Kusanyiko la Wilaya la Mashahidi wa Yehova la 2008
1 Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo Waebrania kukusanyika pamoja na kutiana moyo “na kufanya hivyo zaidi” kwa kadiri walivyoona siku ile kuwa inakaribia. (Ebr. 10:24, 25) Uthibitisho unaonyesha kwamba “siku ile” ambayo Paulo aliizungumzia iko karibu sana! Ndiyo maana sisi hutazamia kwa hamu kukutanika pamoja na ndugu na dada zetu kwa ajili ya elimu ya kiroho ambayo inaweza kutuongoza tupite kwenye ‘siku hizi za mwisho’ zilizo hatari. (2 Tim. 3:1) Fursa kama hiyo itapatikana kwenye kusanyiko la wilaya la 2008.
2 Hudhuria Siku Zote Tatu: Tunakutia moyo uhudhurie siku zote tatu. “Bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe,” hatutakosa chakula muhimu cha kiroho. (Ebr. 10:25) Anza kufanya matayarisho haraka iwezekanavyo. Ni jambo muhimu kumtaarifu mwajiri wako mapema ili aweze kufanya mipango yoyote inayohitajika. Ikiwa watoto wako watakuwa bado hawajafunga shule, waarifu walimu kuhusu mipango yako. Wajulishe kwamba kusanyiko ni sehemu ya kawaida ya ibada yako. Yehova atakubariki unapoendelea kutanguliza masilahi ya Ufalme kwanza.—Mt. 6:33.
3 Wasaidie Wengine Wahudhurie: Paulo pia aliwahimiza akina ndugu ‘wafikiriane.’ (Ebr. 10:24) Je, ndugu na dada katika Funzo lako la Kitabu la Kutaniko wanahitaji msaada ili wahudhurie kusanyiko? Je, unaweza kuwasaidia wanafunzi wako wa Biblia wahudhurie kusanyiko, hata ikiwa ni kwa siku moja? Unapowataarifu watu wa familia yako ambao si waamini kuhusu mipango yako ya kusanyiko, wakaribishe wahudhurie pamoja nawe. Jitihada zako zinaweza kuleta baraka zisizotarajiwa.
4 Jinsi ya Kupata Habari: Kila mwaka watu wengi hupiga simu kwenye ofisi ya tawi wakiuliza kuhusu mahali na wakati kusanyiko la wilaya litafanywa. Karibu simu hizo zote hutoka kwa ndugu na dada ambao tayari wamepata habari hizo. Kabla ya kupiga simu kwenye ofisi ya tawi tunapendekeza uchunguze kwanza gazeti la Mnara wa Mlinzi la Machi 1, 2008 au Huduma Yetu ya Ufalme ya Februari 2008.
5 Ikiwa utahudhuria kusanyiko tofauti na lile ambalo kutaniko lako limepangiwa, unaweza kupata habari kuhusu mahali pa kulala kwa kuwaandikia ndugu wanaohusika ukitumia anwani zilizoonyeshwa nyumba ya fomu ya Ombi la Mahali pa Kulala kwa Wenye Mahitaji ya Pekee. Fomu hizo zitatumwa kwa waandishi wa makutaniko. Ili kupata jibu la ombi lako, unapaswa kuambatanisha barua yako na stempu na bahasha yenye anwani yako.
6 Mahitaji ya Pekee: Ikiwa mhubiri ameomba asaidiwe kupata mahali pa kulala, Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko inapaswa kuamua ikiwa mhubiri huyo anastahili kujaza fomu ya Ombi la Mahali pa Kulala kwa Wenye Mahitaji ya Pekee. Kabla ya mwandishi wa kutaniko kutuma fomu hiyo kwa Idara ya Mahali pa Kulala, miongozo inayopatikana kwenye fomu hiyo na kwenye barua ya Desemba 14, 2007 kwa mabaraza yote ya wazee inapaswa kusomwa kwanza.
7 Kuhifadhi Chumba cha Hoteli: Ikiwa unataka Idara ya Mahali pa Kulala ikusaidie kupata hoteli au nyumba ya kulala wageni, tafadhali iandikie mapema. Taja kiasi cha pesa ambacho ungependa kulipia mtu mmoja kila siku. Eleza ikiwa utakula milo yote hotelini, au unataka tu chumba na kiamsha kinywa, au chumba peke yake.
8 Matendo Mazuri: Kukubali amri ya Yehova kuhusu kukusanyika pamoja ili kuabudu kunatusaidia ‘tujifaidi wenyewe.’ Jambo la maana hata zaidi ni kwamba kunatupa fursa ya kutukuza jina la Yehova. (Isa. 48:17) ‘Matendo yetu mazuri huwa wazi’ kwa watu wengi kwenye kusanyiko la wilaya, na wengine wamechochewa kueleza hisia zao. (1 Tim. 5:25) Katika jiji mmoja ambalo makusanyiko ya wilaya yamefanywa kwa miaka mingi, meneja mmoja wa hoteli alisema hivi: “Watu wengi katika jiji hili wanazungumza kuhusu Mashahidi wa Yehova na jinsi wanavyofaidika kwa sababu ya kusanyiko lenu. Tunajua jinsi watu wenu wanavyosafisha majengo ya umma, na tunawaona wakisafisha mahali pa kuegesha magari. Inafurahisha sana kuwa na watu wenu wakati wa majira ya kiangazi. Tunatarajia uhusiano wetu mzuri utadumu muda mrefu hata zaidi.” Baada ya kuelezea ugumu wanaopata wanaposhughulika na vikundi vingine na watumbuizaji, meneja wa hoteli moja alipongeza ushirikiano na subira ambao ndugu zetu walionyesha kipindi chote walichokuwa wamekaa hotelini hapo. Alisema hivi: “Tunatamani wageni wetu wote wangekuwa kama Mashahidi wa Yehova!” Mwenendo wa ndugu zetu ambao umesababisha watu watoe pongezi hizo na nyingine nyingi zinazofanana na hizo ni lazima ziwe zinaufurahisha moyo wa Mungu wetu, Yehova!
9 Yesu alisema kwamba maisha yetu yanategemea jinsi tunavyosikiliza “kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.” (Mt. 4:4) Kwenye makusanyiko yetu ya wilaya kila mwaka, Yehova anatupa ‘chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa,’ kinachotayarishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45) Kazi kubwa huwa imefanywa kutayarisha na kuandaa karamu hiyo ya kiroho. Acheni tuonyeshe uthamini wetu kwa maandalizi hayo yenye upendo ya Yehova kwa kuhudhuria na kukazia uangalifu kila sehemu ya programu hiyo.
[Maswali ya Funzo]
1. (a) Kwa nini himizo la Paulo kwa Wakristo Waebrania ni muhimu hasa leo? (Soma Waebrania 10:24, 25.) (b) Tuna fursa gani mbele yetu ya kutimiza himizo la Paulo?
2. (a) Kwa nini ni muhimu kuhudhuria siku zote tatu za kusanyiko? (b) Ili tuhudhurie tunahitaji kuanza kufanya matayarisho gani?
3. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunawajali wengine?
4. Tunaweza kupata wapi habari kuhusu tarehe na mahali ambapo makusanyiko ya wilaya yatafanywa?
5. Tunapaswa kufanya nini ikiwa tunahitaji kupata habari kuhusu mahali pa kulala kwenye kusanyiko ambalo kutaniko letu halijapangiwa?
6. Kuna vikumbusha gani kuhusu fomu ya Ombi la Mahali pa Kulala kwa Wenye Mahitaji ya Pekee?
7. Tunaweza kuungaje mkono mipango ambayo imefanywa kuhusu mahali pa kulala?
8. (a) Tunaweza kumtukuzaje Yehova tunapohudhuria kusanyiko? (b) Ni maelezo gani yametolewa na wafanyakazi wa hoteli kuhusiana na mwenendo mzuri wa ndugu zetu?
9. Mathayo 4:4 linaonyeshaje umuhimu wa kukazia uangalifu kila sehemu ya programu?
[Sanduku katika ukurasa wa 3]
Saa za Programu:
Ijumaa na Jumamosi
3:20 asubuhi - 10:55 jioni
Jumapili
3:20 asubuhi - 10:00 jioni