Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 2/15 kur. 75-79
  • Je! Wewe Unastahili Daraka la Kundi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Wewe Unastahili Daraka la Kundi?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • SIFA ZA MAANDIKO ZINAZOPASWA ZITIMIZWE
  • Je! Wewe Wastahili Kutumikia?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Akina Ndugu—Je, Mnajitahidi Kustahili Kutumikia Mkiwa Wazee wa Kutaniko?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Watumishi wa Huduma Hufanya Utumishi Muhimu
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
  • Watumishi wa Huduma Ni Baraka kwa Watu wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 2/15 kur. 75-79

Je! Wewe Unastahili Daraka la Kundi?

WEWE waonaje juu ya daraka? Wanaume wengi katika ulimwengu leo wanaliepuka kwa sababu linaleta kazi na wajibu. Wengine kwa kutaka makuu wanatafuta daraka, wakitumaini kujipatia ukubwa kwa njia hiyo, uwezo na kuwatawala wengine na kujipa wenyewe mapendeleo ya pekee.

Hakuna nafasi ya maoni haya katika kundi la Kikristo. (Mt. 20:25-27; 1 Pet. 5:2, 3) Hata hivyo wanahitajiwa wanaume walio na nia ya kuchukua daraka. Inawapasa hawa wawe na maoni tofauti sana juu ya daraka kuliko maoni ya watu wengi wa ulimwengu. Imewapasa ‘walifikie’ daraka, ndiyo, lakini waongozwe na tamaa ya kuwatumikia wengine​—zaidi Mungu kisha jirani zao, hasa wale waliomo katika kundi. Kwa kufaa wanatafuta wamletee Mungu heshima na kulifanya jina lake lisifike na kuheshimiwa​—si jina lao wenyewe.​—1 Tim. 3:1, NW; Gal. 6:10; Mit. 8:13.

Katika makundi ya kwanza ya Kikristo ya karne ya kwanza, wanaume waliwekwa katika vyeo vyenye madaraka ama kama “wazee” (Kigiriki, pre·sbyʹte·roi) ama kama “watumishi wa huduma” (di·aʹko·noi). (Tito 1:5; Flp. 1:1, NW) Wazee walitakiwa waliangalie kundi katika njia ya kiroho, watumikie kama ‘wachungaji’ wa kundi la Mungu. (Matendo 20:28) Watumishi wa huduma waliwasaidia, wakiangalia “kazi ya lazima” ambayo haikutia sana uangalizi wa kiroho.​—Matendo 6:1-6, NW.

Bila kujali kama wanatumikia kama mzee au mtumishi wa huduma, imewapasa wanaume hawa wawe kama Mwana wa Mungu aliyelikubali daraka zito kuliko madaraka yote, hata hivyo akaja ‘si kutumikiwa, bali kutumikia.’ (Marko 10:45) Maoni yao yanayofaa yanaweza kulinganishwa na mtu ambaye, anapokutana na fulani anayejaribu kuona mahali fulani, anasema, ‘Acha nikuonyeshe utakavyofika huko.’ Au kama mtu ambaye, anapomwona mwingine akichukua mizigo mizito, anasema, ‘Acha nikusaidie mzigo wako. Je! wewe unayo roho hiyo?

SIFA ZA MAANDIKO ZINAZOPASWA ZITIMIZWE

Walakini, tamaa ya kutumikia siyo inayotakiwa peke yake. Vile vile Neno la Mungu linaweka sifa fulani ambazo ni lazima zitimizwe na wale wanaotumikia kama wazee au watumishi wa huduma. Zifikirie hizi sasa, na unapofanya hivyo, jiulize mwenyewe kama ungestahili daraka hilo la kundi. Na uzifikirie sifa hizi kulingana na ambavyo zilipangwa​—kama zilivyoandikwa kwanza kwa ajili ya Wakristo katika karne ya kwanza ya Wakati wetu wa Kawaida. Hii itasaidia kuepuka maelekeo yo yote ya kuzitazama kwa maoni ya kanuni za kilimwengu, kutia na zile zilizomo katika ulimwengu wa leo wa biashara.

Matakwa fulani ya msingi yanawapasa wazee na watumishi wa huduma vile vile. Kati ya haya ni ya kwamba wanaume hawa wawe:

Bila shtaka. Imewapasa wawe ‘wasiolaumika,’ yaani, wasio na shtaka lo lote la kweli juu ya kosa. (1 Tim. 3:2, 8, 10; Tito 1:6, 7) Kwa kweli, hii haitaki ukamilifu kabisa kwa upande wao. Ikiwa ingetaka, hakuna mwanadamu aliye mzao wa mkosaji Adamu ambaye angeweza kustahili. (Yak. 3:2; 1 Yohana 1:8) Lakini kusiwe shtaka lo lote. Na ikiwa lingekuwako shtaka lo lote, bila shaka lingepaswa lipatane na kanuni za Maandiko za mema na mabaya, na si kanuni za vivi hivi za kilimwengu, ambazo mara nyingi sana ni zenye kupotoka. (1 Tim. 6:14; Kol. 1:22) Ikiwa zamani kulifanyika kosa fulani zito, yampasa mtu awe amekwisha kusahaulisha kwa mema suto lo lote lililotokea na akajifanyia mwenyewe jina zuri kwa mwenendo wake mwema. Kwa njia hiyo kuwekwa hakutaleta suto juu ya kundi machoni pa Mungu au ulimwengu.

Mume wa mke mmoja. Akiwa ni mwanamume aliyeoa, yampasa awe na mke mmoja tu aliye hai, kwa hiyo si mume mwenye wake zaidi ya mmoja kama walivyokuwa wanaume wengi wasio Wakristo katika karne ya kwanza.​—1 Tim. 3:2, 12; Tito 1:6.

Si mpiga kelele ya ulevi. Haimpasi awe mtu ambaye ni mnywaji mno wa pombe, hata anapotewa na akili. Hasa, kama inavyoonyeshwa na matakwa ya watumishi wa huduma, hata asingekuwa “mtu wa kuzoelea ulevi,” kwa hiyo si mtu mwenye sifa ya kuwa “mnywaji sana” (The Jerusalem Bible).​—1 Tim. 3:3, 8; Tito 1:7; 1 Pet. 4:3.

Si mpenda fedha, si mwenye pupa ya mapato ya udanganyifu. Kwa vile watu wenye pupa kulingana na Maandiko wanapangwa pamoja na waasherati, waabudu sanamu na walevi, mtu anayependa mno mambo ya kimwili bila shaka asingestahili daraka katika kundi. (1 Kor. 5:11; 1 Tim. 6:9, 10; Ebr. 13:5) Wale wanaostahili wanaepuka “fedha ya aibu.” (1 Tim. 3:3, 8; Tito 1:7; 1 Pet. 5:2) Usemi huu “ya aibu” hautumiwi kwa habari ya mazoea kama kupunja na kudanganya, njia zinazotumiwa na ulimwengu mbovu tu. Ijapokuwa huenda mapato yakawa na maana ya mapato ya fedha au “faida” za kimwili, kama vile katika mambo ya kibiashara (Yak. 4:13), neno hili lina maana zaidi ya hilo. Linamaanisha faida au mapato ya namna yo yote. (Linganisha Wafilipi 1:21; 3:4-8.) Hivyo, ikiwa mtu ye yote angekitumia cheo chenye madaraka katika kundi la Mungu ama kwa kujipendelea mwenyewe kuliko wengine kwa kujipatia faida za kimwili ama ili awapunje wengine kwa uwezo, sifa au ukuu wake, haya, vile vile, yangekuwa mapato ya aibu. Yeye asingekuwa anatenda kwa unyofu kwa Mwenyewe wa kimbinguni wa kundi aliyemgawia kutumikia bila choyo, kwa unyenyekevu.​—Linganisha 1 Petro 5:2, 3; Matendo 20:33-35; Luka 16:14.

