Je, Waitikia Upendo wa Kristo?
1 Akifikiria mwendo wa maisha wa Bwana wake, mtume Yohana aliandika hivi: “Yesu, akiisha kuwa amependa walio wake mwenyewe waliokuwa ulimwenguni, aliwapenda hadi mwisho.” (Yn. 13:1) Katika majira haya ya Ukumbusho, mawazo yetu yanafikiria wonyesho mkuu zaidi wa upendo wa Kristo. Twaweza kuitikia upendo huu kwa kudhihirisha imani katika fidia, kwa kushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri, na kama Yesu, kwa kuvumilia “hadi mwisho.”—Mt. 24:13; 28:19, 20; Yn. 3:16.
2 Kuuitikia Upendo wa Kristo: Yesu alikuwa mwenye shughuli nyingi sana katika juma la mwisho la maisha yake ya kidunia. (Mt. 21:23; 23:1; 24:3) Tukiwa waigaji wa Kristo, sisi pia twachochewa na upendo ‘tujitahidi wenyewe kisulubu’ katika utumishi wa Yehova. (Luka 13:24) Je, waweza kutumia kwa manufaa mipango ya utendaji ulioongezwa wa kutoa ushahidi wakati wa Aprili kwa kuongeza wakati utakaotumia katika huduma?
3 Mwaka huu Mlo wa Jioni wa Bwana utakuwa Jumatano jioni, Aprili 19. Ni wangapi watakaokuwapo katika pindi hii ya maana? Hilo latutegemea sana. Je, umefanya orodha ya wale unaopanga kualika—mafunzo yako ya Biblia na watu wengine wenye kupendezwa, watu wa jamaa, watu unaowafahamu kibiashara, na wanashule wenzako? Je, umewasiliana nao na kuwaalika kwa uchangamfu? Je, utawakumbusha siku chache kabla ya Ukumbusho? Je, wanahitaji msaada wako kufika huko? Wazee pia wanaalika yeyote ambaye amekuwa asiyetenda katika huduma. Kwa kuwa Ukumbusho utafanywa jioni ya siku ya katikati ya juma badala ya mwisho-juma hakuufanyi usiwe wa maana kwa wote kuhudhuria.
4 Njoo Ukiwa Umejitayarisha: Ni muhimu tuwe tumejitayarisha na tuwe na hali nzuri ya akili tunapohudhuria Ukumbusho. Paulo alihimiza sana waamini wenzake wakumbuke uzito wa tukio hilo. (1 Kor. 11:20-26) Mwaweza kusoma sura ya 13 hadi 17 ya Gospeli ya Yohana wakati wa funzo lenu la Biblia la familia kisha mpange kila mshiriki wa familia asimulie dhabihu ya Yesu yamaanisha nini kwake. Msisahau usomaji wa Biblia kila siku kwa juma la Ukumbusho vilevile!
5 Upendo wetu kwa Kristo ni wenye kina sana, nao waendelea hata baada ya Aprili 19. Tumeazimia kumwonyesha upendo wetu milele! Mwadhimisho wa Ukumbusho mwaka huu utatusaidia kuimarisha azimio hilo.