‘Lihubiri Neno la Mungu Kikamili’
1 Unapotoa shukrani kwa moyo wote baada ya kupokea kitu kizuri, je, huonyeshi hivyo kwa mtazamo wako na matendo yako? Bila shaka! Ona jinsi mtume Paulo alivyosema kuhusu wema na fadhili zenye upendo ambazo Yehova anawatendea wanadamu. Alisema hivi: “Shukrani ziwe kwa Mungu kwa ajili ya zawadi yake ya bure isiyoelezeka”! Hiyo ‘zawadi ya bure’ yatia ndani nini? “Fadhili isiyostahiliwa ya Mungu izidiyo” ambayo ametutendea. Tendo lake kuu likiwa ni zawadi ya Mwana wake mwenyewe kuwa fidia ya dhambi zetu.—2 Kor. 9:14, 15; Yn. 3:16.
2 Je, shukrani za Paulo zilikuwa za maneno tu? La, hasha! Alionyesha uthamini mwingi kwa njia nyingi. Alihangaikia sana hali ya kiroho ya Wakristo wenzake na alitaka kufanya yote aliyoweza ili kuwasaidia wanufaike kikamili na fadhili zenye upendo za Mungu. Kuhusu Wakristo hao, Paulo alisema: “Tukiwa na shauku nyororo kwa ajili yenu, tulipendezwa vema kuwapa nyinyi, si habari njema ya Mungu tu, bali pia nafsi zetu wenyewe, kwa sababu mlipata kuwa wapendwa kwetu.” (1 The. 2:8) Zaidi ya kuwasaidia wale ambao tayari walikuwa sehemu ya kutaniko kushikilia wokovu wao, Paulo hakuchoka kuhubiri habari njema. Alisafiri maelfu ya kilometa barani na baharini ili kutafuta wale “waliokuwa na mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele.” (Mdo. 13:48) Shukrani za Paulo kwa yale yote ambayo Yehova alikuwa amemfanyia zilimchochea “kulihubiri neno la Mungu kikamili.”—Kol. 1:25.
3 Je, shukrani zetu kwa yale ambayo Yehova ametufanyia hazituchochei kusaidia wale walio na uhitaji wa kiroho katika kutaniko letu? (Gal. 6:10) Na je, hatuchochewi kushiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri habari njema za Ufalme kotekote katika eneo letu?—Mt. 24:14.
4 Fursa ya Kutoa Shukrani Zetu: Kila mwaka Ukumbusho wa kifo cha Kristo hutupatia fursa ya pekee ya kuwashukuru Yehova na Yesu kwa yale ambayo wametufanyia. Huu si mkutano au tukio la kuchukuliwa vivi hivi tu. Yesu alisema hivi: “Fulizeni kufanya hili katika ukumbuko wangu.” (Luka 22:19) Ukumbusho wa kifo cha Kristo ni pindi ya kutafakari utu wa Yesu. Ni wakati wa kutambua kwamba yeye yuko hai na ni mwenye shughuli leo, na mwenye utukufu na ufalme ambao alipewa kwa sababu ya maisha yake ya uaminifu na ya kujidhabihu. Mwadhimisho huo pia ni fursa ya kuonyesha kwamba tunamtii Kristo akiwa kichwa kwa kuwa yeye anaongoza mambo na utendaji wa kutaniko la Kikristo. (Kol. 1:17-20) Watu wote wa Mungu wanapaswa kuhudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Mwaka huu utafanywa baada ya jua kutua Alhamisi, Machi 28, 2002.
5 Kwa sababu ya juhudi zilizofanywa kabla ya kuadhimisha Ukumbusho mwaka jana, tulikuwa na kilele kikuu kuliko vyote cha wahudhuriaji 75, 597 katika nchi zilizo chini ya ofisi ya tawi ya Kenya. Ni wangapi watahudhuria mwaka huu? Itategemea kama “tunafanya kazi kwa bidii na kujikakamua wenyewe,” tukisaidia wengi iwezekanavyo wahudhurie.—1 Tim. 4:10.
6 Zaidi ya kuhudhuria Mlo wa Jioni wa Bwana, huenda tukaongeza utendaji wetu katika utumishi wa shambani. Bila shaka, makumi ya maelfu ya akina ndugu na dada watafanya upainia-msaidizi kwa mwezi mmoja au zaidi. Kila mwaka tumekuwa na kilele cha mapainia-wasaidizi wakati wa majira ya Ukumbusho, Machi hadi Mei. Je, waweza kupanga mambo yako ili ufurahie kufanya upainia-msaidizi mwaka huu? Itakuwa njia nzuri ya kuonyesha kwamba unathamini kwa dhati zawadi yenye upendo ya dhabihu ya Kristo kutoka kwa Mungu. Bila shaka utapata baraka za Yehova, kama vile mambo yaliyoonwa yafuatayo yanavyoonyesha.
7 Dada mmoja anayefanya kazi ya kimwili wakati wote aliandika kuhusu jambo aliloona akifanya upainia-msaidizi Machi iliyopita: “Huduma Yetu ya Ufalme ya Februari 2001 ilitia moyo kila mtu ambaye hali zake zilimruhusu afanye upainia-msaidizi katika majira ya Ukumbusho. Kwa kuwa Machi ilikuwa na Jumamosi tano, hiyo ilifaana na ratiba yangu. Kwa hiyo nikaamua kujaza fomu ya ombi.” Alipoanza kufanya upainia mwezi huo, alijiwekea mradi wa kujaribu kuanzisha funzo la Biblia la nyumbani. Je, alifaulu? Ndiyo, alifanikiwa kupata funzo alipofikisha saa 52! Alikata kauli gani? “Kuna baraka nyingi tunapojitahidi zaidi.”
8 Familia itanufaikaje ikifanya upainia pamoja? Familia moja ya watu wanne iliyofanya hivyo mwezi wa Aprili mwaka jana, haitasahau mwezi huo kamwe. Mama yao alisema: “Kila siku tulikuwa na furaha, kwa kuwa tulikuwa tumeungana katika huduma! Mazungumzo kuhusu utumishi wetu wa kila siku, yalifanya wakati wa chakula cha jioni ufurahishe sana.” Mwana wao asema hivi: “Nilifurahia kuhubiri na Baba katika utumishi wa shambani katikati ya juma, kwa kuwa kawaida yeye hufanya kazi ya kimwili.” Baba yao aliongeza kusema: “Nikiwa kichwa cha familia, niliridhika kujua kwamba tulikuwa tukifanya kazi ya maana zaidi leo.” Je, familia yenu yaweza kufanya upainia pamoja? Kwa nini msiwe na mazungumzo ya familia na mwone kama nyote mnaweza kufanya upainia-msaidizi wakati wa majira haya ya Ukumbusho?
9 Je, Twaweza Kufanya Machi Kuwa Mwezi Wetu Bora Zaidi? Mapema katika mwaka wa 2000, Huduma Yetu ya Ufalme ilitokeza swali hili: “Je, Twaweza Kufanya Aprili 2000 Kuwa Mwezi Wetu Bora Zaidi?” Itikio lilikuwaje? Kuliwa na vilele vipya mbalimbali. Kwa kuongezea, tulikuwa na vilele vipya katika saa, magazeti yaliyogawanywa, na ziara za kurudia. Je, wakumbuka uchangamfu ambao ulikuwa katika kutaniko lenu kwa sababu ya utendaji mwingi wa kiroho wakati wa mwezi huo wa pekee? Je, twaweza kufanya vivyo hivyo au hata zaidi ya hivyo mwaka huu? Wote wakijitahidi, Machi 2002 waweza kuwa “Mwezi Wetu Bora Zaidi.” Kwa nini mwezi wa Machi?
10 Kuna sababu mbili ambazo zafanya mwezi wa Machi uwe mwezi wa utendaji wa pekee. Kwanza, Ukumbusho utafanywa karibu na mwisho wa mwezi wa Machi, hiyo ikitupa fursa ya kutosha mapema mwezi huo kualika watu wengi iwezekanavyo. Pili, mwaka huu mwezi wa Machi una miisho-juma mitano, hiyo ikifanya iwe rahisi kwa wale wanaofanya kazi ya kimwili au wanaokwenda shuleni kufanya upainia-msaidizi. Kwa nini usiketi sasa na kupanga ratiba itakayofaa, ukitumia kalenda iliyo katika nyongeza hii? Kufanya upainia-msaidizi kwaweza kuwa rahisi kuliko jinsi unavyowazia. Kwa mfano, ukipanga kutumia muda wa saa nane kila mwisho-juma, utahitaji tu kupangia muda wa saa zingine 10 katika mwezi huo ili ufikishe saa 50.
11 Wazee wanaweza kufanya nini ili wasaidie wote kutanikoni “kulihubiri neno la Mungu kikamili”? Watieni moyo akina ndugu mnapozungumza nao na mnapoongoza mikutano. Viongozi wa Funzo la Kitabu la Kutaniko na wasaidizi wao wanaweza kuongea na kila mmoja aliye katika kikundi chao na kumsaidia. Huenda maneno machache ya kitia-moyo au madokezo yanayofaa ndiyo tu yanayohitajiwa. (Mit. 25:11) Wengi wataona kwamba kukiwa na marekebisho fulani katika ratiba yao, wanaweza kufurahia pendeleo la kutumikia wakiwa mapainia-wasaidizi. Katika makutaniko kadhaa, wazee na watumishi wa huduma wengi pamoja na wake zao huweka kielelezo bora kwa kufanya upainia-msaidizi wakati wa Ukumbusho. Hiyo imetia moyo wahubiri wengi sana kujiunga nao. Kwa sababu ya udhaifu wa kimwili au hali nyinginezo, wahubiri wengine hawawezi kufanya upainia, lakini wanaweza kutiwa moyo kutoa shukrani zao kwa kufanya yote wawezayo katika huduma pamoja na kutaniko.
12 Wazee wakifanya mipango mizuri kutakuwa na mafanikio. Mikutano ya utumishi wa shambani yapasa kupangwa wakati unaofaa katika juma. Ikiwezekana, mwangalizi wa utumishi atawapa mapema akina ndugu wanaostahili mgao wa kuongoza mikutano ya utumishi wa shambani. Watahitaji kujitayarisha vizuri ili mikutano hiyo isipite dakika 10 au 15, kutia ndani kupanga watu katika vikundi, kuwapa eneo, na kutoa sala. (Ona Sanduku la Swali katika Huduma Yetu ya Ufalme ya Septemba 2001.) Kutaniko lapasa kuelezwa waziwazi kuhusu ratiba ya mahubiri ya mwezi huo na iwekwe kwenye ubao.
13 Inafaa kuwe na eneo la kutosha. Mwangalizi wa utumishi anapaswa kukutana na ndugu anayeshughulikia maeneo ili afanye mipango ya kuhubiri maeneo ambayo hayahubiriwi kwa ukawaida. Wahubiri wanapaswa kujitahidi kutafuta watu ambao hawapatikani nyumbani, kutoa ushahidi barabarani na duka hadi duka, na kuhubiri jioni. Inapofaa, wahubiri fulani wanaweza kusaidiwa kuhubiri kwa kutumia simu.
14 Wasaidieni Watumikie Tena: Je, kuna wowote katika eneo la kutaniko lenu ambao hawahubiri tena habari njema? Wangali sehemu ya kutaniko na wanahitaji msaada. (Zab. 119:176) Kwa kuwa mwisho wa ulimwengu huu unakaribia na ule mpya uko mbele, twapaswa kujitahidi kusaidia wale wasiotenda. (Rom. 13:11, 12) Katika muda wa miaka mitano iliyopita, zaidi ya watu 1,700 kila mwaka wamekubali msaada na kurudia utendaji. Twaweza kufanya nini ili tusaidie watu wengi warudie upendo wao na uhakika ambao walikuwa nao mwanzoni?—Ebr. 3:12-14.
15 Baraza la wazee lingependa kuzungumzia jinsi linavyoweza kusaidia wale ambao wamekuwa wasiotenda kwa miaka michache iliyopita. (Mt. 18:12-14) Mwandishi apaswa kuchunguza kadi za Rekodi ya Kutaniko ya Mhubiri na aandike wale wote wasiotenda. Wazee wanapaswa kujitahidi sana kufanya ziara za uchungaji ili kuwasaidia wasiotenda. Huenda mzee angependa kutembelea mhubiri asiyetenda ambaye alifahamiana na kushirikiana naye hapo awali, au aombe wahubiri wengine wamsaidie. Labda walijifunza na yule ambaye sasa hatendi na wangefurahia kumsaidia wakati huu ambapo anahitaji msaada. Inatumainiwa kwamba, wengi kati ya wasiotenda watachochewa kuanza kuhubiri tena neno la Mungu. Wakistahili, ingefaa zaidi waanze wakati wa Ukumbusho!—Ona Sanduku la Swali katika Huduma Yetu ya Ufalme ya Novemba 2000 ili upate habari zaidi.
16 Je, Kuna Wengine Wanaostahili Kuhubiri? Yehova anaendelea kubariki watu wake kwa kuleta “vitu vinavyotamaniwa na mataifa yote.” (Hag. 2:7) Kila mwaka maelfu ya watu hustahili kuwa wahubiri wasiobatizwa. Ni nani hao? Watoto wa Mashahidi wa Yehova na mafunzo ya Biblia yanayofanya maendeleo. Twajuaje kama wanastahili kuwa wahubiri wa habari njema?
17 Watoto wa Mashahidi wa Yehova: Watoto wengi wameandamana na wazazi wao katika kazi ya nyumba hadi nyumba kwa miaka mingi, ijapokuwa bado hawajawa wahubiri wasiobatizwa. Huenda Machi ukawa mwezi mzuri wa kuanza kufanya hivyo. Utajuaje kama mtoto wako anastahili? Ukurasa wa 100 wa kitabu Tumefanywa Tengenezo Tutimize Huduma Yetu wasema kwamba ni wakati “mtoto anapokuwa mfano mzuri katika mwenendo wake na anapoweza kueleza binafsi imani yake kwa kuwaambia wengine juu ya habari njema, akiongozwa kutoka moyoni afanye hivyo.” Ikiwa wafikiri kwamba mtoto wako anastahili, ongea na mmoja wa wazee katika Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko.
18 Wanafunzi wa Biblia Wanastahili: Huenda mwanafunzi wa Biblia akataka kuwa mhubiri wa Ufalme baada ya kupata ujuzi na kuhudhuria mikutano kwa muda. Ikiwa unajifunza na mwanafunzi kama huyo, fikiria maswali haya: Je, anafanya maendeleo, kulingana na umri wake na uwezo wake? Je, ameanza kuwaambia wengine kuhusu imani yake? Je, ‘anajivika utu mpya’? (Kol. 3:10) Je, ametimiza matakwa ya kuwa mhubiri asiyebatizwa kama inavyoonyeshwa kwenye ukurasa wa 97-99 katika kitabu Huduma Yetu? Ikiwa ndivyo, wapaswa kujulisha Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko ili mipango ifanywe wazee wawili wakutane nawe pamoja na mwanafunzi huyo. Akistahili, wazee hao wawili watamjulisha kwamba anaweza kuanza kushiriki katika huduma ya hadharani.
19 Vipi Mwezi wa Aprili na Mei? Miezi hiyo pia itakuwa ya pekee kwa ajili ya utendaji mwingi wa huduma ya shambani. Wengi ambao watafanya upainia-msaidizi mwezi wa Machi wanaweza kufanya hivyo tena katika Aprili na/au Mei. Katika Aprili na Mei, tutakuwa tukitoa Mnara wa Mlinzi na Amkeni! katika huduma. Magazeti hayo yamewafaidi kama nini wale wanaoyasoma! Magazeti hayo yametimiza mengi sana katika ongezeko lililopo ulimwenguni pote. Jitihada ya pekee itafanywa Aprili na Mei ili kuachia watu wengi iwezekanavyo magazeti. Panga sasa ili ushiriki kikamili.
20 Kwa kuwa utendaji wa kuhubiri utazidishwa, je, wahitaji kuongeza idadi ya magazeti unayopata kupitia kutaniko? Katika mwaka mzima wa utumishi, kila Jumamosi imetengwa kuwa Siku ya Magazeti ili kutoa Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Hata hivyo, kwa kuwa wengi watakuwa wakifanya upainia-msaidizi, na sote tutakuwa tukitoa magazeti kwa miezi miwili, huenda ukahitaji kuongeza agizo lako la magazeti kupitia kutaniko. Tafadhali mjulishe mtumishi wa magazeti katika kutaniko lenu bila kukawia. Wakati huohuo, mtumishi wa vichapo anapaswa kuhakikisha kwamba kuna trakti Je, Ungependa Kujua Mengi Zaidi Kuhusu Biblia? za kutosha.
21 Wengi wameshukuru kuwepo kwa sehemu ya Huduma Yetu ya Ufalme yenye kichwa “Mambo ya Kusema Kuhusu Magazeti.” Je, umetumia mpango huo kwa kujifunza utoaji huo wa magazeti? Kwa nini usitumie sehemu ya funzo lenu la Biblia la familia kila juma kujizoeza utoaji huo?
22 Tumia Vizuri Majira ya Ukumbusho ya Mwaka Huu: Kama mtume Paulo, na tumwonyeshe Yehova jinsi tunavyomshukuru kwa “zawadi yake ya bure isiyoelezeka” kwa kushiriki kikamili katika utendaji wa kiroho uliopangwa katika majira ya Ukumbusho ya mwaka huu. Utendaji huo utatia ndani (1) kuhudhuria tukio la maana zaidi mwakani, mwadhimisho wa Mlo wa Jioni wa Bwana, Alhamisi, Machi 28, 2002; (2) kusaidia wasiotenda warudie ‘upendo waliokuwa nao hapo kwanza’ (Ufu. 2:4; Rom. 12:11); (3) kusaidia watoto na mafunzo yetu ya Biblia wastahili kuwa wahubiri wasiobatizwa; na (4) kushiriki kikamili iwezekanavyo katika kazi ya kueneza injili, hata kufanya upainia-msaidizi mwezi wa Machi na kuendelea.—2 Tim. 4:5.
23 Twasali kwa bidii kwamba sote tutashiriki kikamili kuhubiri habari njema za Ufalme katika majira haya ya Ukumbusho, tukitoa shukrani zetu nyingi kwa yale yote ambayo Yehova ametufanyia.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
Ratiba Yako ya Utumishi ya Machi 2002
Jumapili Jumatatu Jumanne Jumatano Alhamisi Ijumaa Jumamosi
1 2
Magazeti Siku
3 4 5 6 7 8 9
Magazeti Siku
10 11 12 13 14 15 16
Magazeti Siku
17 18 19 20 21 22 23
Magazeti Siku
24 25 26 27 28 29 30
UKUMBUSHO
31 BAADA YA
JUA KUSHUKA
Je, waweza kupanga kuhubiri muda wa saa 50 ili ufanye upainia-msaidizi mwezi wa Machi?