Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • km 12/95 kur. 3-4
  • Kuacha Nuru Yetu Ing’ae kwa Uendelevu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuacha Nuru Yetu Ing’ae kwa Uendelevu
  • Huduma Yetu ya Ufalme—1995
  • Habari Zinazolingana
  • “Acheni Nuru Yenu Iangaze”
    Huduma Yetu ya Ufalme—2011
  • “Acheni Nuru Yenu Ing’ae”
    Huduma Yetu ya Ufalme—2001
  • “Acheni Nuru Yenu Iangaze” ili Yehova Atukuzwe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2018
  • Fuata Nuru ya Ulimwengu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
Pata Habari Zaidi
Huduma Yetu ya Ufalme—1995
km 12/95 kur. 3-4

Kuacha Nuru Yetu Ing’ae kwa Uendelevu

1 Nuru ni nini? Kamusi yaifafanua kuwa “kitu ambacho hufanya kuona kuwezekane.” Lakini kwa kweli, ijapokuwa tekinolojia yenye maendeleo, mwanadamu bado hajui jibu la swali ambalo Yehova alitokeza kama lilivyorekodiwa kwenye Ayubu 38:24. Je, twaweza kuendelea bila nuru? Bila nuru hatungekuweko. Nuru ni muhimu kwa kuona kimwili, na Biblia hutuambia kwamba katika maana ya kiroho, “Mungu ni nuru.” (1 Yoh. 1:5) Sisi twamtegemea kabisa Yule ‘atupaye nuru.’—Zab. 118:27.

2 Hili ni kweli katika maana ya kimwili lakini hata zaidi sana kwa njia ya kiroho. Dini bandia imepoteza watu wengi sana, ikiwaacha katika giza la kiroho, ‘wakipapasa-papasa kutafuta ukuta kama vipofu.’ (Isa. 59:9, 10) Akisukumwa na upendo na huruma zake zisizoweza kushindwa, Yehova ‘huleta nuru yake na kweli yake.’ (Zab. 43:3) Kwa kweli mamilioni ya watu wenye kuthamini wameitikia, wakitoka ‘gizani wakaingie katika nuru yake ya ajabu.’—1 Pet. 2:9.

3 Yesu Kristo atimiza fungu la maana katika kuleta nuru hii ulimwenguni. Yeye alisema: “Mimi nimekuja ili niwe nuru ya ulimwengu, ili kila mtu aniaminiye mimi asikae gizani.” (Yn. 12:46) Wakati wake wote, nishati, na mali zake zote zilielekezwa katika kufanya nuru ya kweli ijulikane. Yeye alisafiri kotekote katika nchi ya nyumbani kwake, akihubiri na kufundisha katika karibu kila mji na kijiji. Alivumilia mnyanyaso wenye ukatili kutoka kila upande, lakini alibaki imara katika utume wake wa kueneza nuru ya kweli.

4 Yesu alikazia fikira kuteua, kuzoeza, na kupanga wanafunzi, akiwa na mradi fulani akilini. Kwenye Mathayo 5:14-16 twasoma maagizo yake kwao: “Nyinyi ni nuru ya ulimwengu. . . . Nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni.” Kama vile tu Yesu, wao walikuwa wawe “mianga katika ulimwengu,” wakieneza nuru ya kweli kila mahali. (Flp. 2:15) Wao walikubali daraka hilo kwa furaha, wakiliona kuwa kusudi lao kubwa maishani. Wakati mfupi baadaye, Paulo aliweza kusema kwamba habari njema ‘ilihubiriwa katika viumbe vyote vilivyo chini ya mbingu.’ (Kol. 1:23) Kutaniko zima la Kikristo liliunganishwa katika kutimiza kazi hiyo kubwa.

5 Sisi leo twapaswa kuwa wenye shukrani kwamba tumekuwa miongoni mwa wale ambao ‘wameyavua matendo ya giza.’ (Rum. 13:12, 13) Twaweza kuonyesha uthamini wetu kwa kuiga kielelezo kilichowekwa na Yesu na Wakristo waaminifu wa wakati uliopita. Uhitaji wa wengine kusikia kweli ni wenye uharaka zaidi na muhimu zaidi sasa kuliko wakati wowote katika historia ya kibinadamu. Hakuna utendaji mwingine uwezao kulingana na kazi hii kwa uharaka wayo na manufaa zayo nyingi mno.

6 Twaweza Kung’aaje Kama Vimulikaji? Njia ya msingi ya kuacha nuru yetu ing’ae ni kushiriki katika kazi ya kuhubiri Ufalme. Kila kutaniko lina mipango ya kawaida, yenye utaratibu, ya kuhubiri katika eneo lililogawiwa. Fasihi nyingi mno hutolewa kwa unamna mbalimbali na katika lugha nyingi. Elimu nyingi inaandaliwa kupitia mikutano, na usaidizi katika kuzoeza wengine kibinafsi unatolewa na wale wenye uzoefu. Fursa za kushiriki ziko wazi kwa wanaume, wanawake, wazee, na hata watoto. Kila mtu katika kutaniko anaalikwa kushiriki kwa kiwango chochote kile uwezo na hali zake zaruhusu. Shughuli zote za kutaniko zinakazia kuhubiri, pamoja na maandalizi ya kusaidia kila mshiriki ashiriki kwa njia fulani. Ushirikiano wa kawaida, wa karibu na kutaniko ndio njia bora zaidi ya kuhakikisha kwamba nuru yetu yaendelea kung’aa.

7 Twaweza kung’aa katika njia ambazo huenda zisihusishe ushahidi wa maneno. Twaweza kuvutia uangalifu wa wengine kwa mwenendo wetu tu. Hilo ndilo jambo ambalo Petro alikuwa akifikiria aliposihi: “Mwe na mwenendo mzuri kati ya Mataifa, ili, . . . wayatazamapo matendo yenu mazuri, wamtukuze Mungu siku ya kujiliwa.” (1 Pet. 2:12) Wengi hupambanua kazi au shirika fulani kulingana na mwenendo wa wale wanaoshirikiana nalo. Watazamaji wanapoona watu walio safi kiadili, wanyoofu, wenye amani, na wenye kutii sheria, wao huona watu kama hao kuwa tofauti na kuamua kwamba wanaishi kulingana na viwango vilivyo vya juu zaidi kuliko vile vinavyofuatwa na watu walio wengi. Kwa hiyo mume anaacha nuru yake ing’ae anapomheshimu na kumtunza mke wake kwa njia ya upendo; mke vilevile kwa kustahi ukichwa wa mume wake. Watoto wanajitokeza wanapotii wazazi wao na kuepuka ukosefu wa adili katika ngono na matumizi ya dawa za kulevya. Mfanyakazi anayejali sana kazi yake, aliye mnyoofu, na mwenye kuwafikiria wengine anathaminiwa sana. Kwa kuonyesha sifa hizi za Kikristo, tunaacha nuru yetu ing’ae, tukipendekeza njia yetu ya maisha kwa wengine.

8 Kuhubiri ni kuzungumza na wengine juu ya kile ambacho tumejifunza kutoka katika Neno la Mungu. Hilo lafanywa kutoka kwenye jukwaa au milangoni, lakini hakuwekewi mipaka kwa vyovyote kuwe kwa pindi hizo pekee. Utendaji wetu wa kila siku hutufanya tukutane na watu wengi sana. Wewe huongea mara ngapi kwa siku pamoja na jirani zako? Ni mara ngapi mtu hugonga mlangoni pako? Je, wewe hukutana na watu wangapi tofauti-tofauti unaponunua vitu, kupanda basi, au kufanya kazi mahali pako pa kazi? Ikiwa wewe ni kijana shuleni, je, waweza kuhesabu idadi ya watu unaoongea nao kila siku? Fursa za kuongea na wengine ni nyingi sana. Unalohitaji tu kufanya ni kuwa na mawazo machache ya Kimaandiko akilini, kuwa na Biblia na trakti kadhaa, na kuchukua hatua ya kuongea unapopata nafasi.

