Yehova Hupa Nguvu
1 Wewe wamwonaje mtume Paulo? Tusomapo kitabu cha Matendo, twafahamu jinsi alivyokuwa na bidii katika utumishi wa Yehova. Paulo alitimizaje yote aliyofanya? Alisema: “Kwa mambo yote ninayo nguvu kwa njia ya yeye anipaye nguvu.” (Flp. 4:13) Sisi pia twaweza kunufaika kutokana na nguvu ambayo Yehova hutupa. Jinsi gani? Kwa kutumia kwa manufaa maandalizi sita anayotupa ili tupate nguvu mpya na kuimarishwa kiroho.
2 Neno la Mungu: Kama ilivyo lazima tule chakula ili kudumisha nguvu za kimwili, lazima tujilishe Neno la Mungu ili tuendelee kuwa hai kiroho. (Mt. 4:4) Biblia huandaa nguvu ya kututegemeza. Ili kudumisha bidii na uchangamfu wetu kwa ajili ya kweli, twahitaji kujifunza kibinafsi na kutafakari, kila siku ikiwezekana.—Zab. 1:2, 3.
3 Sala: Ni jambo la maana kumkaribia Yehova hasa katika nyakati zenye uhitaji wa pekee. Kupitia roho yake takatifu, yeye huwapa nguvu wote wanaomwomba katika sala. (Luka 11:13; Efe. 3:16) Maandiko hututia moyo ‘tudumu katika sala.’ (Rom. 12:12) Je, wewe hufanya hivyo?
4 Kutaniko: Pia sisi huimarishwa na kutiwa moyo kutokana na mikutano ya kutaniko na kutokana na ushirika mchangamfu tunaofurahia pamoja na ndugu na dada zetu. (Ebr. 10:24, 25) Tunapotaabika, wanatutia moyo na kutusaidia kwa upendo.—Mit. 17:17; Mhu. 4:10.
5 Utumishi wa Shambani: Kushiriki kwa ukawaida katika huduma hutusaidia twendelee kuzingatia Ufalme na baraka zake. Tunachangamshwa tunaposaidia wengine wajifunze kuhusu Yehova. (Mdo. 20:35) Si wote wanaoweza kuhama kutumikia mahali palipo na uhitaji mkubwa au kushiriki katika utumishi wa wakati wote, lakini tunaweza kuwa na sehemu ya maana katika huduma kwa njia nyingine.—Ebr. 6:10-12.
6 Waangalizi Wakristo: Sisi hunufaika kutokana na kitia-moyo na usaidizi unaotoka kwa wazee. Yehova amewapa kazi ya kuchunga kundi la Mungu lililo katika utunzaji wao. (1 Pet. 5:2) Waangalizi wasafirio hujenga makutaniko wanayotumikia, kama alivyofanya Paulo katika siku yake.—Rom. 1:11, 12.
7 Vielelezo vya Waaminifu: Ni jambo lenye kutia nguvu kuchunguza vielelezo vya wafanyakazi wenzetu waaminifu wa kale na wa kisasa. (Ebr. 12:1) Unapohitaji kutiwa nguvu mpya, kwa nini usisome masimulizi ya maisha yenye kutia moyo katika magazeti yetu, ripoti yenye kujenga katika Yearbook, au baadhi ya masimulizi yenye kusisimua ya historia ya siku ya kisasa ya Mashahidi wa Yehova katika kitabu Wapiga-Mbiu?
8 Ndugu mmoja, ambaye sasa yuko katika umri wake wa miaka ya katikati ya 90, alikubali kweli alipokuwa kijana mchanga. Alipokuwa angali kijana, imani yake ilijaribiwa. Kwanza kabisa, watu fulani ambao walikuwa washiriki watendaji wa kutaniko waliliacha tengenezo la Yehova. Kisha mahubiri ya nyumba hadi nyumba yalikuwa magumu. Ingawa hivyo, sikuzote alimtegemea Yehova. Punde si punde akaanza kufurahia huduma. Na leo je? Ijapokuwa afya mbaya, angali mshiriki wa familia ya Betheli ya Brooklyn, akitumikia katika Baraza Linaloongoza. Hajuti kushikamana na tengenezo la Yehova.
9 Dada mmoja ambaye ni mshiriki wa familia ya Betheli huko Uingereza alibatizwa alipokuwa na umri wa miaka 13. Alianza upainia pamoja na ndugu yake mwaka uliofuata, na mwaka mmoja baada ya hapo, baba yake alifungwa gerezani kwa sababu ya kutopendelea upande wowote wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili. Aliendelea kumtegemea Yehova apate nguvu, na akaendelea kumtumikia Mungu wa kweli. Baada ya muda, aliolewa na ndugu mwaminifu, na pamoja wakaendelea kufanya mapenzi ya Yehova. Baada ya miaka 35 ya ndoa, mume wake alikufa kwa ghafula. Lakini alipata nguvu kutoka kwa Yehova na ameendelea kumtumikia mpaka leo, akitazamia kutumikia milele akiwa mshiriki wa familia ya kidunia ya Yehova.
10 Yehova husaidia na kuwapa nguvu watumishi wake waaminifu. “Anampa aliyechoka nguvu, na yule asiye na nishati yenye msukumo humfanya awe na uwezo tele.” Twaweza kupata nguvu hiyo isiyo na mpaka kwa kutumia kwa manufaa maandalizi sita yaliyotajwa juu. Kumbuka: “Wale wanaomtumaini Yehova watarudiwa na nguvu tena. . . . Watakimbia na wasiwe na uchovu; watatembea na wasichoke.” (Isa. 40:29-31, NW) Paulo alimtegemea sana Yehova ili apate nguvu, nasi lazima tufanye vivyo hivyo.