Kuthamini Vichapo
1 “Hakuna mwisho wo wote wa kutunga vitabu vingi.” (Mhu. 12:12) Vitabu vingi vinavyochapwa havina thamani. Hata hivyo, vichapo ambavyo Sosaiti ya Watchtower huchapisha ni tofauti. Ni vyenye thamani kwa sababu vina chakula cha kiroho chenye kuokoa uhai. Vichapo hivyo husaidia wanaopendezwa wapate kumjua Yehova, navyo huimarisha imani ya wale ambao tayari ni watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu.
2 Twataka kuwapa wengine vichapo vyetu kwa kuwa twajua kwamba vitawafaidi. Hata ingawa vyatolewa bila malipo, kuna gharama zinazotumiwa kuvichapisha na kuvigawanya. Kwa hiyo, hatungetaka kugawanya vichapo bila kutumia busara. Ikiwa hatuna uhakika kwamba mwenye nyumba anapendezwa, kwa kawaida tutatoa nakala mojamoja za Mnara wa Mlinzi na Amkeni! au labda trakti tu. Tunapaswa kumtembelea yeyote ambaye amekubali kichapo, na akionyesha kupendezwa wakati huo, twaweza kumpa kichapo kingine.
3 Wengine husita kuwaambia wenye nyumba kwamba kazi yetu yategemezwa kwa michango ya kujitolea, lakini inafaa sikuzote kuwaambia hivyo. Hilo huwafahamisha wazi wenye nyumba kwamba kazi yetu si ya kibiashara. Huonyesha kwamba lengo letu kuu ni kuhubiri habari njema za Ufalme na kufanya wanafunzi. Hutusaidia kutambua wanaopendezwa kikweli. Mara nyingi watu huwa na pesa za kununua tumbaku na vichapo vya kilimwengu. Ikiwa kwa kweli wanapendezwa na yale unayowaambia, wataona umuhimu wa kutoa mchango ili kutegemeza Ukristo wa kweli. Kwa kueleza jinsi kazi hii inavyotegemezwa, twaonyesha kwamba twathamini vichapo vyetu. Twaonyesha kwamba twatambua gharama za kuvichapisha.
4 Tukiwaeleza vizuri juu ya michango, wenye nyumba wengi watapendezwa kusaidia katika kazi yetu muhimu. Huenda kukawa na nyakati ambazo wahisi haifai kutaja kuhusu michango, lakini kwa kawaida ni vizuri kuitaja katika ziara ya kwanza mwenye nyumba anapopendezwa kusoma vichapo tunavyotoa.