Iweni Wenye Bidii kwa Lililo Jema!
1 Tunapokaribia majira ya Ukumbusho ya mwaka wa 2003, tuna sababu nyingi za kuwa “wenye bidii kwa lililo jema.” (1 Pet. 3:13) Sababu kuu zaidi ni fidia ya Yesu Kristo. (Mt. 20:28; Yoh. 3:16) Kuhusiana na jambo hilo mtume Petro aliandika hivi: “Haikuwa kwa vitu vyenye kuharibika, kwa fedha au dhahabu, kwamba mlikombolewa kutoka kwenye namna ya mwenendo usio na matunda. . . . Bali ilikuwa kwa damu yenye bei, kama ile ya mwana-kondoo asiye na waa na asiye na doa, naam, ya Kristo.” (1 Pet. 1:18, 19) Kwa sababu tunathamini sana upendo huo mkubwa tunasukumwa kuwa na shughuli nyingi katika kufanya yaliyo mema tukitambua kwamba Yesu ‘alijitoa mwenyewe kwa ajili yetu ili apate kutukomboa sisi kutoka kwenye kila namna ya uasi-sheria na kujisafishia mwenyewe watu walio wake mwenyewe pekee, wenye bidii kwa kazi zilizo bora.’—Tito 2:14; 2 Kor. 5:14, 15.
2 Tunapofanya yale ambayo yanampendeza Mungu tunafurahia uhusiano wa karibu naye, na anatulinda kwa upendo. Petro aliongeza hivi: “Yeye ambaye angependa uhai na kuona siku zilizo njema, . . . acheni ageuke mbali kutoka lililo baya na kufanya lililo jema; acheni atafute sana amani na kuifuatia. Kwa maana macho ya Yehova yako juu ya waadilifu, na masikio yake yaelekea dua zao.” (1 Pet. 3:10-12) Katika nyakati hizi za hatari, ni jambo zuri sana kujua kwamba Yehova anatulinda na yu tayari kutusaidia, na ‘kutuhifadhi kama mboni ya jicho’ lake.—Kum. 32:10; 2 Nya. 16:9.
3 Licha ya majaribu, Wakristo wa mapema ambao Petro aliwaandikia walikuwa na shauku na bidii nyingi, nao walitangaza habari njema kotekote. (1 Pet. 1:6; 4:12) Watu wa Mungu wanafanya vivyo hivyo leo. Ijapokuwa tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” tunasukumwa kufanya mapenzi ya Yehova kwa bidii kwa sababu tunathamini wema wake. (2 Tim. 3:1; Zab. 145:7) Na tuchunguze baadhi ya mambo mema ambayo tutafanya katika majira haya ya Ukumbusho.
4 Waalike Watu Kwenye Ukumbusho: Njia moja ambayo tunaweza kuonyesha uthamini wetu kwa zawadi bora ya fidia ni kwa kuhudhuria mwadhimisho wa kifo cha Yesu, ambao utafanywa mwaka huu Jumatano Aprili 16, baada ya jua kushuka. (Luka 22:19, 20) Mwaka uliopita watu 15,597,746 walihudhuria Ukumbusho katika makutaniko 94,600 ulimwenguni pote! Hilo lilikuwa ongezeko la watu 220,000 ikilinganishwa na mwaka uliotangulia.
5 Ni wangapi watakaohudhuria mwaka huu? Jambo hilo litategemea jitihada zetu za kuwatia wengine moyo wahudhurie. Anza kwa kuandika orodha ya majina ya wale unaotaka kuwaalika. Kwanza waalike watu wa familia yako. Ikiwa una mwenzi wa ndoa asiyeamini, mwambie kwamba unataka sana ahudhurie pamoja nawe. Mume mmoja asiyeamini alisema kuwa alihudhuria mwaka uliopita kwa sababu alitambua kwamba mke wake angefurahi sana kama angehudhuria. Kisha waalike watu wa ukoo, majirani, wafanyakazi au wanashule wenzako. Na usisahau kuwaalika wanafunzi wako wa Biblia.
6 Baada ya kuandika orodha yako, panga kuwaalika wote kibinafsi. Tumia vikaratasi vya mwaliko wa Ukumbusho. Ili kuwasaidia watu kukumbuka wakati na mahali pa mwadhimisho, chapa au uandike vizuri wakati na mahali pa Ukumbusho chini ya kikaratasi cha mwaliko. Tarehe 16 ya Aprili ikikaribia, wakumbushe wale uliowaalika kwa kuwatembelea au kwa simu. Na tuwasaidie wengi iwezekanavyo wahudhurie tukio hilo takatifu sana.
7 Wasaidie Wale Watakaohudhuria Ukumbusho: Ukumbusho ni tukio lenye kufurahisha sana. Hiyo ni nafasi ya kuwakaribisha watu ambao hawahudhurii mikutano yetu kwa ukawaida. Panga ufike mapema na kubaki baada ya Ukumbusho hali za kwenu zikiruhusu. Ongea na wapya ili upate kuwajua. Wakaribishe kwa uchangamfu.—Rom. 12:13.
8 Je, unaweza kuwasaidia wale wanaohudhuria Ukumbusho kufanya maendeleo ya kiroho kwa kujifunza Biblia nao? Jitahidi kujua majina na makao ya wageni ambao hawatembelewi na Mashahidi kwa sasa ili uendelee kuwasaidia. Wakisaidiwa kwa upendo huenda wengine wao wakafanya maendeleo na kustahili kuwa wahubiri wasiobatizwa kabla ya Ukumbusho wa mwaka ujao. Unapowarudia wale waliohudhuria Ukumbusho, waalike kwenye hotuba ya pekee itakayotolewa Aprili 27.
9 Je, Unaweza Kuwa Painia-Msaidizi Katika Majira Haya ya Ukumbusho? Kila mwaka bidii yetu kwa Yehova hutusukuma kuhubiri zaidi katika miezi ya utendaji wa pekee. Bidii ya wote kutanikoni ya kuhubiri habari njema katika majira ya Ukumbusho inaweza kuleta matokeo mazuri.
10 Kutaniko moja lenye wahubiri 107 na mapainia wa kawaida 9 liliripoti kwamba mwezi wa Aprili mwaka jana ulikuwa “wa kipekee,” kwa kuwa wahubiri 53 walikuwa mapainia-wasaidizi, kutia ndani wazee wote na watumishi wa huduma. Wazee waliwezaje kuwatia moyo wahubiri wawe mapainia-wasaidizi mwezi huo? Walianza mapema kutia moyo wengi iwezekanavyo wajiandikishe. Mikutano ya utumishi wa shambani ilifanywa mara kadhaa kwa siku ili ifae hali za wote kutanikoni.
11 Wazee walimalizia ripoti yao kwa kusema hivi: “Tulifurahi sana na tunashukuru kwa pendeleo la kutumikia na baraka ambazo Yehova amempa kila mmoja wetu.” Mkipanga vizuri, kutaniko lenu pia linaweza kufurahia baraka hizo.
12 Watie Moyo Wote Washiriki Katika Huduma: Upendo wetu kwa Mungu na jirani hutusukuma kununua wakati kila mwezi kuzungumza na wengine kuhusu habari njema. (Mt. 22:37-39) Waangalizi wa Funzo la Kitabu la Kutaniko na wasaidizi wao wanapaswa kujitahidi kuwasaidia wahubiri wote katika kikundi chao kuhubiri kila mwezi. Njia nzuri ya kufanya hivyo ni kupanga mapema kuhubiri pamoja na wahubiri mbalimbali katika kikundi. Badala ya kungoja hadi mwisho wa mwezi, anzeni mapema. Kufanya hivyo kutawapa fursa nyingi zaidi za kuwasaidia wengine.
13 Je, kuna wahubiri wagonjwa katika kikundi chenu cha funzo la kitabu walio na matatizo ya kushiriki katika huduma? Iwapo wengine hawawezi kutoka nyumbani, tunaelewa kwamba hawana fursa nyingi za kutoa ushuhuda. Lakini wakitumia fursa chache wanazopata kuangaza nuru, huenda wakawachochea wale wanaoona matendo yao mazuri wapendezwe na kweli. (Mt. 5:16) Waangalizi wa mafunzo ya kitabu wanapaswa kuhakikisha kwamba wahubiri hao wanajua kuwa wanaruhusiwa kutoa ripoti wakitumia angalau dakika 15 kutoa ushuhuda kwa mwezi. Wahubiri hao waaminifu hutiwa moyo wanapoweza kuripoti wakati wanaotumia katika kutoa ushuhuda, na hilo linawaletea uradhi na furaha. Jambo hilo pia linafanya ripoti ya ulimwenguni pote ya utendaji wa watu wa Mungu iwe sahihi.
14 Vijana Wenye Bidii ya Kufanya Yaliyo Mema! Inafurahisha kama nini kuwaona vijana Wakristo wanaotumia nguvu zao katika utumishi wa Yehova! (Mit. 20:29) Iwapo wewe ni kijana, unawezaje kuonyesha bidii yako kwa Yehova wakati wa miezi hii ya utendaji wa pekee?
15 Iwapo wewe si mhubiri asiyebatizwa, je, unaweza kujitahidi kustahili pendeleo hilo? Unaweza kujiuliza maswali yafuatayo: ‘Je, ninaelewa kweli za msingi za Biblia? Je, ninataka kushiriki katika utumishi wa Ufalme? Je, mwenendo wangu ni mzuri? Je, ninaweza kuwaeleza wengine imani yangu kwa kuongea nao kuhusu habari njema? Je, moyo wangu unanisukuma kufanya hivyo?’ Ikiwa ndivyo, basi ongea na wazazi wako kuhusu tamaa yako ya kuwa mhubiri. Wazazi wako wanaweza kuongea na mmoja wa wazee katika halmashauri ya utumishi.
16 Iwapo tayari wewe ni mhubiri wa habari njema, je, unaweza kutumia wakati mwingi zaidi katika huduma wakati shule zinapofungwa? Vijana wengi waliobatizwa wameweza kuwa mapainia-wasaidizi kwa kupanga ratiba nzuri na wakisaidiwa na wazazi wao na wengine. Jambo hilo lisipowezekana, basi jitahidi kushiriki zaidi katika huduma ya shambani. Jiwekee mradi. Mbali na kuweka mradi wa kutumia muda fulani katika huduma, jiwekee mradi mwingine wa kuongeza ustadi wako katika huduma. Unaweza kujitahidi kusoma andiko kwenye kila mlango, kufanya ziara za kurudia kwa ustadi zaidi, kuanzisha funzo la Biblia, au kupanua huduma kwa kutumia njia nyingine ya kutoa ushahidi. Vipi ukiweka mradi wa kuhudhuria Ukumbusho pamoja na jirani yako, mwanashule mwenzako, au mtu wa ukoo? Tukishiriki kikamili katika utendaji huo tutapata uradhi na bila shaka tutawatia wengine moyo kutanikoni.—1 The. 5:11.
17 Wasaidie Wapya Kufanya Maendeleo: Mafunzo ya Biblia zaidi ya 60,000 yaliongozwa kila mwezi katika mwaka wa utumishi uliopita katika eneo la Afrika Mashariki. Baada ya muda, wengi wa wanafunzi hao watafanya maendeleo na kujiweka wakfu na kubatizwa. Hata hivyo, kabla hawajafikia mradi huo twahitaji kuwasaidia wastahili kuwa wahubiri wa habari njema. Hiyo ni hatua muhimu ya kuwasaidia wapya kuwa wafuasi wa Yesu Kristo. (Mt. 9:9; Luka 6:40) Je, una mwanafunzi yeyote wa Biblia ambaye yuko tayari kuchukua hatua hiyo?
18 Iwapo hujui kama mwanafunzi wako anastahili, omba msaada kutoka kwa mwangalizi wa funzo lako la kitabu au mwangalizi wa utumishi. Labda unaweza kumwalika ashiriki katika funzo lako. Kwa sababu ndugu hao wana ujuzi mwingi wanaweza kukadiria maendeleo ya kiroho ya mwanafunzi. Wanaweza kupendekeza mambo yatakayomsaidia mwanafunzi kuendelea kufanya maendeleo ya kiroho.
19 Mwanafunzi wako anaposema kwamba anataka kuwa mhubiri asiyebatizwa nawe unaona anastahili, ongea na mwangalizi-msimamizi. Atapanga wazee wawili wakutane nawe na mwanafunzi wako ili kuona kama anastahili, wakitumia habari katika kitabu cha Huduma Yetu kwenye ukurasa 98-99. (Ona Mnara wa Mlinzi, Novemba 15, 1988, ukurasa wa 17.) Mwanafunzi akikubaliwa kuwa mhubiri, unapaswa kuanza kumzoeza bila kukawia. Baada ya yeye kutoa ripoti ya utumishi wa shambani, kutaniko litatangaziwa kwamba yeye ni mhubiri asiyebatizwa. Tumaini letu ni kwamba wahubiri wengi wapya, vijana kwa wazee, wataweza kuchukua hatua hiyo muhimu wakati wa miezi hiyo ya utendaji wa pekee.
20 Tukipanga Vizuri Tutatimiza Mengi: Tukipanga mapema tutafanikiwa katika shughuli zetu za kiroho katika majira haya ya Ukumbusho. (Mit. 21:5) Kuna mambo mengi ambayo wazee wanahitaji kushughulikia.
21 Ili kusaidia kutaniko kutimiza mengi iwezekanavyo katika huduma ya shambani, wazee wanapaswa kupanga mikutano ya utumishi wa shambani juma lote. Mwangalizi wa utumishi anapaswa kusimamia mipango hiyo. Je, inawezekana kupanga mikutano ya ziada ifanywe asubuhi na mapema, alasiri, na jioni? Kutaniko linapaswa kutangaziwa mipango hiyo. Inafaa kuweka ratiba ya mikutano hiyo kwenye ubao wa matangazo.
22 Wazee wanapaswa kuhakikisha kwamba mipango ya Ukumbusho imekamilishwa muda mrefu kabla ya Aprili 16. Mipango hiyo inatia ndani kuwasiliana na makutaniko mengine yatakayotumia Jumba la Ufalme, usafi wa Jumba la Ufalme, kuteua wakaribishaji na wale watakaopitisha mkate na divai, na kununua divai na kutayarisha mkate. Kutaniko linapaswa kutangaziwa wakati na mahali ambapo Ukumbusho utafanywa na mabadiliko yoyote ya saa za mikutano juma hilo. Tukishughulikia hayo yote kwa bidii mwadhimisho huo ‘utatukia kwa adabu na kwa mpango.’—1 Kor. 14:40.
23 Vichwa vya familia wanatiwa moyo kutumia wakati wa funzo la familia kuzungumzia jinsi wote wanavyoweza kushiriki zaidi katika utendaji wakati wa majira ya Ukumbusho. Je, wote katika familia yako wanaweza kuwa mapainia-wasaidizi? Au je, familia inaweza kumwunga mkono mtu mmoja au zaidi katika familia awe painia-msaidizi? Jambo hilo lisipowezekana, wekeni mradi hususa kama familia wa kutumia wakati mwingi zaidi katika huduma. Je, kuna mtoto au kijana katika familia ambaye anaweza kutiwa moyo na kusaidiwa kuwa mhubiri asiyebatizwa? Familia yenu inaweza kuwaalika watu wangapi kwenye Ukumbusho mwaka huu? Mkipanga vizuri familia yenu itapata baraka na furaha nyingi.
24 Tumia Ifaavyo Wakati Unaobaki: Mtume Petro alipowaandikia Wakristo katika karne ya kwanza aliwakumbusha kwamba waliishi wakati wa mwisho wa mfumo wa Wayahudi. (1 Pet. 4:7) Leo kuna uthibitisho mwingi unaoonyesha kwamba mwisho wa ulimwengu wa sasa umekaribia. Kila siku maisha yetu yanapaswa kuonyesha kwamba tunasadiki hivyo. Tukiwa watumishi wenye bidii wa Yehova, tunapaswa kutia maanani kazi muhimu ya kuhubiri habari njema.—Tito 2:13, 14.
25 Sasa ndio wakati wa kuwa wenye bidii! Tafakari yale ambayo Yehova amekufanyia wewe, familia yako, na kutaniko. Ijapokuwa hatuwezi kamwe kumlipa Yehova kwa ajili ya vyote ambavyo ametufanyia, tunaweza kumwabudu kwa nafsi yote. (Zab. 116:12-14) Yehova atabariki jitihada zetu za bidii. (Mit. 10:22) Sisi sote na tuwe “wenye bidii kwa lililo jema” wakati huu wa utendaji wa pekee, “ili katika mambo yote Mungu apate kutukuzwa kupitia Yesu Kristo.”—1 Pet. 3:13; 4:11.
[Sanduku katika ukurasa wa 3]
Hudhurio la Ukumbusho Ulimwenguni Pote
1999 14,088,751
2000 14,872,086
2001 15,374,986
2002 15,597,746
[Sanduku katika ukurasa wa 4]
Utamwalika Nani Kwenye Ukumbusho?
□✔ Familia yako na watu wa ukoo
□✔ Majirani na watu unaowajua
□✔ Wafanyakazi na wanafunzi wenzako
□✔ Ziara za kurudia na wanafunzi wa Biblia
[Sanduku katika ukurasa wa 5]
Wasaidie Watakaohudhuria Ukumbusho
□✔ Wakaribishe kwa uchangamfu
□✔ Warudie
□✔ Jitolee kujifunza Biblia pamoja nao
□✔ Waalike kwenye hotuba ya pekee
[Sanduku katika ukurasa wa 5]
Una Miradi Gani Katika Majira Haya ya Ukumbusho?
□✔ Kuhakikisha kwamba mtu mmoja uliyemwalika anahudhuria Ukumbusho
□✔ Kustahili kuwa mhubiri wa habari njema
□✔ Kutumia muda fulani katika huduma
□✔ Kufanya maendeleo katika sehemu fulani ya huduma
□✔ Kutumikia kama painia- msaidizi