Mwenye kuisimamia nyumba yake vema, ajuaye kutiisha watoto wake. Wala watumishi wa huduma wala wazee hawapaswi wawe vivulana (vitoto) tu bali imewapasa wawe wanaume wazima kuweza kuwa na watoto. Akiwa mtu aliyeoa, imempasa mwanamume ajipatie heshima kama mume na baba mwema, anayesimamia kulingana na kanuni za Biblia. (1 Tim. 3:4, 5, 12; Tito 1:6) Je! hii inataka kwamba kila mshiriki wa jamaa ataitikia kabisa kanuni za kimungu?

Bila shaka, angejitahidi kuelekea mradi huo, lakini​—ingawa jitihada zake nzuri​—huenda hii isitokee hivyo. Hali fulani zinapita uwezo wa kibinadamu. Huenda mke wa mtu asiwe Mkristo anayeamini; huenda hata apinge au kumtesa mume wake kwa sababu ya imani yake. (Mt. 10:36; Luka 12:52) Au, kutokana na watoto wake huenda akawako mmoja anayefanya ufisadi, au ambaye hata anakuwa mbaya kati ya wengine. Walakini, imetupasa tufahamu ya kwamba hata wengine kati ya wana wa kiroho wa Mungu mwenyewe waliasi, kama walivyofanya watoto wake wawili wa kwanza wa kibinadamu. Hata hivyo Mungu hakuweza kulaumiwa hata kidogo kuwa mwenye kosa.

Kwa hiyo, ikiwa mshiriki wa jamaa wa mume au baba wa Kikristo anafanya kosa, swali kubwa ni: Mwanamume wa nyumba ana daraka la tendo hili kwa kadiri gani? Je! yeye alikuwa hatimizi wajibu wake? Ikiwa ndivyo, asingeheshimiwa na kundi au wale walio nje. Kwa upande mwingine, ikiwa yeye alikuwa amefanya yote ambayo angeweza kutazamiwa kufanya, hasa, akipata itikio jema kwa washiriki wengine wa jamaa, kushindwa kwa mshiriki mmoja kuitikia uongozi wake mwema kusingemwondolea sifa.

Si mtu aliyegeuka hivi karibuni. Ili astahili kimojawapo cha vyeo, cheo cha mzee au mtumishi wa huduma, ingalimpasa ‘ajaribiwe juu ya kufaa kwanza,’ aonyeshe kutumainika na uaminifu wake. (1 Tim. 3:6, 10, NW) Hii inachukua wakati. Na, kama ilivyo desturi, ungetakiwa wakati zaidi kwa mzee kuliko kwa mtumishi wa huduma, kama ambavyo usemi wenyewe “mzee” ungeonyesha. Walakini, watu wanatofautiana na kadiri yao ya maendeleo ya kiroho inatofautiana. Kwa hiyo hakuna muda uliowekwa, lakini yawapasa wale wanaompendekeza huyo watumie akili nzuri na wasifanye haraka kumtanguliza mpya, “asije labda akajitutumua kwa kiburi” kama Ibilisi. Mwacheni kwanza asitawishe “nia” ya Kristo​—ile ya unyenyekevu.​—Flp. 2:3-8.

Matakwa fulani mengine yamepangwa hasa kwa ajili ya watumishi wa huduma. Hata hivyo haya vile vile yamepaswa yatimizwe na wale wanaostahili vyeo vya wazee. Kati ya matakwa haya ni kwamba mwanamume awe:

Mzito. Tafsiri nyingine za 1 Timotheo 3:8 zinatumia usemi kama “wenye kuheshimika,” “wanaume wenye heshima,” “wastahivu,” “wanaume wenye kanuni bora,” na hizi vile vile ni maana zenye kukubalika za neno la Kigiriki lililotumiwa na mtume. Hivyo, ijapokuwa inafaa kucheka pindi kwa pindi, hakuna mmoja wa wanaume hawa ambaye angekuwa mpuzi kila mara; wala wasingeelekea kuliona daraka kama mchezo.