9 Hata ijapokuwa ushahidi wa vivi hivi ni sahili sana, wengine husita kuujaribu. Huenda ni wasio na uwezo wa kuongea sana, wakisisitiza kwamba ni wenye haya sana au wenye wasiwasi sana kufikia watu wasiowafahamu. Huenda wakahisi woga kuhusu kuvuta fikira upande wao au kupata itikio kali. Wale walio na uzoefu katika ushahidi wa vivi hivi wanaweza kukuambia kwamba mara nyingi hakuna sababu yoyote ya kuwa na wasiwasi. Wengine ni kama sisi tu; wana mahitaji yaleyale, wana mahangaikio yaleyale, nao wanataka kujipatia wenyewe na familia zao vitu vilevile. Wengi wataitikia kwa njia yenye fadhili kwa tabasamu yenye uchangamfu au salamu ya kirafiki. Ili uanze, huenda ukahitaji ‘kujipa ujasiri.’ (1 The. 2:2, NW) Hata hivyo, unapoanza, huenda ukashangazwa na kufurahishwa na matokeo.

10 Twabarikiwa Tunapoacha Nuru Yetu Ing’ae: Hapa kuna baadhi ya vielelezo vya mambo yaliyoonwa yenye kuburudisha yatokanayo na ushahidi wa vivi hivi: Bibi mmoja mwenye umri wa miaka 55 alikuwa akijaribu kuvuka barabara. Wakati ambapo karibu tu gari limgonge, dada alimshika mkono wake na kumvuta kwenye usalama, akisema: “Tafadhali uwe mwangalifu. Tunaishi katika nyakati zenye hatari!” Kisha akasimulia ni kwa nini nyakati ni zenye hatari sana. Bibi yule akauliza, “Je, wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova?” Akiwa amekipata kimojapo vitabu vyetu kutoka kwa dada yake, yule bibi alitaka kukutana na mmoja wa Mashahidi wa Yehova, na hilo kutano lilifanya hilo liwezekane.

11 Dada mmoja alianzisha mazungumzo na mwanamke katika chumba cha kungojea kwenye ofisi ya daktari. Mwanamke huyo alisikiliza kwa uangalifu kisha akasema: “Kwa muda fulani nimekuwa nikikutana na Mashahidi wa Yehova; lakini ikiwa mimi mwenyewe nitapata kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova wakati ujao, itakuwa ni kwa sababu ya kile ulichotoka kuniambia. Kukusikiliza ni kama kuanza kuona nuru mahali penye giza.”

12 Tendo la fadhili laweza kuwa hatua ya kusaidia wengine wajifunze kweli. Walipokuwa wakitembea nyumbani kutoka kwenye utumishi wa shambani, dada wawili waliona mwanamke mzee-mzee aliyeonekana kuwa mgonjwa alipotoka kwenye basi. Walisimama na kumuuliza huyo bibi kama alihitaji msaada. Alishangaa sana kwamba watu wawili asiowafahamu kabisa wangeonyesha kupendezwa naye hivi kwamba alisisitiza kujua ni nini kilichowasukuma kufanya tendo hilo la fadhili. Jambo hilo liliandaa fursa ya kutoa ushahidi. Bibi huyo alitoa anwani yake bila kusita na akawaalika kwa uchangamfu wamtembelee. Funzo likaanzishwa. Upesi bibi huyo akaanza kuhudhuria mikutano na sasa anashiriki kweli pamoja na wengine.

13 Dada mzee-mzee hutumia kwa manufaa ushahidi wa asubuhi mapema ufuoni kwao. Yeye hukutana na wafanyakazi wa nyumbani, watunzaji wa watoto, makarani wa benki, na wengine ambao hutembea asubuhi kwenye kijia kando ya ufuo. Yeye huongoza mafunzo ya Biblia, akiwa amekaa karibu na ufuo. Watu kadhaa wamejifunza kweli kutoka kwake nao sasa ni Mashahidi wa Yehova.

14 Akiwa mahali pake pa kazi, dada mmoja alimsikia mfanyakazi mwenzake akiongea juu ya chama cha kisiasa ambacho aliamini kingetatua matatizo ya ulimwengu. Dada huyo akaongea naye, akisimulia ahadi kuhusu kile ambacho Ufalme wa Mungu utafanya. Mazungumzo haya kazini yaliongoza kwenye funzo la Biblia la kawaida nyumbani, na hatimaye yule bibi na mume wake wakawa Mashahidi.

15 Usisahau Kamwe Kuwa Wewe Ni Shahidi! Yesu alipowafafanua wanafunzi wake kuwa “nuru ya ulimwengu,” alitoa sababu kwamba wanapaswa kuwa wakisaidia wengine wanufaike na mwangaza wa kiroho wa Neno la Mungu. Tukitumia shauri la Yesu, tutaionaje huduma yetu?

16 Wanapotafuta kazi ya kuajiriwa, watu wengine huchagua kazi isiyo ya wakati wote. Wao huwekea mipaka kiasi cha wakati na jitihada watakayotumia katika hiyo kwa sababu wanapendelea kutumia wakati wao mwingi wakifuatia utendaji wanaoona kuwa wenye kuthawabisha zaidi. Je, sisi twaona huduma yetu kwa njia hiyohiyo? Hata kama huenda tukahisi tuna wajibu na hata kuwa tayari kuweka kando wakati kwa ajili ya huduma, je, mapendezi yetu ya msingi yapaswa kuwa kwingineko?

17 Kutambua kwamba hakuna Ukristo usio wa wakati wote, tulifanya wakfu wetu, ‘tukijikana wenyewe’ na tukikubali kumfuata Yesu ‘kwa kuendelea.’ (Mt. 16:24, NW) Tamaa yetu ni kuendelea kuwa wenye ‘nafsi yote,’ tukitumia kwa manufaa kila fursa kuacha nuru yetu ing’ae ili tuwafikie watu popote walipo. (Kol. 3:23, 24) Lazima tukinze mitazamo ya kilimwengu, tudumishe bidii yetu kama vile mwanzoni, na tuhakikishe kwamba nuru yetu yaendelea kung’aa kwa uangavu. Huenda wengine wakawa waliruhusu bidii yao ipoe na nuru yao ififie, hata isiweze kuonekana kutoka mwendo mfupi. Mtu kama huyu huenda akahitaji kusaidiwa kurudisha bidii iliyopotea ya huduma.

18 Wengine huenda wakasita kwa sababu ujumbe wetu haupendwi na wengi. Paulo alisema kwamba ujumbe juu ya Kristo ulikuwa ‘upuzi kwao wanaopotea.’ (1 Kor. 1:18) Hata hivyo, haidhuru kile wengine walichosema, yeye alitangaza kwa bidii hivi: “Siionei haya Injili.” (Rum. 1:16) Mtu anayeona haya hujihisi kuwa wa hali ya chini au asiyestahili. Tungewezaje kuhisi haya tunapoongea juu ya Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote mzima aliye Mkuu Kabisa na maandalizi ya ajabu ambayo amefanya kwa furaha yetu ya milele? Haiwaziki kwamba tungehisi tukiwa wa hali ya chini au kutostahili tunapoongea na wengine kweli hizi. Badala ya hivyo, twapaswa kuhisi tumesukumwa kufanya yote tuwezayo, tukionyesha usadikisho wetu kwamba hatuna “sababu ya kutahayari.”—2 Tim. 2:15, italiki ni zetu.

19 Nuru ya kweli inayong’aa sasa katika nchi zilizo duniani kote hutoa kwa uchangamfu tumaini la uhai udumuo milele katika ulimwengu mpya ulio paradiso. Acheni tuonyeshe kwamba tumezingatia moyoni onyo la upole la kuacha nuru yetu ing’ae kwa uendelevu! Tukifanya hivyo, tutakuwa na sababu ya kushangilia kama vile tu wanafunzi ambao kila siku “hawakuacha kufundisha na kuhubiri habari njema za Yesu kwamba ni Kristo.”—Mdo. 5:42, italiki ni zetu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki