Mkusanyiko wa Wilaya wa 2000 wa “Watekelezaji wa Neno la Mungu” wa Mashahidi wa Yehova
1 “Nitakushukuru katika kusanyiko kubwa; nitakusifu kati ya watu wengi.” (Zab. 35:18) Hebu wazia jinsi ambavyo Daudi angesisimka leo kuona maelfu wengi wakikusanyika pamoja kwa amani ili kufundishwa kwenye mikusanyiko yetu! Je, ulikuwa miongoni mwa watu 61,000 waliohudhuria mojawapo ya Mikusanyiko ya Wilaya ya “Neno la Mungu la Kiunabii”? Kuanzia mwanzo-mwanzo wa Agosti hadi katikati ya Septemba 1999, jumla ya mikusanyiko 32 ilifanywa katika miji na majiji 25 katika nchi 6 zilizo chini ya ofisi yetu ya tawi. Mikusanyiko yetu ya wilaya mwaka wa 2000 itatuandalia fursa mpya za kukusanyika na wenzetu wanaomsifu Yehova ambao wanaona “uhitaji wao wa kiroho” na wana furaha na hamu ya ‘kusikia lile ambalo roho huyaambia makutaniko.’—Mt. 5:3; Ufu. 2:29.
2 Kupanga Mahali Pako pa Kulala: Kila mwaka, tunafurahi kuwaarifu jinsi mnavyoweza kupanga mahali mtakapolala wakati wa mkusanyiko, na twathamini sana ushirikiano wenu kuhusu maagizo haya. Idara ya kwenu ya Mahali pa Kulala sikuzote huwa tayari kutosheleza mahitaji yoyote ya mahali pa kulala. Tafadhali fuateni kwa uangalifu maagizo yanayotolewa na idara hii kuhusu mahali popote pa kulala palipoandaliwa. Kwa sababu ya kanuni za moto na usalama, wale wanaolala katika madarasa au vyumba vya shule vya kulala hawapaswi kupika humo.
3 Hoteli zapatikana katika mengi ya majiji na miji ya mkusanyiko. Kama ungependa Idara ya Mahali pa Kulala ikutafutie mahali pa kulala katika hoteli, tafadhali andikia idara hii mapema ukionyesha kiwango cha pesa unachotaka kulipa kwa mtu mmoja kwa siku.
4 Ukiomba Idara ya Mahali pa Kulala ikuhifadhie chumba katika hoteli fulani, tafadhali usibadilishe mpango huo na kwenda kwenye hoteli nyingine. Kufuata mwelekezo huu hutupatia fursa ya kuonyesha upendo wetu kwa ndugu zetu Wakristo na kuepuka mtazamo wa “mimi kwanza” ambao umeenea sana ulimwenguni leo.—1 Kor. 10:24.
5 Kuweka Amana Katika Hoteli na Kushughulikia Matatizo ya Hoteli: Ili kuhakikisha unahifadhiwa chumba, hoteli kadhaa hutaka amana ya kila chumba unachohifadhi. Bila amana, hoteli ina haki ya kumpa mtu mwingine chumba chako. Ikiwa hivyo, Idara ya Mahali pa Kulala itakujulisha jinsi ya kupeleka amana. Ukipata magumu yoyote kabla na baada ya mkusanyiko, unaweza kujulisha Idara ya Mahali pa Kulala. Tatizo likitokea wakati wa mkusanyiko, wapaswa kwenda kwenye Idara ya Mahali pa Kulala ya mkusanyiko mara moja iwezekanavyo ili ndugu hao wakusaidie kabla ya kuondoka hotelini.
6 Kutunza Walio na Mahitaji ya Pekee: Watu wa jamaa, wazee, na wengine katika kutaniko ambao wanajua hali za pekee za wazee-wazee, wadhaifu, watumishi wa wakati wote, au wengine walio na mahitaji ya pekee wanaweza kuonyesha upendo na kujali kwa kuwasaidia wahudhurie mkusanyiko. (Linganisha 1 Timotheo 5:4.) Fomu ya Sosaiti ya Ombi la Mahali pa Kulala kwa Wenye Mahitaji ya Pekee huonyesha matakwa yanayohitajiwa ili kuleta fomu hiyo. Uandalizi huu ni wa wahubiri wenye msimamo mzuri tu, kutia ndani wale ambao wana watoto wenye tabia nzuri, ambao wameidhinishwa na Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko. Maombi hayo yapasa kutumwa kwa Idara ya Mahali pa Kulala mara moja iwezekanavyo.