Si wenye kauli mbili. Bali, wenye kusema kweli, wanaume “ambao maneno yao yanaweza kutumainiwa,” si wenye unafiki, wenye porojo au wenye hila.​—1 Tim. 3:8, New American Bible; Jerusalem Bible; An American Translation.

Katika dhamiri safi. Dhamiri yake imepaswa ishuhudie mbele za Mungu kwamba yeye si mtu mwenye kuzoea mambo ya kichini-chini, yasiyo safi au ya unajisi, ijapokuwa mazoea haya yasijulikane waziwazi. (1 Tim. 3:9; Rum. 9:1; 2 Kor. 1:12; 4:2; 7:1) Isipokuwa yeye mwenyewe anashikamana na kuzitegemeza kanuni za haki, bila shaka asingeweza kustahili kulitumikia kundi la Mungu katika njia ya uaminifu.​—Mt. 23:3.

Zaidi ya matakwa haya, ambayo ni ya msingi kwa wazee na watumishi wa huduma, kuna mengine yanayowahusu wazee peke yao. Kazi yao waliyogawiwa kama wachungaji na waalimu inaonyeshwa na matakwa haya yanayokazia uwezo wa kutoa uongozi na agizo la upole, lenye msaada lakini lililo thabiti kwa “kondoo” wa Mungu. Yanatia kuwa:

Mwenye kiasi; mwenye kujiweza. Mtu anayestahili kama mzee imempasa azizuie nguvu zake za moyoni na mwilini ili asifanye kwa upumbavu kupita kiasi, wala kutenda katika njia isiyo ya kawaida na isiyosawazika. Kwa hiyo, yeye anaweza kujiendesha mwenyewe katika njia ya busara.​—1 Tim. 3:2; 2 Tim. 4:5; Tito 1:8, NW.

Timamu katika akili. Imempasa mzee awe mtu wa akili; usemi na matendo yake yakiwa yenye akili na yenye kusudi. Busara na maoni yake vingeongezwa kwa mafundisho yenye afya ya Neno la Mungu. 1 Tim. 3:2, NW; Rum. 12:3; linganisha Marko 5:15; Matendo 26:25; 2 Wakorintho 5:13.

Mtu wa utaratibu. Neno la Kigiriki linalotumiwa hapa (1 Timotheo 3:2) ni neno lile lile lililotafsiriwa “yaliyotengenezwa vizuri” katika 1 Timotheo 2:9 (New World Translation). Basi imempasa mzee awe na maisha yenye utaratibu na yenye ustahifu, akiwa mtu mwenye ‘adabu nzuri,’ si ‘asiye na adabu,’ kama tafsiri nyingine za usemi wa Kigiriki zinavyoonyesha. (Linganisha 1 Wakorintho 14:33, 40; walakini, maneno ya hapo ya Kigiriki yana asili tofauti.) Ijapokuwa kwa hakika haimpasi mtu adharau hali ya kutochelewa kwa kadiri ya kuwa asiyefikiria au asiye na adabu, na ikumbukwe ya kwamba kundi la Kikristo katika siku za mtume halikufanya kufuata sana wakati kuwa jambo kubwa, kama unavyofanya ulimwengu wa kisasa wa kibiashara. Vile vile maandishi hayakuonwa kuwa kitu cha maana sana katika siku zao bila shaka. Ili kuwa mchungaji anayefaa wa kundi mzee hatakiwi na Maandiko awe mfanya kazi wa kuandika au bwana fedha mwenye ujuzi sana. Huenda akawako mtu fulani kati ya watumishi wa huduma anayeweza kufanya yo yote yanayohitajiwa kufanywa katika habari hii. (Matendo 6:1-6) Zaidi ya yote, imempasa mzee asikose kuwa mwenye utaratibu na haimpasi awe mshupavu, mtu asiyejali shauri la kimtume.​—1 The. 5:14; 2 The. 3:6-12; Tito 1:10.

Mkaribishaji. Imempasa awakaribishe wageni kwenye mikutano ya Kikristo, akionyesha usawa wa kupendezwa na maskini na wanyenyekevu sawa na wale ambao ni matajiri. Vile vile imempasa aonyeshe ukaribishaji kwa ndugu zake, kwa kadiri hali zake zinavyoruhusu, na kulingana na mahitaji yao.​—Rum. 12:13; 1 Tim. 3:2; Tito 1:8; Yak. 2:14-16.

Mwenye kustahili kufundisha. Imempasa awe “mwenye kushikamana sana na neno la uaminifu kwa habari ya ustadi [au, namna, njia] wake wa kufundisha, apate kuweza kutia moyo kwa fundisho ambalo ni lenye afya na kukaripia pia wale wanaopinganisha.” (Tito 1:9; 1 Tim. 3:2, NW) Kustahili kwake hakutokani na elimu ya kilimwengu au wepesi wa akili au ufasaha wa kusema. (Linganisha 1 Wakorintho 2:1-5, 13; 2 Wakorintho 10:10; 11:6.) Pahali pake, kunatokana na sababu ya “kushikamana sana na neno la uaminifu” kwa namna anavyofundisha. (Linganisha 2 Wakorintho 10:1; 2 Timotheo 4:2.) Hivyo, wakati anaposhikamana na kilicho chema na kweli, vile vile anaweza kujizuia mwenyewe na ‘kuwafundisha kwa upole wale wasiotaka.’ (2 Tim. 2:23-26, NW) Huenda asione ni vyepesi kukaripia, lakini upendo unamwongoza afanye hivyo pasipo kuogopa ikiwa kuna haja ya kweli. (Matendo 20:19-21, 26, 27) Namna gani ikiwa yeye ana uwezo kidogo wa kutoa hotuba za watu wote? Jambo hili halimzuii kuwachunga “kondoo” kwa upendo kama mmoja mmoja au kama jamaa kwa “fundisho ambalo ni lenye afya,” akiwatia moyo katika njia ya Kikristo ya uzima. (Tito 2:1-10; linganisha 1 Wakorintho 13:1, 2.) Hata kati ya wazee, si wote watakaoonyesha “neno la hekima” au “neno la maarifa” kwa kadiri ile ile, lakini tofauti hii yapaswa itazamiwe na kwa lazima haionyeshi ukosefu fulani wa kutimiza matakwa ya Maandiko kwa cheo cha mzee.​—1 Kor. 12:4-11.

Si mpigaji, bali mwenye kusikiliza shauri, si mtaka vita. Wala yeye hawapigi watu kwa kimwili wala si mwenye matusi wala mwenye msemo wenye kuchukiza, si mwenye kuwapiga-piga wengine. Yeye ni “mwenye kusikiliza shauri,” au kama usemi wa Kigiriki unavyomaanisha, “wepesi wa kukubali.” Juu ya usemi huu Expository Dictionary of New Testament Words ya Vine inasema: “. . . . si kusisitiza sana juu ya sheria; unaonyesha kule kufikiria kunakoyatazama mambo ya hakika ya shauri ‘kwa huruma na kwa kiasi.’ “(Yak. 3:17; Ebr. 5:1, 2; linganisha 1 Petro 2:18.) Hivyo, yeye si mtawala mwenye amri peke yake; si mwenye kuelekea kuyafanya mambo madogo yanakuwa makubwa. (Linganisha 1 Wakorintho 9:12, 18-23.) Neno la Kigiriki linalokamatana na hilo linamaanisha “fadhili.” (2 Kor. 10:1, NW) Akiwa “si mtaka vita,” anaepuka magombano, hivyo si “mwepesi wa hasira.”​—1 Tim. 3:3, NW; Tito 1:7; 3:2; Yak. 1:19, 20.

Si mwenye kutaka yake. Kama ilivyo, si ‘mwenye kujipendekeza mwenyewe’ au “mwenye kujikinai.” Kama kamusi za Kigiriki zinavyoonyesha, yeye anajinyenyekeza mwenyewe na uwezo wake, bila kuwa na mawazo ya juu ya uamuzi wake mwenyewe hata kujiona na kujifanya mkubwa; si “mwenye kujitegemea mwenyewe” au “mwenye kujikinai,” kana kwamba aweza mwenyewe kufanya kila jambo, au bora kuliko mtu mwingine ye yote. Kwa hiyo, yeye yuafurahia kushiriki daraka, akifanya kazi kwa unyenyekevu pamoja na wengine kama kundi, na kuona ubora wa wingi wa washauri.​—Tito 1:7; linganisha Hesabu 11:27-29; Warumi 12:3, 16.

Mwenye kupenda wema; mwenye haki. Kuwa ‘mwenye haki’ kunakamatana na kufuata kwa mtu sheria ya Mungu, kanuni zake za mema na haki. Mtu kama huyo atakuwa asiyependelea. (Luka 1:6; Yohana 7:24; Yak. 2:1, 4, 9) “Wema” unatofautiana na haki kwa vile unaendelea zaidi ya kile kinachotakiwa na haki. (Mt. 20:4, 13-15; Rum. 5:7) Mtu anayependa wema atawafanyia wengine zaidi ya kinachotakiwa au kinachotazamiwa kwake, akifanya matendo yenye msaada na fadhili kwa ukarimu, akiwa mkunjufu, mwenye kufikiria. Vile vile anaona, anashukuru na kusifu wema wa wengine.​—⁠Tito 1:8; Luka 6:35; Matendo 9:36, 39; 1 Tim. 5:10.

Mwaminifu. Ni mtu anayeendeleza uaminifu na ukamilifu usiovunjika kwa sheria ya Mungu na kwa faida ya kundi la Kikristo, bila kujali matokeo.​—Luka 1:74, 75; Matendo 4:19, 20; 5:29; 1 The. 2:10.

Bila shaka mtu kama huyo angepata “kushuhudiwa mema na watu walio nje.” Kama alivyokuwa nabii Danieli, mtu mwenye kutumainika ambaye wapinzani hawakuweza kupata uzembe ndani yake au jambo chafu, iliwapasa watu hao wa nje waseme, ‘Hatuwezi kupata sababu ya kumshitaki yeye, isipokuwa katika mambo ya sheria ya Mungu wake.’​—1 Tim. 3:7; Dan. 6:4, 5.

Ni kweli kwamba wale wanaostahili daraka la kundi watakuwa wenye nguvu zaidi katika nyingine za sifa hizi kuliko katika nyingine. Ebu fikiria tofauti kati ya mitume​—tofauti kati ya Tomaso na Petro​—hata hivyo baraza inayoongoza ya kwanza ilianzia na wanaume hawa. Lakini imewapasa wanaume hao watimize matakwa yote ya daraka lao kwa kadiri na kwa uaminifu wa kadiri. Kwa mfano, kosa moja katika kuamua hakumaanishi kwamba mtu si “timamu katika akili,” wala kuonyesha hasira mara moja kwa lazima hakumfanyi yeye kuwa “mtaka vita.”

Kwa kweli, matakwa si yasiyofikika kwa mwanamume ye yote wa Kikristo mwenye unyofu wa moyo, kwa maana, kama vile uchunguzi wa Maandiko unavyoonyesha, wingi wa sifa hizi umeandikwa kama mambo ambayo Wakristo WOTE, wanaume kwa wanawake, wamepaswa wajitahidi kufikia. Basi, wanaume walio na vyeo hivi vyenye madaraka wamepaswa wawakilishe kile ambacho kundi lote limepaswa liwakilishe kwa kufaa, kuwakilisha anavyopaswa kila Mkristo wa kweli awe. Wewe unatimizaje?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki