarishe kufanya hivyo.
5 Kuwasaidia Walio na Mahitaji ya Pekee: Je, katika kutaniko lenu kuna wale ambao huenda wakahitaji msaada wa kuhudhuria kusanyiko? Mahitaji ya pekee ya walio na umri mkubwa zaidi, wagonjwa, au walio katika utumishi wa wakati wote yanashughulikiwa hasa na watu wa ukoo walio Wakristo, lakini wazee na wengine ambao wanajua hali za watu hao wanaweza pia kuwasaidia kwa upendo.
6 Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko itachunguza fomu zote za Maombi ya Walio na Mahitaji ya Pekee zinazotolewa na wahubiri. Wakitumia miongozo iliyo katika fomu hiyo, walio katika halmashauri ya utumishi wanapaswa kuchunguza waone kama kila ombi lililofanywa ni la uhitaji wa pekee. Mpango huo ni wa wahubiri walio na msimamo mzuri tu, pamoja na watoto wao wenye mwenendo mzuri. Idara ya Mahali pa Kulala itawasiliana na mwandishi wa kutaniko ikiwa kuna maswali yoyote kuhusu ombi la pekee.
7 Kuhudhuria Kusanyiko Lingine: Hali zako zikikulazimu uhudhurie kusanyiko lingine mbali na lile unalopaswa kuhudhuria na ikiwa utahitaji mahali pa kulala, tafadhali mwone mwandishi wa kutaniko lenu, ambaye atakusaidia kujua mahali unapoweza kutuma barua yako ya kuomba mahali pa kulala hotelini.
8 Sisi Ni Watu wa Kutazamwa na Wote: Je, watu huona tofauti kati ya Mashahidi wa Yehova na watu wengine wa ulimwengu huu? Bila shaka! Angalia baadhi ya maelezo kutoka kwa wasimamizi wa hoteli katika jiji moja: “Sikuzote tumeshughulika na wakusanyikaji, lakini nyinyi ndio mnaoshirikiana nasi zaidi na wenye fadhili kuliko wote.” “Juma lililopita tulikuwa na kikundi kingine cha kidini hapa. Kuna tofauti kubwa sana kati yenu nao.” “Twajua kwamba sikuzote twaweza kuwa na hakika kwamba mtatusaidia na kushirikiana nasi.” Je, maelezo hayo hayatusaidii kuona jinsi “hekima ya kutoka juu” inavyoboresha utu wetu? (Yak. 3:17) Kwa kuwa sisi “tumekuwa kitu cha kutazamwa mahali pa michezo kwa ulimwengu,” mwenendo wetu na udhihirishe sikuzote adhama na utukufu wa Mungu wetu Yehova.—1 Kor. 4:9.
9 Kwa kuwa “mandhari ya ulimwengu huu inabadilika,” twahitaji makusanyiko ya wilaya ya kutusaidia twendelee kuwa macho kiroho. (1 Kor. 7:31) Kufanya mipango ya kuhudhuria siku zote kutahitaji jitihada, lakini jitihada hizo zinafaa. Kusanyiko la Wilaya la mwaka huu lenye kichwa “Mpe Mungu Utukufu” limetayarishwa kutusaidia tudumu tukiwa imara tunapongojea kutekelezwa kwa hukumu ya Yehova dhidi ya ulimwengu huu wa Shetani. Tusiache kamwe kitu chochote kituzuie kupata mafundisho ambayo Yehova ametutayarishia.—Isa. 51:4, 5.
[Sanduku katika ukurasa wa 3]
Saa za Programu
Ijumaa na Jumamosi
3:30 asubuhi – 11:00 jioni
Jumapili
3:30 asubuhi – 10:05 jioni