Kuishi Kupatana na Wakfu Wetu
1 Iwe ulibatizwa hivi karibuni au miaka mingi iliyopita, yaelekea unakumbuka hatua hiyo muhimu sana katika maisha yako. Ubatizo wetu si mwisho, bali mwanzo wa maisha ya utumishi wa kujitolea unaoweza kudumu milele. (1 Yoh. 2:17) Kuishi kupatana na wakfu wetu kwamaanisha nini?
2 Kufuata Mfano wa Kristo: Baada ya Yesu kubatizwa, ‘alianza kazi yake,’ ya kutangaza “habari njema ya ufalme wa Mungu.” (Luka 3:23; 4:43) Vivyo hivyo, baada ya kujiweka wakfu kwa Yehova na kuonyesha hivyo kwa ubatizo, tulikuja kuwa wahudumu waliowekwa rasmi wa habari njema. Ijapokuwa huenda tukahitaji kutumia wakati na jitihada nyingi ili kutimiza mahitaji ya lazima maishani, kazi yetu kuu ni huduma ya Kikristo. (Mt. 6:33) Badala ya kung’ang’ana kupata umaarufu au utajiri, wale waliojiweka wakfu kwa Mungu hujitahidi ‘kuitukuza huduma yao,’ kama alivyofanya mtume Paulo. (Rom. 11:13) Je, wewe huthamini pendeleo lako la kumtumikia Yehova na kufanya yote uwezayo katika utumishi?
3 Lazima ‘tumpinge Ibilisi,’ kama Yesu alivyofanya. (Yak. 4:7) Shetani alimjaribu Yesu baada ya kubatizwa, naye huwashambulia watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu leo. (Luka 4:1-13) Kwa kuwa tumezungukwa na ulimwengu wa Shetani, lazima tuwe watu wenye kujizuia, tukiepuka chochote kinachoweza kuchafua akili yetu au kupotosha moyo wetu. (Mit. 4:23; Mt. 5:29, 30) Wakristo wanashauriwa kwamba ‘hawawezi kuwa wakishiriki “meza ya Yehova” na meza ya roho waovu.’ (1 Kor. 10:21) Twahitaji kujiepusha na vitumbuizo visivyo safi, mashirika mabaya, na hatari za Internet. Pia twahitaji kuepuka vitabu vya waasi-imani. Kuwa macho kutambua mbinu hizi na nyinginezo za Shetani, kutatusaidia tuishi kupatana na wakfu wetu.
4 Tumia Maandalizi ya Mungu: Ili kutusaidia tuishi kulingana na wakfu wetu, Yehova ametupatia msaada kupitia Neno lake na kutaniko la Kikristo. Uwe na zoea la kusoma Biblia na kusali kwa Yehova kila siku. (Yos. 1:8; 1 The. 5:17) Furahia mikutano. (Zab. 122:1) Shirikiana na wale ambao wanamhofu Yehova na kutii amri zake.—Zab. 119:63.
5 Kwa msaada wa Mungu, unaweza kuishi kupatana na wakfu wako kwa Yehova na kuwa na shangwe ya kumtumikia milele.—Zab. 22:26, 27; Flp. 4:13.