Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • km 9/04 uku. 3
  • Sanduku la Swali

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sanduku la Swali
  • Huduma Yetu ya Ufalme—2004
Huduma Yetu ya Ufalme—2004
km 9/04 uku. 3

Sanduku la Swali

Je, inafaa kwa Wakristo kunywa kwa kuwatakia wengine heri, afya njema, au kuwapongeza?

Katika nchi fulani, marafiki wanapoagana, huinua gilasi zenye kileo kisha huzigonganisha na kusema ‘afya njema’ au maneno mengine kama hayo. Kwenye karamu za arusi mara nyingi watu hufanya vivyo hivyo ili kuwatakia maharusi afya njema na furaha. Kwa hiyo, inaeleweka ni kwa nini wengine wameuliza ikiwa inafaa Kimaandiko kwa Wakristo kushiriki katika mambo hayo.

Bila shaka hakuna ubaya wowote kwa Mkristo kumtakia rafiki yake furaha na afya njema. Wala si kosa kufanya hivyo wakiwa kikundi. Wanaume wazee kiroho wa karne ya kwanza walimalizia barua walizoandikia makutaniko ya Kikristo kwa kusema, “Afya njema kwenu!”—Mdo. 15:29.

Lakini je, hilo tu ndilo linalohusishwa katika desturi za kugonganisha gilasi? Kwa nini wale wanaoshiriki huinua gilasi au vikombe vyao na kuvigonganisha? Je, wanaiga mapokeo fulani? Ona jinsi The Encyclopædia Britannica, Chapa ya 11, Buku la 13, ukurasa wa 121, inavyosema:

“Ile desturi ya kunywa kwa kumtakia mtu aliye hai afya njema yaelekea sana ilitokana na zoea la kale la kidini la kunywa kwa heshima ya miungu na wafu. Walipokuwa wakila, Wagiriki na Waroma walikuwa wakimwaga vinywaji kwa ajili ya miungu yao, na kwenye karamu za kisherehe walikunywa kwa heshima ya miungu hiyo na wafu.” Kisha, baada ya kuonyesha jinsi desturi hizo za kipagani zilivyoendelezwa na Waskandinavia na Wateutoni, kitabu hicho chasema hivi: “Lazima kule kunywa kwa kuwatakia watu walio hai afya njema kunahusiana sana na desturi hizo za kutoa dhabihu za vinywaji.”

Watu wengi wanapojiunga na wengine katika desturi hizo, labda hawadhani kwamba wanaiga desturi za kuinua kinywaji au kutolea miungu ya kipagani dhabihu ya kinywaji, lakini huenda hivyo ndivyo wanavyofanya hasa. Bila shaka, Mkristo mwaminifu hawezi kushiriki kutoa dhabihu za kipagani, kwa kuwa anatambua kwamba ‘hawezi kuwa akinywa kikombe cha Yehova na kikombe cha roho waovu.’ (1 Kor. 10:21) Pia, Mkristo mkomavu ataepuka hata kuiga desturi fulani za dini ya uwongo. Kujiendesha hivyo kwa ukomavu humpendeza Yehova. Kumbuka kwamba, Mungu aliwaonya Waisraeli wasiige mazoea ya kidini ya mataifa ya kipagani yaliyowazunguka.—Law. 19:27; 21:5.

Ikiwa Mkristo anamtakia mwingine baraka za Mungu, basi njia inayofaa ya kufanya hivyo ni kumwomba Mungu kutoka moyoni, wala si kwa kufuata desturi zinazotokana na ibada ya kipagani ambayo Yehova anachukia.—Flp. 1:9; 2 Kor. 1:11.

Kuna desturi na mazoea mengi duniani pote. Ikiwa Mkristo mkomavu anajua kwamba desturi fulani imetokana moja kwa moja na dini ya uwongo, bila shaka ataiepuka. Hata hivyo, baadhi ya desturi si mbaya. Huenda baadhi yake zimetokana na tamaduni za kuonyesha heshima wala hazikutokana na dini ya uwongo, kama vile kumsalimu mtu kwa mkono au kuinama. (Mwa. 23:7) Kila mmoja anaweza kufikiria mambo anayojua kuhusu desturi fulani na nia yake mwenyewe kuhusiana nayo. Kwa nini anafanya hivyo? Pia anaweza kujiuliza, ‘Je, kufanya hivyo kutawakwaza wengine, au watu watahusianisha matendo yangu na dini ya uwongo?’ (1 Kor. 10:32, 33) Hakuna mtu anayeweza kuwa dhamiri ya Mkristo mwingine; kwa hiyo kila mmoja anaweza kufikiria jambo hilo na kufanya uamuzi ili awe na dhamiri safi.—Mdo. 23:1; 2 Kor. 1:12.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki