“Makusanyiko ya Wilaya ya Mashahidi wa Yehova ya 2005 ya ‘Utii wa Kimungu’”
1 Kwa kuwa Yehova Mungu ndiye Mfunzi wetu Mtukufu, yeye hupanga tukusanyike pamoja ili tufundishwe katika njia zake. (Isa. 30:20, 21; 54:13) Yeye hufanya hivyo kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara, ambayo hupanga kuwe na mikutano kama vile makusanyiko yetu ya wilaya ya kila mwaka. (Mt. 24:45-47) Tuna maoni kama ya mtunga-zaburi Daudi aliyeimba: “Kati ya makundi yaliyokutanika nitambariki Yehova.” (Zab. 26:12) Daudi alielewa vizuri umuhimu wa kufundishwa na Yehova, naye aliazimia kuwa miongoni mwa watu Wake wakati walipokusanyika pamoja.
2 Je, utakuwa kati ya “makundi yaliyokutanika” ambayo yatahudhuria Makusanyiko ya Wilaya ya “Utii wa Kimungu” mwaka huu? Ikiwa ndivyo, habari ifuatayo itakusaidia unapofanya mipango ya kuhudhuria.
3 Panga Sasa Uhudhurie Kila Siku: “Mipango ya mwenye bidii bila shaka huleta faida.” (Met. 21:5) Maneno hayo yanakazia umuhimu wa kufanya mipango bila kukawia ili uhudhurie. Ili kuhakikisha kwamba hutakosa sehemu yoyote ya kusanyiko hilo lenye kuchochea kiroho, lingekuwa jambo la hekima kuanza sasa kufanya mipango yoyote inayohitajiwa ili kuhudhuria siku zote tatu. Ikiwa ni lazima uombe ruhusa kazini, fanya hivyo bila kukawia. Iwapo utahitaji kuzungumzia mipango yako pamoja na mwenzi wako wa ndoa asiyeamini, usingoje hadi dakika ya mwisho. Hata uwe na matatizo gani, sali kwa Yehova, ukitumaini kwamba kwa msaada wake “mipango yako itafanywa imara.” (Met. 16:3) Zaidi ya hayo, ingefaa kuwasaidia wanafunzi wako wa Biblia wanapofanya mipango ya kuhudhuria vipindi vyote.
4 Mahali pa Kulala: Mipango inayofaa tayari imefanywa ili kuwe na mahali pa kulala katika kila mji au jiji la kusanyiko. Ushirikiano wenu mzuri huwasaidia ndugu wa Idara ya Mahali pa Kulala kufanya mipango hiyo. Kwa hiyo, tafadhali fikiria mapema mahali ambapo wewe na familia yako mngependa kulala. Kama ungependa kukaa hotelini, tafadhali hakikisha kwamba umeijulisha Idara ya Mahali pa Kulala pesa unazoweza kumlipia kila mmoja katika familia yako kwa kila siku.
5 Mahitaji ya Pekee: Mtume Paulo alisema kwamba ndugu fulani walikuwa ‘msaada wenye kumtia nguvu.’ (Kol. 4:7-11) Njia moja ambayo ndugu hao walimsaidia Paulo ni kwa kumhudumia kuhusiana na mahitaji yake ya kibinafsi. Unawezaje kuwa ‘msaada wenye kuwatia nguvu’ wengine kuhusiana na kusanyiko? Huenda wahubiri waliozeeka, wagonjwa, watumishi wa wakati wote, na wengineo wakahitaji kusaidiwa kuhusiana na usafiri au mahali pa kulala. Watu wa ukoo ndio wana daraka kubwa la kuwashughulikia watu hao. (1 Tim. 5:4) Hata hivyo, ikiwa hawawezi kufanya hivyo, wanaweza kusaidiwa na waamini wenzao. (Yak. 1:27) Waangalizi wa funzo la kitabu wanapaswa kuzungumza na wale walio na mahitaji ya pekee katika kikundi chao ili kuhakikisha kwamba wamefanya mipango yao mapema kabla ya kusanyiko.
