“Acheni Nuru Yenu Ing’ae”
1 Ulimwengu unaotuzunguka umo gizani kiadili na kiroho. Nuru ya kweli hufichua “kazi [za giza] zisizozaa matunda” ili vipingamizi hivyo hatari vyenye kukwaza viepukwe. Kwa sababu hiyo, mtume Paulo aliwasihi Wakristo hivi: “Endeleeni kutembea kama watoto wa nuru.”—Efe. 5:8, 11.
2 “Matunda ya nuru” yanatofautiana sana na giza la ulimwengu huu. (Efe. 5:9) Ili tuzae matunda haya twapaswa tuwe vielelezo bora sana katika maisha ya Kikristo, aina ya watu ambao Yesu hukubali. Pia lazima tuonyeshe sifa kama vile kujitoa kwa moyo wote, unyoofu, na uchangamfu kwa ile kweli. Matunda haya yahitaji kuonyeshwa katika maisha yetu ya kila siku na katika huduma yetu.
3 Ng’aa Katika Kila Fursa: Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Acheni nuru yenu ing’ae mbele ya watu.” (Mt. 5:16) Tunapomwiga Yesu, twaangaza nuru ya Yehova kwa kuhubiri juu ya Ufalme wa Mungu na makusudi yake. Twang’aa kama vimulikaji tunapotembelea watu nyumbani na tunapotangaza kweli kazini, shuleni, miongoni mwa jirani zetu, au popote pale tunapopata fursa.—Flp. 2:15.
4 Yesu alisema kwamba wengine wangeichukia nuru. (Yn. 3:20) Kwa hiyo hatuvunjiki moyo watu wengi wanapokataa kuangaziwa “mmuliko wa habari njema yenye utukufu juu ya Kristo.” (2 Kor. 4:4) Yehova husoma mioyo ya binadamu naye hataki wasio waadilifu wawe miongoni mwa watu wake.
5 Tunapofuata njia za Yehova na kufurahia nuru ya kiroho, twaweza kuwaangazia wengine nuru hiyo. Wanapotambua kupitia mwenendo wetu kwamba ‘tunayo nuru ya uhai,’ basi wao pia watachochewa kufanya mabadiliko yanayohitajiwa ili kuwa wabebaji wa nuru.—Yn. 8:12.
6 Kwa kuacha nuru yetu ing’ae, tunamletea Muumba wetu sifa na kusaidia watu wenye mioyo minyoofu kumjua na kupata tumaini la uhai udumuo milele. (1 Pet. 2:12) Kwa kuwa tuna nuru, acheni tuitumie kuwaelekeza wengine watoke katika giza la kiroho na kufanya kazi ambazo ni za nuru.