Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 9/15 kur. 10-15
  • Watumishi wa Huduma Ni Baraka kwa Watu wa Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Watumishi wa Huduma Ni Baraka kwa Watu wa Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Wajaribiwe Juu ya Kufaa Kwanza”
  • Wanasaidiwa na Huduma ya Wakati Wote
  • Wajibu Mbalimbali wa Watumishi wa Huduma
  • Wanatimizaje Sifa Hizo?
  • Watumishi wa Huduma Hufanya Utumishi Muhimu
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
  • Watumishi wa Huduma Dumisheni Msimamo Mzuri!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Watumishi wa Huduma Wana Majukumu Gani?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
  • Kudumisha Upatano Kati ya Wazee na Watumishi wa Huduma
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 9/15 kur. 10-15

Watumishi wa Huduma Ni Baraka kwa Watu wa Yehova

“Acha hawa wajaribiwe juu ya kufaa kwanza, ndipo acha watumike kuwa wahudumu, kwa vile hawana shtaka.”​—1 TIMOTHEO 3:10, Biblia ya New World Translation

1. Ni nani wanaosaidia kuhakikisha kundi lina furaha na umoja?

YEHOVA ndiye “Mungu mwenye furaha,” naye anawataka watumishi wake wawe wenye furaha. (l Timotheo 1:11, NW) Kwa kusudi hilo, amefanya uandalizi kuwe na wazee na watumishi wa huduma ili kubariki watu wake. Wanaume hao wenye madaraka wanatumikia kwa makusudi yenye kuleta faida na msaada ili kuhakikisha kundi la Kikristo linaendeshwa kwa furaha, umoja na unyofu. Hakika Mashahidi wa Yehova wanashukuru sana kwa sababu ya utumishi wenye upendo na msaada unaotolewa na watu hao waliowekwa rasmi ndani ya tengenezo la kitheokrasi la Mungu!

2. Wazee na watumishi wa huduma wanapaswa kuwa na nia gani, lakini haiwapasi kamwe kuacha kuangalia nini?

2 Lakini, ijapokuwa wazee na watumishi wa huduma wanashiriki kutoa msaada unaohitajiwa kabisa kwenye kundi, haiwapasi kutukuza umaana wao wenyewe. Ni lazima wakumbuke kwamba Yesu Kristo aliwaonya kwa upole wafuasi wake wawe wanyenyekevu. Wakati mmoja aliwaambia: “Ye yote ajinyenyekeshaye mwenyewe kama mtoto huyu, huyo ndiye aliye mkuu katika ufalme wa mbinguni.” (Mathayo 18:4) Naye mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Nyenyekeeni mbele ya [Yehova], naye atawainueni.” (Yakobo 4:10, HNWW; Warumi 12:3) Lakini kuwa na nia ya unyenyekevu si takwa la kwamba wanaume hao wadharau umaana wa kazi yao wakiwa wazee na watumishi wa huduma. Wanaweza kuwa wanyenyekevu na bado waongoze katika utendaji mbalimbali wa utumishi. Hawapaswi kamwe kuacha kuona ubora wa makusudi yenye faida yanayotimizwa na utendaji wao, bali inawapasa sikuzote wakumbuke wajibu wao, kwa Yehova na pia kwa ndugu zao Wakristo, ili wafanye yote wawezayo katika kutimiza wajibu wao.

3. Utendaji wenye umoja kati ya Mashahidi wa Yehova unaweza kulinganishwa na nini, na wanaume walio wakfu wanaweza kuendelezaje umoja huo na kusogeza mbele faida za Ufalme?

3 Utendaji wenye umoja kati ya Mashahidi wa Yehova leo unaweza kulinganishwa na umoja katika mwili wa kibinadamu. Kwa kweli, mtume Paulo alifananisha mwili wa kiroho wa Kristo na mwili wa kibinadamu wenye viungo vingi. Hata hivyo viungo vyote vya mwili vinafanya kazi pamoja kwa faida ya vyote. (1 Wakorintho 12:12-31) Na, kwa uhakika, wazee na watumishi wa huduma waliowekwa rasmi ni baraka kwa watu wa Yehova, kwa maana wanaume hao wanasogeza mbele uendeshaji wenye umoja wa kundi la Kikristo leo. (Linganisha Wakolosai 2:18, 19.) Washiriki wa kiume walio wakfu kundini ambao wanajitahidi kuunga mkono mpango wa tengenezo la Yehova kwa kujitahidi ‘wafikie cheo cha mwangalizi’ wanafanya sehemu inayohitajiwa kabisa ili kuleta umoja wa Kikristo na kuendeleza faida za Ufalme. (1 Timotheo 3:1, NW) Lakini mwanamume Mkristo anastahilije kwanza kuwa mtumishi wa huduma?

“Wajaribiwe Juu ya Kufaa Kwanza”

4. (a) Ni kwa sababu gani wanaotazamiwa kuwa watumishi wa huduma wanapaswa “wajaribiwe juu ya kufaa kwanza”? (b) Wanaume hao wanapaswa wawe na nia ya kufanya nini?

4 Mtume Paulo alimwambia Timotheo mfanya kazi mwenzake mambo yaliyotakwa kabla wanaume hawajaweza kuwekwa rasmi wawe watumishi wa huduma. Kati ya mambo mengine, Paulo aliandika hivi: “Acha hawa wajaribiwe juu ya kufaa kwanza, ndipo acha watumike kuwa wahudumu, kwa vile hawana shtaka.” (1 Timotheo 3:10, NW) Kufanya hivyo kungezuia kuweka rasmi wanaume wasiostahili, wale wasiotimiza matakwa fulani ya msingi ya Kimaandiko. Kungeruhusu wakati wa kujua makusudi ya waliotazamiwa kuwa watumishi wa huduma. Kwa uhakika, wanaume hao hawapaswi kusukumwa na tamaa ya kupata fahari, kwa maana hiyo ingeonyesha ukosefu wa unyenyekevu. Bali, ndugu akitambua uhakika wa kwamba wakfu wa Mkristo haufanywi kwa kuwekea Mungu masharti fulani bali unahusu kufanya yote yatakwayo, ndugu anapaswa awe na nia ya kutumikia katika cheo cho chote ambamo Yehova anaona inafaa kumtumia katika tengenezo Lake. Ndiyo, wanaotazamiwa kuwa watumishi wa huduma wanapaswa wawe na nia ya kutumikia kama Isaya mwaminifu: aliyesema: “Mimi hapa, nitume mimi.”​—Isaya 6:8.

5. (a) Ni matakwa gani ya watumishi wa huduma yaliyoonyeshwa katika 1 Timotheo 3:8? (b) Maana yake nini kuwa “wazito”? (c) Paulo alimaanisha nini kwa kusema kwamba ni lazima watumishi wa huduma wasiwe “wenye kauli mbili”?

5 “Watumishi wa huduma imewapasa vivyo hivyo wawe wazito, si wenye kauli mbili, si wenye kujitoa wenyewe kwa divai nyingi, si wenye pupa ya pato la udanganyifu,” Paulo akaeleza. (1 Timotheo 3:8, NW) Ingawa huenda watumishi wa huduma wengine wakawa ni vijana wakilinganishwa na wenzao, wao si vijana wadogo na ni lazima wawe “wazito.” Ni lazima wawe wamejifunza kuchukua mambo ya maana kwa uzito. (Linganisha Mithali 22:15.) Ni lazima wawe wenye kutegemeka na wenye kudhamiria mambo kwa bidii, si wanaume wenye maelekeo ya kuchukua madaraka kimchezo. Kwa kweli, wanapaswa kuwa wenye kutegemeka, wenye kuchukua wajibu wao kwa uzito. Ingawaje, ni nini kingine kingepasa kuhangaikiwa kwa uzito zaidi ya utumishi mtakatifu anaopewa Yehova? Huo ni jambo la uzima na kifo kwao na kwa wengine. (Linganisha 1 Timotheo 4:16.) Tena, kwa kusema kwamba watumishi wa huduma wasiwe “wenye kauli mbili,” Paulo alimaanisha kwamba walipaswa kuwa wenye kusema mambo kwa unyofu na ukweli, si wenye porojo, wanafiki, au wenye kufanya mambo kwa njia ambazo hazikunyooka vizuri.​—Mithali 3:32.

6. Ni kati ya njia gani ambazo watumishi wa huduma wanapaswa kuonyesha usawaziko?

6 Usawaziko mzuri ni wa lazima katika maisha ya kibinafsi ya wanaume wanaostahili kuwa watumishi wa huduma. Kwa wazi Paulo alimaanisha kwamba ni lazima waepuke ulevi, pupa, na ukosefu wa unyofu wakati aliposema kwamba hawapaswi kuwa “wenye kujitoa wenyewe kwa divai nyingi” wala kuwa “wenye pupa ya pato la udanganyifu.” Ni lazima wanaume hao Wakristo waepuke hata kufanya watu wawe na wazo la kwamba wao wanapendezwa na anasa au vitu vya kimwili kupita kiasi. Sikuzote wanapaswa wajitahidi kutanguliza mambo ya kiroho maishani. Jambo hilo litawasaidia wadumishe “dhamiri safi” mbele ya wanadamu wenzao na, hasa zaidi, machoni pa Mungu.​—1 Timotheo 3:8, 9, NW.

7. (a) Kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba madaraka ya watumishi wa huduma hayakusudiwi wapewe vijana wadogo? (b) Uhakika wa kwamba mtumishi wa huduma ni mseja (hajaoa) huenda ukaonyesha nini juu yake?

7 Madaraka mazito yanayokalia watumishi wa huduma hayakusudiwi wapewe vijana wadogo. Wanaume hao wanatajwa katika Andiko kuwa wenye umri wa kuweza kuoa na kuwa na jamaa. Chini ya hali hizo, ingewapasa wawe “wenye kusimamia kwa njia nzuri watoto na nyumba zao wenyewe.” (1 Timotheo 3:12, NW) Je! hiyo maana yake ni kwamba kijana mwanamume hangefaa kuwa mtumishi wa huduma mpaka aoe kwanza na kukuza jamaa? Sivyo, hata kidogo. Kwa kweli, kutokutaka kwake kujiingiza haraka-haraka katika ndoa bila kujitayarisha vya kutosha au kabla ya kupata mwenzi anayefaa, aliye Mkristo na aliyebatizwa, huenda kukaonyesha ana ukomavu wa kadiri fulani unaohitajiwa ili kutunza vizuri mambo ya kibinafsi na madaraka ya kundi ambayo ni yenye uzito zaidi.

8. Kuhusiana na 1 Timotheo 3:13 na Mathayo 24:14, ni daraka gani linalokalia watumishi wa huduma?

8 Paulo alisema kwamba “wanaume wanaohudumu kwa njia nzuri wanajipatia wenyewe msimamo mzuri na uhuru mkubwa wa kusema katika imani kuhusiana na Kristo Yesu.” (1 Timotheo 3:13, NW) Njia moja ambavyo wanaweza kuonyesha “uhuru mkubwa wa kusema” unaotakwa ni kwa kushiriki kwa bidii katika kuzihubiri “habari njema hizi za ufalme (Mathayo 24:14, NW) Wanapaswa wajue kwamba wanashiriki pamoja na wazee daraka la kutoa uongozi katika kuhubiri nyumba kwa nyumba na kushiriki katika namna nyingine za huduma. (Matendo 5:42; 20:20, 21) Mfumo mbovu wa Shetani unapokaribia haraka mwisho wao, utendaji wa kuhubiri unakuwa wa haraka zaidi. Basi, watumishi wa huduma wanapaswa kulionyesha kundi uharaka wa kazi ya kuhubiri Ufalme kwa kuweka mfano bora wa kibinafsi katika huduma ya shambani.

Wanasaidiwa na Huduma ya Wakati Wote

9. Kwa sababu ya uharaka wa nyakati zetu, Wakristo wengi wamechukua utumishi gani?

9 Kwa sababu ya uharaka wa nyakati zetu za hatari, wanaume na wanawake wengi Wakristo wamechukua huduma ya wakati wote. Wengi, ambao wanaitwa mapainia, wanatumia wastani wa kila siku wa kati ya saa mbili na tano katika kazi ya kuhubiri, wengine wao wakiwa wamisionari katika nchi za kigeni. Wengine wanatumikia wakati wote kwenye makao makuu ya Sosaiti yetu au katika afisi za matawi za Sosaiti hiyo duniani pote. Utumishi wao ni chanzo cha furaha na uradhi kwao na kwa wale wanaowatumikia. Na katika visa vingi ujuzi unaopatikana katika utumishi wa wakati wote umesaidia wanaume kusitawisha sifa zinazohitajiwa ili kutumikia kundi kwa njia yenye faida wakiwa watumishi wa huduma.

10, 11. Kama inavyoonyeshwa na maneno ya kibinafsi yaliyotajwa hapa, wanaume wanaotaka kuwa watumishi wa huduma wanaweza kufaidiwaje na utumishi wa wakati wote?

10 Mmoja aliyekuwa mtumishi wa huduma, ambaye sasa ni mzee katika kundi fulani la Berlin, Ujeremani, anasema hivi juu ya kazi ya painia aliyochukua miaka kadha iliyopita akiwa kijana mwanamume: “Naweza kusema ilikuwa hatua ambayo sijajuta kamwe kwamba niliichukua. Yehova amenibariki. Uhusiano wangu pamoja naye umekuwa wa ndani zaidi.” Ndiyo, kama maelfu ya wengine, ndugu huyo aligundua kwamba huduma ya wakati wote inaweza kuongeza kina cha uhusiano wa mtu pamoja na Yehova na kuharakisha maendeleo yake kuelekea ukomavu wa Kikristo.

11 Painia mwingine wa muda mrefu anaeleza namna utumishi wa wakati wote ulivyomsaidia. “Nilitulia nikawa mwenye usawaziko zaidi juu ya kutokufanya maamuzi ya haraka-haraka,” anasema. “Nilipata furaha nyingi zaidi nikawa mwenye kubadilikana zaidi katika kushughulika na namna mbali-mbali za watu.” Je! hizo si kati ya sifa zinazohitajiwa na wanaume wanaotaka kutumikia wakiwa watumishi wa huduma?

12. (a) Kuna nafasi gani za kushiriki katika huduma ya wakati wote? (b) Kushiriki katika huduma ya wakati wote kunahitaji uwezo gani mbalimbali ambao ungesaidia mtumishi wa huduma atimize wajibu wake?

12 Kushiriki katika huduma ya wakati wote, ikiwa madaraka ya Kimaandiko yanaruhusu, kunaweza kuwa nafasi nzuri sana kwa Wakristo wa kiume ya ‘kujaribiwa juu ya kufaa kwanza.’ Wengine wanaweza kuchukua huduma hiyo waifanye daima, wengine mara kwa mara. Vijana wanaweza kufanya hivyo wakati wa malikizo ya shule, na watu wazee-wazee wakati wa vipindi vya likizo au nyakati nyingine zinazofaa mwakani. Bila shaka, kushiriki katika utumishi wa wakati wote kunahitaji usawaziko na mipango ya uangalifu. Uwezo huo unahitajiwa na mtumishi wa huduma na utamsaidia atimize wajibu wake mbalimbali. Wajibu gani mbalimbali?

Wajibu Mbalimbali wa Watumishi wa Huduma

13. Andiko la Matendo 6:1-6 linadokeza nini juu ya namna ya kazi wanayogawiwa watumishi wa huduma?

13 Ingawa andiko la Matendo 6:1-6 (NW) halihusu moja kwa moja kuweka rasmi watumishi wa huduma, yanayosemwa hapo yanadokeza namna ya kazi au hali ya wajibu mbalimbali ambao kwa kawaida watumishi wa huduma ndio wangegawiwa. Kwa kugawa chakula, wala si kwa kufundisha waamini wenzao, wale “wanaume saba waliothibitishwa” wakachaguliwa wakati huo walifanya mitume wawe na uhuru wa ‘kujitoa kwa sala na huduma ya lile neno.’ Kwa kutunza wajibu mbalimbali unaofanana na huo leo, watumishi wa huduma wanawapa wazee wakati mwingi zaidi wa kuchunga na kufundisha “kundi la Mungu.”​—1 Petro 5:2, 3.

