Saidia Wengine Wawe Rafiki za Mungu
Tulifurahi tulipopokea broshua mpya yenye kichwa, Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu! Gazeti Mnara wa Mlinzi lilisema hivi kuihusu: “Kuna uhitaji mkubwa wa kutoa elimu sahili ya Biblia katika sehemu nyingi ulimwenguni, na broshua hiyo itatumiwa kutimiza uhitaji huo. Itakuwa baraka kubwa kwa watu wenye elimu ya chini au wasioweza kusoma vizuri.” (w01-SW 1/15 uku. 25) Twaweza kuitumiaje ili kusaidia watu hao wawe rafiki za Mungu?—Yak. 2:23.
Tumekuwa tukitumia broshua Furahia Maisha na picha zake nyingi zenye kuvutia kwa wale wasioweza kusoma lakini wanapendezwa na Biblia. Baada ya kumaliza broshua hiyo, ingefaa kusoma broshua Rafiki ya Mungu kisha broshua Anataka. Pia ingefaa kusaidia watu hao wajifunze kusoma na kuandika kwa kutumia kijitabu Jitahidi Mwenyewe Kusoma na Kuandika. Mwishowe, tunaweza kujifunza kitabu Ujuzi na watu hao, wanapojitayarisha kujiweka wakfu na kubatizwa.
Pia waweza kutoa broshua Rafiki ya Mungu unapohubiria watu katika ziara za kwanza na kuitumia kuanzisha funzo la Biblia. Zaidi ya kupatikana katika Kiingereza na Kiswahili, broshua hiyo yapatikana pia katika lugha nyingine za kienyeji kama vile Kiacholi, Kiganda, Kikamba, Kikuyu, na Kirundi.
Wazazi, je, mmesoma broshua Rafiki ya Mungu pamoja na watoto wenu wachanga? Broshua hii itawasaidia wafurahie uhusiano bora pamoja na Yehova. Wafundisheni watoto wenu jinsi ya kujua vile Mungu anavyohisi. Mnapojifunza na watoto wenu na pia watu wengine wenye kupendezwa, waonyesheni jinsi mnavyompenda Yehova na matendo yake. (Zab. 103:2) Hivyo tutakuwa tukiwasaidia kuwa rafiki za Mungu.