7 Kuhudhuria Mkusanyiko Mwingine: Kama wahitaji kuhudhuria mkusanyiko katika sehemu nyingine, nawe wahitaji mahali pa kulala kupitia Idara ya Mahali pa Kulala, tafadhali andika mapema. Idara ya Mahali pa Kulala imepata magumu, msaada wa mahali pa kulala unapoombwa wakati huohuo.
8 Panga Kuhudhuria Siku Zote Tatu: Je, Shetani amejaribu kukukengeusha usikazie fikira mambo ya kiroho? Kwa kusikitisha, ndugu na dada wengi na familia zao wanakosa chakula muhimu cha kiroho. Jinsi gani? Kwa kutohudhuria vipindi vya Ijumaa vya mkusanyiko wa wilaya. Katika visa fulani imeonekana kwamba asilimia kubwa ya akina ndugu wanakosa mafundisho ya kiroho na ushirika ambao huandaliwa katika vipindi vya Ijumaa.
9 Inawezekana kwamba akina ndugu fulani husita kuwafikia waajiri wao kuomba nafasi ya kuhudhuria mkusanyiko. Je, hivyo ndivyo wewe hufanya? Mbona usisali kwa Yehova juu ya jambo hilo na uwe mwenye moyo mkuu wa kumweleza mwajiri wako hali yako? Kumbuka matokeo mazuri ya Nehemia, ambaye alikuwa katika hali kama hiyo. (Neh. 2:1-6) Uwe na imani kwamba Baba wa mbinguni yu tayari kukusaidia, ukijua kwamba ukitanguliza masilahi ya Ufalme, atakuandalia mahitaji ya lazima ya maisha.—Mt. 6:32b, 33.
10 Mikusanyiko Yetu Hukuathirije? Dada mmoja kutoka mashariki mwa Marekani aliandika hivi: “Asanteni sana kwa mkusanyiko wa wilaya wa 1999. Kushirikiana na akina ndugu ambao mimi huwaona mara moja tu kwa mwaka huniletea shangwe. Nilipata kweli nikiwa tineja mwenye mimba, nami nakumbuka kwa furaha sana aliyejifunza nami Biblia aliponipeleka kwenye mkusanyiko wangu wa kwanza. Nilitazama mawingu katika stediamu hiyo iliyokuwa wazi tulipoimba wimbo wa Ufalme ‘Ndugu Makumi ya Elfu,’ nami nikatoa machozi. ‘Kukiwa na watu hawa wenye kupendeza kando-kando yangu,’ nikajiuliza, ‘Yehova anawezaje kunitaka?’ Siku hiyo nikaamua kumtumikia Yehova kabisa.” Inachangamsha moyo kama nini! Kwa kweli ni jambo lenye kupendeza kushirikiana na watu safi wa Yehova, sivyo?
11 Tukiwa katika sehemu ya kumalizia ya siku za mwisho, twahitaji mkusanyiko wetu wa wilaya wa kila mwaka zaidi ya wakati mwingine wowote. Ni uandalizi kutoka kwa Yehova kudumisha afya na usawaziko wetu wa kiroho. Kwa hiyo, azimia kuhudhuria sikuzote tatu za Mkusanyiko wa Wilaya wa mwaka huu wa “Watekelezaji wa Neno la Mungu.” Waweza kuendeleaje mpaka mwisho na azimio lako? Mwombe mwajiri wako mapema akupe ruhusa ya kuhudhuria mkusanyiko wote. Ikiwa huna hela za kutosha, anza sasa kuweka kando fedha zinazohitajiwa ili uhudhurie. Mwombe Yehova msaada ushinde kizuizi chochote. Ukifanya hivyo, waweza kutazamia kufurahia ushirika mchangamfu wa ndugu na dada zako na kusikia semi za uhai wa milele kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni, Yehova.—Linganisha Yohana 6:68.
[Sanduku katika ukurasa wa 3]
Saa za Programu
Ijumaa na Jumamosi
3:30 asubuhi – 11:00 jioni
Jumapili
3:30 asubuhi – 10:00 jioni