6 Fomu za Ombi la Mahali pa Kulala kwa Wenye Mahitaji ya Pekee zinapatikana tu kwa ajili ya wahubiri ambao mahitaji yao ya mahali pa kulala hayawezi kushughulikiwa na watu wa familia zao au kutaniko. Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko inapaswa kuchunguza sifa za mhubiri, wakitumia miongozo kwenye fomu hiyo. Ni wahubiri wenye msimamo mzuri tu pamoja na watoto wao wenye tabia nzuri wanaoweza kufaidika na mpango huo.
7 Kuhudhuria Kusanyiko Lingine: Ili kuhakikisha kwamba hakuna upungufu wa viti, vichapo, mahali pa kulala, na kadhalika, wahubiri wanatiwa moyo wahudhurie kusanyiko ambalo kutaniko lao limepangiwa kuhudhuria. Iwapo hali zako zinakulazimu kuhudhuria kusanyiko lingine, tafadhali mwone mwandishi wa kutaniko lenu.
8 Wajitoleaji Wahitajiwa: Yesu aliweka kielelezo kizuri kwa kushughulikia mahitaji ya wengine kwa unyenyekevu. (Luka 9:12-17; Yoh. 13:5, 14-16) Wale ambao hujitolea kufanya kazi makusanyikoni huonyesha roho kama hiyo. Kwenye kusanyiko moja mwaka uliopita, asilimia 20 ya wahudhuriaji walijitolea kufanya kazi kupitia Idara ya Utumishi wa Kujitolea. Hivi karibuni, ndugu katika Halmashauri ya Kusanyiko watawakaribisha wengine kufanya kazi pamoja nao ili kusiwe na upungufu wa wafanyakazi kwenye idara za makusanyiko. Wazee hasa wanahitaji kujitolea na kukubali migawo mbalimbali. Roho yao ya kujitolea ni kielelezo kizuri kwa wote kutanikoni.—1 Pet. 5:2, 3.
9 Yale Ambayo Wengine Huona: Meneja wa mauzo katika hoteli fulani alisema hivi kuhusu Mashahidi: “Tunawapenda sana. Mwenendo wenu ni mzuri sana unapolinganishwa na wa wengine. Wale wanaotunza nyumba hueleza jinsi wanavyotendewa vizuri na kupewa bakshishi. Hata kila mfanyakazi hutaka kuwa kazini mwisho-juma ambao mnakuwa hapa!” Mwakilishi mwingine wa hoteli alisema: “Ni rahisi sana kuwashughulikia Mashahidi wa Yehova.” Ofisa mmoja aliyesimamia mahali ambapo makusanyiko yalifanywa mwaka uliopita alisema, “Mliacha mahali hapa pakiwa safi zaidi kuliko mlivyopapata. Watu walikula chakula chao hapo lakini hakuna makaratasi yaliyotapakaa. Watoto walikuwepo pia, lakini vyoo viliachwa vikiwa safi. Nilikuwa nimesikia kwamba Mashahidi wa Yehova ni watu safi na nadhifu, lakini sasa nimeamini kabisa. Mnakaribishwa tena.” Labda maneno hayo yalisemwa kwa sababu ya mwenendo wako mzuri. Wazia jinsi Yehova anavyofurahi anapoona tukitenda kwa njia ambayo huleta sifa kama hizo!—1 Pet. 2:12.
10 Kupitia “msimamizi-nyumba mwaminifu,” Yehova Mungu amepanga ili watu wake wakusanyike mwaka ujao kwa ajili ya mafundisho ya kiroho. (Luka 12:42) Tunahitaji kujitahidi katika mipango yetu ya kuhudhuria siku zote tatu, lakini jitihada hizo hazitakuwa za bure. Makusanyiko ya Wilaya ya “Utii wa Kimungu” yataimarisha azimio letu la kumtumikia Yehova sasa na milele. Na tuazimie kufuata himizo hili la mtunga-zaburi: “Katika makundi yaliyokutanika mbarikini Mungu.”—Zab. 68:26.
[Sanduku katika ukurasa wa 3]
Saa za Programu
Ijumaa na Jumamosi
3:30 asubuhi - 11:05 jioni
Jumapili
3:30 asubuhi - 10:10 jioni