Msaada Wako Unahitajiwa
1 “Asanteni sana kwa yote mnayofanya kwa niaba yetu. Kazi yenu hutunufaisha sana.” Maneno hayo yanaonyesha wazi shukrani zetu kwa wazee na watumishi wa huduma. Kwa kuwa tengenezo la Mungu linaendelea kupanuka, wanaume waliokomaa wanahitajiwa ili kutumikia katika makutaniko 100,000 hivi duniani. Ikiwa wewe ni ndugu aliyebatizwa, msaada wako unahitajiwa.
2 ‘Kujitahidi’ Kufikia Mapendeleo Zaidi: Unawezaje kujitahidi ufikie mapendeleo zaidi ya utumishi? (1 Tim. 3:1) Unaweza kufanya hivyo hasa kwa kujiendesha vizuri maishani mwako. (1 Tim. 4:12; Tito 2:6-8; 1 Pet. 5:3) Shiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri, na kuwasaidia wengine wafanye hivyo. (2 Tim. 4:5) Pendezwa kikweli na hali ya waamini wenzako. (Rom. 12:13) Jifunze Neno la Mungu kwa bidii, na usitawishe ‘ufundi wa kufundisha.’ (Tito 1:9; 1 Tim. 4:13) Shughulikia kwa bidii na kwa makini migawo unayopewa na wazee. (1 Tim. 3:10) Ikiwa wewe ni kichwa cha familia, ‘simamia nyumba yako mwenyewe kwa njia nzuri.’—1 Tim. 3:4, 5, 12.
3 Ili kuwekwa kuwa mtumishi wa huduma au mzee, unahitaji kuwa mwenye bidii na mwenye roho ya kujitolea. (1 Tim. 5:17) Kwa hiyo, unapojitahidi kufikia mapendeleo hayo, zingatia kuwatumikia wengine kwa unyenyekevu. (Mt. 20:25-28; Yoh. 13:3-5, 12-17) Tafakari juu ya mwelekeo wa Timotheo, na ujitahidi kuuiga. (Flp. 2:20-22) Kama yeye, acha mwenendo wako mzuri ukupendekeze. (Mdo. 16:1, 2) Unapositawisha sifa za kiroho zinazohitajiwa ili kushughulikia madaraka mbalimbali, na pia kufuata ushauri wowote unaopewa ili kuboresha sifa hizo, ‘maendeleo yako yatakuwa wazi kwa watu wote.’—1 Tim. 4:15.
4 Wazazi, Zoezeni Watoto Kusaidia: Watoto wanaweza kujifunza kusaidia wakiwa na umri mdogo. Wazoezeni kusikiliza kwenye mikutano, kuhubiri, na kuwa na mwenendo mzuri wanapokuwa kwenye Jumba la Ufalme na shuleni. Wazoezeni kuwatumikia wengine, kwa kusaidia kusafisha Jumba la Ufalme, kuwasaidia waliozeeka, na kadhalika. Acheni wapate furaha inayotokana na kutoa. (Mdo. 20:35) Mazoezi hayo yanaweza kuwasaidia wawe mapainia, watumishi wa huduma, na wazee wakati ujao.