Kusanyiko la Wilaya la Mashahidi wa Yehova la Mwaka wa 2009
1. (a) Tutafurahia baraka gani kwa kuhudhuria siku zote tatu za kusanyiko la wilaya? (b) Tunapaswa kufanya mipango gani sasa?
1 Sote tunatazamia kwa hamu kusanyiko la wilaya la mwaka wa 2009 na nafasi za kukusanyika pamoja na wasifaji wenzetu wa Yehova, ambao ‘wanatambua uhitaji wao wa kiroho.’ (Mt. 5:3) Kwa kuwa siku ya Yehova iko karibu sana, tunamsihi kila mmoja ahudhurie siku zote tatu ili afaidike kikamili kutokana na ushirika wa Kikristo wenye kuchangamsha na mahimizo yenye kutia moyo ya kusimama imara katika imani. (Sef. 1:14) Walimu na waajiri wanapaswa kujua kwamba kusanyiko ni sehemu muhimu ya ibada yako. Fanya mipango mapema kwa ujasiri na uombe baraka za Yehova; uwe na hakika kwamba atakusaidia.—Isa. 50:10.
2. Hata ikiwa hatukualikwa kuhudhuria kusanyiko la kimataifa, kwa nini tunaweza kutazamia kwamba makusanyiko yatakuwa kama ya kimataifa?
2 Makusanyiko ya Kimataifa: Kwa kuwa makusanyiko ya kimataifa yatafanywa katika nchi na majiji kadhaa, ni wale tu walioteuliwa wanaopaswa kuhudhuria. Kufuata mpango huo kutazuia msongamano wa watu. (1 Kor. 14:40; Ebr. 13:17) Hata hivyo, makusanyiko mengi ya wilaya yatakuwa kama ya kimataifa kwa kuwa wamishonari wengi, Wanabetheli wanaotumika katika nchi za kigeni, na watumishi wa kimataifa watahudhuria makusanyiko katika nchi zao.
3. Tunaweza kuwaonyeshaje upendo wa Kikristo watu fulani katika kutaniko letu?
3 Kuwasaidia Wengine Kuhudhuria: Je, watu fulani katika kutaniko lenu wanahitaji msaada ili wahudhurie kusanyiko? Unapowasaidia wengine kufanya hivyo, ‘unaendelea kuangalia, si faida za kibinafsi za mambo yako mwenyewe tu, bali pia faida za kibinafsi za wengine.’—Flp. 2:4.
4, 5. Unapaswa kufanya nini ikiwa kwa sababu ya hali utalazimika kuhudhuria kusanyiko ambalo kutaniko lenu halikugawiwa?
4 Kupata Habari: Ili kupunguza idadi ya simu zinazopigwa kwenye ofisi ya tawi kuulizia tarehe na mahali pa makusanyiko, tunakuomba kwanza usome gazeti la Mnara wa Mlinzi la Machi 1, 2009, Huduma Yetu ya Ufalme ya Februari 2009, au umwombe mwandishi wa kutaniko lenu habari unazohitaji.
5 Ikiwa utahudhuria kusanyiko ambalo kutaniko lenu halikugawiwa kuhudhuria, unaweza kuandika barua na kuituma kwa anwani ya ofisi ya mahali pa kulala, iliyo nyuma ya fomu ya Ombi la Mahali pa Kulala kwa Wenye Mahitaji ya Pekee. Waandishi wa makutaniko watatumiwa fomu hizo hivi karibuni. Ili upate jibu la ombi lako, tafadhali tia ndani katika barua yako bahasha yenye stempu na anwani yako.
6. Ni utaratibu gani unaopaswa kufuatwa mhubiri mwenye mahitaji ya pekee anapoomba msaada wa kupata mahali pa kulala?
6 Mahitaji ya Pekee: Mhubiri akiomba msaada wa kupata mahali pa kulala, Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko inapaswa kuamua ikiwa mhubiri huyo anastahili kutuma fomu ya Ombi la Mahali pa Kulala kwa Wenye Mahitaji ya Pekee. Halmashauri hiyo inapaswa kupitia miongozo iliyo katika fomu hiyo kabla mwandishi wa kutaniko hajatuma fomu hiyo kwa Idara ya Mahali pa Kulala.
7. Tunaweza kufanya nini ili kuhifadhi chumba cha hoteli?
7 Kuhifadhi Chumba cha Hoteli: Ikiwa unahitaji msaada kutoka kwenye Idara ya Mahali pa Kulala ili kupata hoteli inayofaa au chumba cha wageni, tafadhali iandikie idara hiyo mapema. Taja kiasi cha pesa ambacho ungependa kulipa kila siku kwa ajili ya mtu mmoja, idadi ya siku ambazo utakaa hotelini, na ikiwa unataka kukaa katika hoteli inayoandaa chumba cha kulala na milo yote, chumba cha kulala na kiamsha-kinywa, au chumba cha kulala peke yake.
8. Tunaweza kuonyeshaje roho ya ushirikiano tunaposhughulika na Idara ya Mahali pa Kulala?
8 Usihifadhi vyumba ambavyo hukusudii kuvitumia wala usibadili mpango wa kulala kwenye chumba cha hoteli dakika ya mwisho na kuhamia hoteli nyingine. Kwa kushirikiana na mpango huo, utamwezesha kila mtu kupata chumba cha hoteli kwa kiwango kinachofaa.—1 Kor. 10:24.
9. Tunapaswa kukazia fikira hasa nini tunapojitayarishia na kuhudhuria kusanyiko la wilaya la 2009?
9 Kazi Zinazomtukuza Mungu: Tunapoonyesha matunda ya roho katika shughuli zetu zote, na kukazia fikira maneno na mwenendo wetu tunaposhughulika na wafanyakazi wa hoteli na wengine katika jiji au mji wa kusanyiko, tunachangia sifa nzuri ya watu wa Yehova na kuepuka kuwakwaza wengine. (1 Kor. 10:31; 2 Kor. 6:3, 4) Na umtukuze Mungu kupitia kuhudhuria kwako na mwenendo wako wakati wa kusanyiko la wilaya la 2009!—1 Pet. 2:12.
[Sanduku katika ukurasa wa 5]
Saa za Programu:
Alhamisi (Makusanyiko ya Kimataifa Pekee)
7:20 alasiri - 10:55 jioni
Ijumaa na Jumamosi
3:20 asubuhi - 10:55 jioni
Jumapili
3:20 asubuhi - 10:00 jioni