Kazi Inayotaka Tuwe Wanyenyekevu
1 Neno la Mungu hutushauri tuwe ‘wanyenyekevu katika akili, tusilipe ubaya kwa ubaya bali, kinyume cha hivyo, tutoe baraka.’ (1 Pet. 3:8, 9) Bila shaka shauri hilo linafaa katika kazi ya kuhubiri. Kwa kweli, huduma ya Kikristo inaweza kujaribu unyenyekevu wetu.
2 Unyenyekevu ni sifa inayotusaidia kuvumilia hali ngumu. Tunapohubiri, sisi huwatembelea watu tusiowajua bila kualikwa, tukijua kwamba wengine hawatapendezwa kamwe. Twahitaji unyenyekevu ili tuendelee kuhubiri katika hali hizo. Katika eneo moja gumu sana, akina dada wawili mapainia walikwenda nyumba hadi nyumba kila siku kwa miaka miwili bila kukaribishwa! Hata hivyo, walivumilia, na leo kuna makutaniko mawili katika sehemu hiyo.
3 Kukabiliana na Ujeuri: Unyenyekevu utatusaidia tumwige Yesu watu wanapokuwa wajeuri na wasio na fadhili. (1 Pet. 2:21-23) Kwenye nyumba moja, dada mmoja alitukanwa, kwanza na mke kisha mume wa nyumba hiyo, ambaye alimwamuru aondoke hapo. Dada huyo alitabasamu tu na kusema kuwa alitumaini kuongea nao wakati mwingine. Jambo hilo liliwavutia wenzi hao wa ndoa hivi kwamba walimsikiliza Shahidi ambaye aliwatembelea wakati mwingine na walikubali kuhudhuria mkutano kwenye Jumba la Ufalme. Dada ambaye alikuwa ametukanwa alikuwepo na akaenda kuwasalimu kisha akawahubiria zaidi. Sisi pia twaweza kupunguza ukali wa wale wasiotaka kutusikiliza kwa kuwa wenye “tabia-pole na staha yenye kina kirefu.”—1 Pet. 3:15; Mit. 25:15.
4 Epuka Kiburi: Hatupaswi kuwatukana au kuwadharau watu eti kwa sababu tuna ujuzi wa Biblia. (Yoh. 7:49) Badala yake, Neno la Mungu hutushauri ‘kutosema kwa ubaya juu ya yeyote.’ (Tito 3:2) Tunapokuwa wapole, kama alivyokuwa Yesu, tunawaburudisha wengine. (Mt. 11:28, 29) Kuwahubiria wengine kwa unyenyekevu huwafanya wavutiwe zaidi na ujumbe wetu.
5 Naam, unyenyekevu hutusaidia kuvumilia katika eneo gumu. Waweza kuwafanya watu wasiotaka kusikiliza wapunguze ukali wao, na kuwavutia wengine kusikiliza ujumbe wa Ufalme. Zaidi ya yote, unyenyekevu humfurahisha Yehova, ambaye “huwapa wanyenyekevu fadhili isiyostahiliwa.”—1 Pet. 5:5.