Kusanyiko la Wilaya la Mashahidi wa Yehova la 2007 la “Mfuateni Kristo!”
1 Musa aliwaamuru Waisraeli na wakaaji wageni wote wakusanyike pamoja kila baada ya miaka saba ili wasomewe Sheria. Kwa kusudi gani? “Ili wasikilize na ili wajifunze.” (Kum. 31:10-12) Yehova aliona uhitaji wa watu wake kukusanyika pamoja katika vikundi vikubwa. Hivi karibuni, watu wa Yehova watakusanyika tena kwa siku tatu kwa ajili ya Makusanyiko ya Wilaya ya “Mfuateni Kristo!”
2 Je, umeanza kufanya matayarisho? Je, unahitaji kumwomba mwajiri wako ruhusa? Je, unaweza kuwasaidia wanafunzi wako wa Biblia au watu wa familia yako ambao si Mashahidi wahudhurie kusanyiko pamoja nawe? Je, kuna wengine katika kutaniko wanaohitaji msaada ili waweze kuhudhuria? Je, unapanga kuhudhuria kusanyiko lingine badala ya lile ambalo kutaniko lenu limepangiwa? Utahitaji mahali pa kulala? Habari ifuatayo itakusaidia kufanya matayarisho.
3 Hudhuria Siku Zote Tatu: Yehova huwaandalia watu wake chakula kingi cha kiroho. (Isa. 25:6) Chakula hicho kinatia ndani karamu ya kiroho ambayo huandaliwa katika makusanyiko yetu ya kila mwaka. Imeonekana kwamba hudhurio la siku ya Ijumaa huwa chini sana ikilinganishwa na siku zile nyingine. Azimia kuhudhuria siku zote tatu za kusanyiko lenye kuburudisha ambalo tengenezo la Yehova limetuandalia! Ikiwa unahitaji kumwomba mwajiri wako ruhusa, sali kuhusu jambo hilo. Kisha ‘jipe ujasiri’ na uzungumze na mwajiri wako mara tu tarehe ya kusanyiko utakalohudhuria itakapotangazwa. (1 The. 2:2; Neh. 2:4, 5) Huenda ikasaidia ukimweleza kwamba makusanyiko yanayofanywa kila mwaka ni sehemu ya ibada yako. Ukifanya hivyo mapema utamwezesha mwajiri wako afanye mabadiliko kazini ili kutimiza ombi lako.
4 Kuwatayarisha Wanafunzi Wako wa Biblia na Familia Yako: Ingefurahisha sana kuhudhuria kusanyiko pamoja na wanafunzi wako wa Biblia ili wajionee wenyewe upendo wa undugu wetu wa Kikristo “katika kutaniko kubwa”! (Zab. 22:25) Wajulishe mapema ili watenge wakati wa kuhudhuria kusanyiko. Waeleze ni kwa nini wewe hufurahia kuhudhuria makusanyiko. Unaweza kuwatayarisha wanafunzi wa Biblia kwa kuwaonyesha video zetu ambazo huonyesha makusanyiko yaliyopita, hasa video United by Divine Teaching, ikiwa inapatikana. Mahali ambapo video hazipatikani, unaweza kutumia picha kwenye ukurasa wa 18 katika broshua Mashahidi wa Yehova—Wanafanya Mapenzi ya Mungu kwa Umoja Ulimwenguni Pote. Wajulishe watu wa familia ambao si Mashahidi mipango yako. Huenda wakapanga kuja kutazama drama au kuhudhuria kusanyiko pamoja nawe kwa angalau siku moja.
5 Kuwasaidia Ndugu na Dada Zako: Mtume Paulo aliwashauri Wakristo ambao walikuwa matajiri kimwili “wafanye mema, wawe matajiri katika matendo mazuri, wawe wakarimu, tayari kushiriki.” (1 Tim. 6:17, 18) Tunaweza kuonyesha roho ya ukarimu ambayo Paulo alipendekeza kwa kufikiria mahitaji ya walio wazee, wagonjwa, watumishi wa wakati wote, familia zilizo na mzazi mmoja tu, na pengine wengine katika kutaniko ambao huenda wakahitaji msaada ili waweze kuhudhuria kusanyiko. Ni jukumu la watu wa ukoo walio katika kweli kuwashughulikia watu hao, lakini wazee na wengine wanaweza kutumia busara na kusaidia ikihitajika.—Gal. 6:10; 1 Tim. 5:4.
6 Ikiwa kuna yeyote kutanikoni anayehitaji kusaidiwa kutafuta mahali pa kulala, Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko inapaswa kuamua ikiwa mhubiri huyo anastahili kujaza fomu ya Ombi la Mahali pa Kulala kwa Wenye Mahitaji ya Pekee.
7 Kuhudhuria Kusanyiko Lingine: Huduma Yetu ya Ufalme ya Februari 2007 itakuwa na orodha ya makusanyiko yote yatakayofanywa Afrika Mashariki. Ikiwa unahitaji habari zaidi kuhusu kusanyiko lingine tofauti na lile ambalo kutaniko lenu limepangiwa, unaweza kuwaandikia wale wanaosimamia kusanyiko hilo ukitumia anwani ambayo mwandishi wa kutaniko lenu atapata nyuma ya fomu ya karibuni ya Ombi la Mahali pa Kulala kwa Wenye Mahitaji ya Pekee. Ili wasimamizi wa kusanyiko hilo wakujibu, hakikisha kwamba umetia ndani bahasha iliyo na stempu.
8 Kuhifadhi Vyumba vya Hoteli: Ikiwa ungependa kukaa hotelini na unataka Idara ya Mahali pa Kulala ikusaidie kupata hoteli inayofaa kwenye mji au jiji la kusanyiko, tafadhali andikia Idara ya Mahali pa Kulala mapema. Taja pesa ambazo ungependa kulipia mtu mmoja kila siku. Eleza ikiwa utakula milo yote hotelini, au unataka tu chumba na kiamsha kinywa, au chumba peke yake.
9 Fuata Mipango Iliyofanywa: Tunapofika mahali pa kusanyiko, sisi huona kwamba kazi nyingi imefanywa ili kututayarishia mahali hapo. Ndugu wenye upendo wanaotumikia kama wakaribishaji hutusalimu, hutupatia programu, na kutusaidia kupata mahali pa kuketi. Ndugu na dada huwa wamesafisha mahali hapo na kutengeneza jukwaa maridadi. Kazi muhimu isiyoonekana waziwazi imefanywa kutayarisha sehemu za programu, kuzungumza na wasimamizi wa hoteli ili watupe bei nafuu, na kushughulikia mambo mengine mengi.
10 Kwa kila kusanyiko, ndugu wengi huwa wamefanya kazi kwa miezi kadhaa kufanya matayarisho yanayohitajika, na familia zao huwa zimechangia kwa kuwaruhusu washughulikie mambo hayo muhimu. Je, hatuthamini jinsi ambavyo ndugu hao wamejidhabihu kwa faida yetu? Tunaweza kuonyesha uthamini wetu kwa kufuata maagizo ambayo yametolewa katika makala hii na mwongozo zaidi ambao huenda tukapokea kabla ya kusanyiko. (Ebr. 13:17) Ushirikiano wa kila mtu hufanya mambo yote “yatendeke kwa adabu na kwa mpango.”—1 Kor. 14:40.
11 Kadiri ‘tunavyoona siku ile kuwa inakaribia’ ndivyo inavyokuwa muhimu hata zaidi kwa watu wa Mungu kukusanyika pamoja. (Ebr. 10:25) Katika makusanyiko yetu ya Kikristo, mtumwa mwaminifu na mwenye busara hutuandalia habari ambayo itatusaidia “kuyatimiza maneno yote” ambayo Yehova anataka tufanye. (Kum. 31:12) Anza sasa kufanya mipango ya kuhudhuria siku zote tatu za Kusanyiko la Wilaya la “Mfuateni Kristo!” na hivyo ufaidike na mafundisho ya kiroho na ushirika mchangamfu!
[Maswali ya Funzo]
1, 2. (a) Musa aliwatiaje moyo Waisraeli wanufaike kwa kukusanyika pamoja? (b) Tunahitaji kuanza kufanya matayarisho gani sasa?
3. (a) Andiko la Isaya 25:6 linatimizwaje leo? (b) Ni jambo gani limeonekana kuhusu hudhurio la siku ya Ijumaa ya kusanyiko, na kila mmoja wetu anapaswa kufanya nini?
4. Tunaweza kuwatayarishaje wanafunzi wetu wa Biblia na watu wa familia ambao si Mashahidi kwa ajili ya kusanyiko?
5, 6. (a) Tunaweza kuonyeshaje roho ya ukarimu inayotajwa kwenye 1 Timotheo 6:18? (b) Kuna maandalizi gani ya kuwasaidia wale ambao huenda wakahitaji mahali pa kulala?
7. Ni utaratibu gani ambao umetolewa ikiwa tutahitaji kuhudhuria kusanyiko lingine badala ya lile ambalo kutaniko letu limepangiwa?
8. Tunapaswa kufuata miongozo gani ikiwa tunapanga kukaa hotelini?
9, 10. (a) Ni matayarisho gani huwa yamefanywa kabla hatujafika mahali pa kusanyiko? (b) Tunaweza kuonyeshaje uthamini na shukrani kwa kazi yote ambayo imefanywa kwa ajili yetu? (Soma Waebrania 13:17.)
11. (a) Kwa nini makusanyiko ya watu wa Yehova ni muhimu sana katika siku zetu? (b) Kila mmoja wetu anaweza kufanya nini sasa?
[Sanduku katika ukurasa wa 3]
Saa za Programu
Ijumaa na Jumamosi
3:20 asubuhi - 11:05 jioni
Jumapili
3:20 asubuhi - 10:10 jioni