“Zawadi Zikiwa Wanadamu” Huchunga Kundi la Mungu kwa Hamu
1 Yehova ametoa msaada wenye upendo kama nini kupitia Mwana wake kwa kutupatia“zawadi zikiwa wanadamu”! (Efe. 4:8, 11, 12) Wana madaraka mbalimbali, kutia ndani kuchunga kundi la Mungu kwa bidii na kwa hamu. (1 Pet. 5:2, 3) Sote twanufaika na msaada huo tunaohitaji sana. Iwe wengine wanakabili magumu, wamejiunga na kutaniko hivi karibuni, wana udhaifu fulani, au wamekengeuka, wanaume hao wanapendezwa sana na hali ya kiroho ya watu wote.—Flp. 2:4; 1 The. 5:12-14.
2 Matukio ya ulimwengu yenye kutaabisha yanapotufanye tuwe na wasiwasi, wachungaji hawa huthibitika kuwa “kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba.” Tukiwa tumechoka au kulemewa na twahitaji kufarijiwa, wao hutuchangamsha “kama mito ya maji mahali pakavu” au “kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu.”—Isa. 32:2.
3 Kuwatia Moyo Wasiotenda: Wazee wanajitahidi sana kuwatia moyo wale wasio wa kawaida au wasiotenda, wakiwasaidia kurudia utendaji wao wa kutaniko kwa ukawaida. Ziara za wachungaji wenye upendo zimesaidia wengi wahudhurie mikutano ya kutaniko kwa ukawaida na kujengwa kiroho hivi kwamba wameanza kushiriki tena katika huduma ya shambani. Jitihada zote hizo za wazee huonyesha upendo wa Yehova na uongozi wa Yesu Kristo. Aliweka kielelezo cha kuonyesha anawajali kondoo wake wowote ambao huenda wakawa wamekengeuka au kupotea.—Mt. 18:12-14; Yn. 10:16, 27-29.
4 Wachungaji hao huwa macho kuona dalili ambazo zaonyesha kwamba huenda mtu akawa anasitasita kiroho. Wowote ambao wanaonyesha dalili za kuvunjika moyo, hawahudhurii mikutano kwa ukawaida, au wamepunguza utumishi wao wa shambani yaelekea wanahitaji kusaidiwa kiroho. Wazee wako tayari kusaidia yeyote anayeonyesha mwelekeo wa kuvalia na kujipamba kilimwengu au ambaye ana mtazamo wa kuchambua kutaniko. Waangalizi wenye kujali na wenye shauku ya kweli wako tayari ‘kuwapatia watu nafsi zao wenyewe’ wakijitahidi kusaidia watu kama hao kuanza kumpenda Yehova tena.—1 The. 2:8.
5 Wakristo fulani waliojiweka wakfu wameacha kushirikiana na kutaniko, na kuwa wasiotenda kiroho kwa sababu wamelemewa na magonjwa, matatizo ya kiuchumi, au misongo ya familia. Bila kuwachambua, wazee wanaweza kuwahakikishia kwa fadhili kwamba Yehova huwajali kondoo wake wote naye atawategemeza katika hali ngumu. (Zab. 55:22; 1 Pet. 5:7) Wachungaji wa kundi walio macho wanaweza kuwasaidia watambue kwamba ‘wakimkaribia Mungu, atawakaribia,’ na kuwapa faraja na pumziko.—Yak. 4:8; Zab. 23:3, 4.
6 Kuwajali Wagonjwa: Wachungaji wenye upendo huwahangaikia pia wale ambao huenda wakapuuzwa. Katika kila kutaniko kuna wagonjwa, walio katika hospitali za kuwatunza wazee au walemavu. Hawawezi kushiriki sana kutangaza ujumbe wa Ufalme kwa sababu ya hali zao, na hiyo yaeleweka. Labda fursa wanayoweza kupata ni kupitia kuongea na wageni, wagonjwa wengine, au wale wanaowatunza. Hata hivyo, chochote kile wanachoweza kufanya chathaminiwa na kuonwa kuwa tegemezo kwa kazi ya kuhubiri. (Mt. 25:15) Hata wakihubiri kwa dakika 15 tu, wanapaswa kuripoti dakika hizo, nao wataendelea kuhesabiwa kuwa wahubiri wa kawaida wa Ufalme.
7 “Zawadi zikiwa wanadamu” wanajua kabisa mahitaji ya kiroho ya ndugu zao wakati huu wa mwaka—majira ya Ukumbusho. Huu ni wakati unaofaa kama nini kwa wazee kujitahidi zaidi kusaidia wote ambao wamekengeuka kufurahia tena shangwe na amani ya akili inayotokana na kushirikiana kwa uchangamfu na kutaniko! Tunafurahi tunapoona watu kama hao ambao “katika imani ni jamaa zetu” wakiwa kwenye mikutano ya kutaniko na katika huduma, wakionyesha tena imani yao katika dhabihu ya fidia.—Gal. 6:10; Luka 15:4-7; Yn. 10:11, 14.