14. Ni kazi za namna gani mbalimbali wanazoweza kugawiwa watumishi wa huduma?

14 Kuhusu wajibu mbalimbali wa watumishi wa huduma, kitabu Tumefanywa Tengenezo Tutimize Huduma Yetu kinasema: “Mtumishi wa huduma mmoja anaweza kupewa mgawo wa kuangalia vitabu vya kundi, akifanya iwezekane kwetu sote kupata vitabu tunavyohitaji kwa matumizi yetu ya kibinafsi na ya utumishi wa shambani. Mwingine anaweza kuangalia magazeti katika kundi. Wengine wanagawiwa kazi za kutunza maandishi kama vile hesabu za kundi au kugawa eneo, au wanatumiwa kurekebisha maikrofoni, kushughulika na vikuza-sauti, kutunza jukwaa au labda kusaidia wazee kwa njia nyingine. Kuna kazi nyingi za kutunza na kutengeneza Jumba la Ufalme na kuliweka safi, hivyo watumishi wa huduma wanaombwa wasaidie kutimiza madaraka hayo. Vilevile watumishi wa huduma wanapewa migawo ya kuwa wakaribishaji, wanakaribisha wapya na kusaidia kutunza utaratibu penye mikutano ya kundi.”​—Kurasa 57-8.

15. (a) Ili mtu atumikie kwa matokeo mazuri akiwa mtumishi wa huduma, ni jambo gani linalohitajiwa zaidi ya kuwa na uwezo wenye mafaa? (b) Ingawa watumishi wa huduma wanatunza mambo mbalimbali, hangaikio lao kuu linapasa kuwa nini?

15 Je! ndugu ye yote tu aliye na uwezo unaofaa angeweza kufanya kazi ya namna hiyo? Hapana, kwa maana wale ‘wanaume waliothibitishwa’ ambao walichaguliwa katika Yerusalemu wa karne ya kwanza walikuwa “wamejawa na roho na hekima,” au walikuwa “wenye mafaa hata wenye akili za kufikiria mambo ya kiroho.” (Matendo 6:3, Phillips) Hata ikiwa tayari walikuwa wanaume wenye umri mkubwa kati ya watu wa Yehova, waligawiwa kazi inayofanana na ile inayofanywa sasa na watumishi wa huduma. Kwa hiyo ikiwa watumishi wa huduma wa kisasa wanataka kutimiza wajibu wao kwa matokeo mazuri, ni lazima wawe “wenye mafaa hata wenye akili za kufikiria mambo ya kiroho.” Ingawa wanashughulika na mambo ya kitengenezo, upendezi wao mkuu unapasa kuwa kutumikia watu kwa njia zenye kuwafaidi kiroho.

16. Ikiwa katika kundi hamna wazee wa kutosha, watumishi wa huduma wanaweza kugawiwa kazi gani?

16 Kwa kuwa ni lazima watumishi wa huduma wawe na akili za kufikiria mambo ya kiroho, nyakati nyingine wanaweza kutumiwa kwenye kazi ambayo kwa kawaida inafanywa na wazee. Kitabu Tumefanywa Tengenezo Tutimize Huduma Yetu (ukurasa 59) kinaeleza hivi: “Kama hakuna wazee wa kutosha kuongoza Mafunzo ya Kitabu ya Kundi, wengine kati ya watumishi wa huduma wenye kustahili zaidi wanatumiwa kuwa viongozi wa funzo waangalie vikundi walivyogawiwa. Wanaweza kupewa migawo ya kuongoza sehemu katika Mkutano wa Utumishi na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na kutoa hotuba za watu wote katika kundi la kwao. Watumishi fulani wa huduma wanaweza kupewa mapendeleo mengine ikiwa kuna uhitaji na ikiwa wanatimiza matakwa ya mgawo.​—Linganisha 1 Petro 4:10.”

17. Stefano alikuwa mwanamume wa namna gani, na jambo hilo linatokeza ulizo gani kuhusu watumishi wa huduma?

17 Mmoja wa wale “wanaume saba waliothibitishwa” nyakati za Biblia alikuwa “Stefano, mwanamume mwenye kujawa na imani na roho takatifu.” (Matendo 6:5, NW) Kabla ya kufa akiwa mfia-imani mwaminifu, Stefano alitoa ushuhuda wenye kusisimua mbele ya baraza kuu la Kiyahudi. Soma masimulizi hayo, nawe utasadiki kwamba alikuwa mwenye akili ya kufikiria mambo ya kiroho na alikuwa mwenye nia ya kutoa uhai wake katika utumishi wa Yehova. (Matendo 6:8–7:60) Ikiwa wewe ni mtumishi wa huduma, je! unachukua wajibu wako mbalimbali wa kundi na huduma ya shambani kwa uzito kama vile inavyoonekana wazi kwamba Stefano aliyachukua kwa uzito madaraka yake na pendeleo la kunena ukweli?

Wanatimizaje Sifa Hizo?

18. Ni nini linaloweza kusemwa juu ya kazi ya watumishi wa huduma wengi, nao wanaweza kuwa na uhakika juu ya nini?

18 Watumishi wa huduma wengi wanaweka mfano mwema katika maisha ya Kikristo, wanatunza vizuri sana madaraka yao ya kundi, na wanatoa uongozi mzuri katika huduma ya shambani. Kazi yao inathaminiwa sana na waabudu wenzao na haitaachwa bila kuthawabishwa na Yehova, kwa maana Wakristo Waebrania walihakikishiwa hivi: “Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu, na hata hivi sasa mngali mkiwahudumia.”​—Waebrania 6:10.

19. (a) Kila mtumishi wa huduma anaweza kujiuliza maulizo gani? (b) Kwa sababu gani litakuwa jambo lenye faida kuzungumza matatizo wanayopata watumishi wa huduma?

19 Lakini, ingefaa kila mtumishi wa huduma ajiulize hivi: Mimi natimizaje matakwa ya Kimaandiko? Kweli mimi nashiriki kuongeza umoja wa kundi? Je! ninautunza wajibu niliogawiwa kwa njia inayofaa na kwa bidii? Je! ninaweka mfano mwema katika huduma ya shambani? Watumishi wa huduma wengine wamekabili matatizo katika kutimiza mambo wanayotakwa wafanye. Kwa hiyo acheni tuyazungumze mengine ya matatizo hayo. Kufanya hivyo kunaweza kusaidia kila mtumishi wa huduma “athibitishe kazi yake mwenyewe ikoje.” (Wagalatia 6:4, NW) Kunapasa pia kuongeze uthamini wa wengine juu ya kazi za upendo zinazofanywa na wanaume hao wanaotumikia kwa makusudi yenye faida kati ya Mashahidi wa Yehova na ambao ni baraka kweli kweli kwa watu wa Mungu.

Unaweza Kueleza?

◻ Ni kwa njia gani watumishi wa huduma ni baraka kwa watu wa Yehova?

◻ Huduma ya wakati wote inaweza kusaidiaje ndugu wanaotaka kuwa watumishi wa huduma?

◻ Kwa sababu gani ni lazima watumishi wa huduma wawe “wenye mafaa na hata wenye akili za kufikiria mambo ya kiroho”?

◻ Stefano mwaminifu alikuwaje mfano mzuri kwa watumishi wa huduma leo?

[Picha katika ukurasa wa 11]

Wazee na watumishi wa huduma ni Baraka kwa kundi

[Picha katika ukurasa wa 13]

Utumishi wa painia ni mazoezi bora kwa wale wanaotaka kuwa watumishi wa huduma au wazee

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki