“Acheni Nuru Yenu Iangaze”
1. Tuna pendeleo la kufanya nini?
1 Kutoka mapambazuko hadi jioni, nuru maridadi inayoonekana humletea Yehova Mungu sifa. Hata hivyo, Yesu aliwaalika wanafunzi wake wawe na aina nyingine ya nuru, yaani, “nuru ya uzima.” (Yoh. 8:12) Kuwa na ujuzi huu wa kiroho ni pendeleo la pekee linalohusisha madaraka mazito. Yesu aliagiza: “Acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu,” na hivyo, kuwanufaisha wengine. (Mt. 5:16) Kwa kuwa ulimwengu huu uko katika giza kubwa la kiroho, kuna uhitaji mkubwa zaidi leo wa kuangaza nuru ya kiroho. Kama Kristo, tunaweza kuachaje nuru yetu iangaze?
2. Yesu alionyeshaje umuhimu wa kuwahubiria wengine kuhusu nuru ya kiroho?
2 Kwa Kuhubiri: Yesu alitumia wakati wake, nguvu zake, na vitu alivyokuwa navyo ili kuwajulisha watu nuru ya kweli katika nyumba zao, maeneo ya umma, juu ya milima—popote ambapo watu wangepatikana. Alitambua thamani yenye kudumu ya kuwaandalia watu nuru ya kweli ya kiroho. (Yoh. 12:46) Ili kuwafikia watu wengi hata zaidi, Yesu aliwatayarisha wanafunzi wake ili wawe “nuru ya ulimwengu.” (Mt. 5:14) Waliacha nuru yao iangaze kwa kuwafanyia majirani wao mema na kwa kuwahubiria kweli za kiroho.
3. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunaithamini kabisa nuru ya kweli?
3 Watu wa Mungu huchukulia kwa uzito daraka lao la ‘kuendelea kutembea kama watoto wa nuru,’ nao huhubiri popote ambapo watu wanaweza kupatikana. (Efe. 5:8) Kusoma Biblia au machapisho mengine ya Kikristo mahali ambapo watu wanatuona wakati wa mapumziko kazini au shuleni, kunaweza kutokeza fursa ya kuanzisha mazungumzo ya Kimaandiko. Kwa kufanya hivyo, dada mmoja kijana alianzisha funzo la Biblia na kuwaachia wanafunzi wenzake vitabu 12!
4. Kwa nini ‘kuacha nuru yetu iangaze’ kunahusisha mwenendo mzuri?
4 Kwa Matendo Mazuri: Kuacha nuru yetu iangaze kunahusisha pia matendo yetu ya kila siku. (Efe. 5:9) Tunapokuwa kazini, shuleni, na sehemu nyingine za umma, watu hutambua mwenendo wetu wa Kikristo na hilo hutokeza fursa za kuwahubiria kweli za Biblia. (1 Pet. 2:12) Kwa mfano, mwenendo mzuri wa mvulana mmoja mwenye umri wa miaka mitano ulimchochea mwalimu wake awasiliane na wazazi wake. Mwalimu huyo alisema, “Sijawahi kamwe kuona mtoto kama huyu, anayeamini kabisa kwamba ni muhimu kutenda mema!” Naam, huduma yetu pamoja na mwenendo wetu mzuri unawavutia watu kwenye “nuru ya uzima” na humletea Mungu wetu sifa.