Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • km 3/02 uku. 6
  • Barua Kutoka Kwa Baraza Linaloongoza

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Barua Kutoka Kwa Baraza Linaloongoza
  • Huduma Yetu ya Ufalme—2002
Huduma Yetu ya Ufalme—2002
km 3/02 uku. 6

Barua Kutoka Kwa Baraza Linaloongoza

Tuanzapo karne ya 21, ni furaha yetu kuwaandikia barua mkiwa “ushirika mzima wa ndugu” ulimwenguni, na kuwapongeza kwa bidii yenu. (1 Pet. 2:17) Yapata miaka 2,000 iliyopita, Yesu aliuliza hivi: “Mwana wa binadamu awasilipo, je, kwa kweli ataipata hiyo imani duniani?” (Luka 18:8) Utendaji wenu wa bidii wakati wa mwaka wa utumishi uliopita waonyesha wazi kwamba imani ipo duniani! Baadhi yenu mmedharauliwa na kudhihakiwa kwa sababu ya imani yenu. Katika maeneo mengi, mmevumilia vita, misiba, magonjwa, au njaa. (Luka 21:10, 11) Kwa sababu ya bidii yenu kwa kazi njema, Yesu bado anaweza ‘kuipata imani duniani.’ Kwa kweli kuna shangwe mbinguni kwa sababu hiyo!

Twajua kwamba si rahisi kuvumilia. Hebu fikiria majaribu ya ndugu zetu katika nchi moja ya magharibi ya Asia. Jeuri dhidi ya Mashahidi wa Yehova imekuwa jambo la kawaida katika nchi hiyo. Hivi majuzi, polisi walivuruga kusanyiko lenye amani la watu karibu 700. Kufungwa kwa njia kulizuia wengine 1,300 wasihudhurie kusanyiko. Umati wa watu waliofunika nyuso zao, baadhi yao wakiwa polisi, waliingia kwa kishindo kusanyikoni, wakawapiga wahudhuriaji wengi, na kuwasha moto jengo ambalo lilikuwa litumiwe kwa ajili ya kusanyiko. Katika pindi nyingine, wanadini wenye siasa kali wamewapiga vibaya ndugu zetu kwa rungu zilizojaa misumari.

Mashambulio hayo ni yenye kushtua lakini hayashangazi. Mtume Paulo alipuliziwa kuandika hivi: “Wote wale wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watanyanyaswa pia.” (2 Tim. 3:12) Katika karne ya kwanza, Wakristo walivumilia mnyanyaso wa maneno na wa kimwili, na hata wengine waliuawa. (Mdo. 5:40; 12:2; 16:22-24; 19:9) Ndivyo ilivyokuwa pia katika karne ya 20, na bila shaka itaendelea kuwa hivyo katika karne ya 21. Lakini, Yehova atuambia hivi: “Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa.” (Isa. 54:17) Huo ni uhakikisho mzuri kama nini! Kwa kweli, sisi tu wenye thamani sana kwa Yehova hivi kwamba alisema hivi kupitia nabii wake Zekaria: “Anayewagusa nyinyi anagusa mboni ya jicho langu.” (Zek. 2:8, Biblia Habari Njema) Maadui wa waabudu wa Yehova hawatashinda kamwe. Ibada safi itashinda!

Kwa mfano, katika nchi iliyotajwa awali, Mashahidi wa Yehova wamepata vilele vipya viwili vya wahubiri katika mwaka wa utumishi wa 2001. Naam, ndugu zetu huko wanavumilia kujapokuwa magumu, kama vile wafanyavyo wengine kotekote. Katika mwaka wa utumishi uliopita, watu 5,066 walibatizwa kila juma ulimwenguni pote, huo ukiwa wonyesho wa wakfu wao kwa Yehova. Sasa sisi sote kutia ndani wapya hao tumeazimia ‘kusimama tukiwa kamili na kwa usadikisho imara katika mapenzi yote ya Mungu.’—Kol. 4:12.

Pia, fikiria matukio ya hivi karibuni huko Ugiriki. Ijapokuwa kumekuwa na mnyanyaso mkali kwa miaka mingi kutoka Kanisa Othodoksi la Ugiriki, Mashahidi wa Yehova sasa wanatambuliwa na serikali kuwa “dini inayojulikana.” Hati iliyoonyesha hivyo yaendelea kusema kwamba jengo la Betheli ya Ugiriki ni “mahali patakatifu na palipowekwa wakfu kwa ibada ya Mungu.” Pia tuna furaha kuwaambia kwamba katika mwaka wa utumishi uliopita, mahakama zilifanya maamuzi ya kisheria yanayounga mkono ibada yetu huko Bulgaria, Japani, Kanada, Marekani, Rumania, Ujerumani, na Urusi. Twamshukuru Yehova kama nini kwa kufungua mlango wa utendaji katika nchi hizo!

Tufikiriapo njia ambazo Yehova hutegemeza watu wake katika siku hizi za mwisho, twaona kwamba yeye ndiye Rafiki yetu mkubwa zaidi. Twafurahia urafiki wetu pamoja naye, tukijua kwamba anatupenda, anatufundisha, na kutusahihisha. Naam, imani yetu itaendelea kujaribiwa. Lakini imani thabiti katika Yehova itatutegemeza. Yakobo aliandika hivi: “Fikirieni yote kuwa shangwe, ndugu zangu, mkutanapo na majaribu ya namna mbalimbali, kama mjuavyo kwamba ubora huu uliojaribiwa wa imani yenu hutokeza uvumilivu.” (Yak. 1:2, 3) Zaidi ya hayo, uvumilivu wetu huonyesha upendo wetu kwa Yehova, na hiyo hutuletea shangwe kubwa! Ndugu wapenzi, mwe na hakika kwamba Yehova atategemeza kila mmoja wetu. Tukiendelea kuwa waaminifu, bila shaka atatusaidia mpaka tuingie katika ulimwengu mpya. Yeye anataka tufanikiwe.

Kwa hiyo, twawasihi nyie akina ndugu na dada, vijana kwa wazee, mwendelee kukumbuka baraka za ajabu zilizo mbele. Mtazamo wetu na uwe kama ule wa mtume Paulo, ambaye aliandika hivi: “Nahesabu kwamba mateso ya majira yaliyopo si kitu kwa kulinganisha na utukufu utakaofunuliwa katika sisi.” (Rom. 8:18) Mtegemee Yehova unapokabiliwa na janga la aina yoyote ile. Vumilia, na usikubali kukata tamaa. Hutaghairi kamwe, kamwe. Neno la Mungu latuhakikishia kwamba: “Mwenye haki ataishi kwa imani yake.”—Hab. 2:4.

Ndugu zenu,

Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki