Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 9/15 kur. 15-20
  • Watumishi wa Huduma Dumisheni Msimamo Mzuri!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Watumishi wa Huduma Dumisheni Msimamo Mzuri!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Useja na Ndoa
  • Kazi ya Kuajiriwa na Kupenda Mno Vitu vya Kimwili
  • Utii Kamili kwa Ufalme wa Mungu
  • Uhitaji wa Kuwa na Ujuzi Mkubwa Zaidi
  • Kupambana na Hali ya Kuvunjika Moyo
  • Namna Wengine Wanavyoweza Kusaidia
  • Watumishi wa Huduma Ni Baraka kwa Watu wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Watumishi wa Huduma Hufanya Utumishi Muhimu
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
  • Watumishi wa Huduma Wana Majukumu Gani?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
  • Kudumisha Upatano Kati ya Wazee na Watumishi wa Huduma
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 9/15 kur. 15-20

Watumishi wa Huduma Dumisheni Msimamo Mzuri!

“Wanaume wanaohudumu kwa njia nzuri wanajipatia wenyewe msimamo mzuri na uhuru mkubwa wa kusema katika imani kuhusiana na Kristo Yesu.”​—1 TIMOTHEO 3:13, Biblia ya New World Translation.

1. Baada ya mwanamume kuwekwa rasmi awe mtumishi wa huduma, mradi wake unapaswa kuwa nini, na wengine kundini wanapaswa watake kufanya nini?

WANAUME ambao sasa ni watumishi wa huduma ‘wamejaribiwa juu ya kufaa kwanza.’ (1 Timotheo 3:10, NW) Lakini kuwekwa kwao kwenyewe hakukuwa ndiko mwisho. Mradi wao ni kuendelea ‘kujipatia wenyewe msimamo mzuri’ kwa kutimiza kazi zao “kwa njia nzuri.” (1 Timotheo 3:13, NW) Kila mshiriki wa kundi la Kikristo lenye umoja atataka kuwaunga mkono waufikie mradi huo.

2. Washiriki wa kundi wanapatwa na matokeo ya namna gani kwa sababu ya mambo yanayofanywa na watumishi wa huduma?

2 Mtume Paulo alionyesha kwamba washiriki wote wa mwili wa kiroho wa Kristo wanafaidika kwa kufanya kazi pamoja na kutunzana. (1 Wakorintho 12:12-31) Vivyo hivyo, wakati watumishi wa huduma wanapofanya “kwa njia nzuri” kazi yao waliyopewa na Mungu, kila mshiriki wa kundi la Kikristo la kisasa anafaidika. Lakini wakati watumishi wa huduma wanapokuta matatizo yanayowazuia kutimiza vizuri kazi zao, huenda jambo hilo likawatatiza washiriki wote wa kundi.

3. (a) Ni matatizo gani yaliyo ya kawaida sana kwa watu wote wa Yehova? (b) Uchunguzi wa karibuni unasaidia kuonyesha nini?

3 Watu wote wa Yehova wana pigano lile lile moja, “kushindana mweleka, si juu ya damu na nyama, bali . . . juu ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.” (Waefeso 6:12, NW) Tena, watumishi wote wa Yehova wana pigano dhidi ya hali zao wenyewe za kutokamilika na maelekeo yenye dhambi. Lakini, wakiwa kikundi, watumishi wa huduma wanaelekewa na matatizo fulani kwa njia ya wazi zaidi ya vikundi vingine vya Mashahidi wa Yehova. Unaosaidia kutoa mfano wa jambo hilo ni uchunguzi wa karibuni uliofanywa katika makundi zaidi ya 320 yenye watumishi wa huduma 1,360 katika nchi moja ya magharibi ya Ulaya.

Useja na Ndoa

4. Watumishi wa huduma wasiooa wanapaswa kuuonaje useja, na wengine wanaweza kuwapa kitia-moyo gani?

4 Kati ya watumishi wa huduma waliochunguzwa, hesabu inayozidi kidogo asilimia 10 wangali waseja. Hivyo wanafurahia uhuru wa kutokuwa na madaraka fulani yaliyo kawaida ya wale karibu asilimia 90 ambao wameoa. Lakini ni lazima ndugu waseja wajihadhari wasitumie uhuru huo kwa kusudi la kufuatia tu mambo ya kibinafsi kama tafrija za kupita kiasi au starehe za kirafiki. Wala wasiruhusu ile tamaa ya asili ya kutaka ndoa itangulizwe mbele ya kila jambo jingine maishani. (Mathayo 6:33) Wala wasiruhusu mkazo kutoka kwa rafiki zao waliooa uwalazimishe kuingia katika ndoa ya haraka-haraka au isiyo ya hekima. Na kwa uhakika Wakristo, ambao wanatunzana wao kwa wao wataheshimu hali ya useja ya waamini wenzao wasiooa na kuwatia moyo watumie kwa faida uhuru wao mkubwa zaidi ili watumie wakati mwingi zaidi kwenye shughuli za kitheokrasi, labda kwa kuchukua huduma ya wakati wote.

5. Kuna hatari gani kubwa kwa watumishi wa huduma waliooa kuliko kwa wale walio waseja?

5 Kulingana na uchunguzi uliotangulia kutajwa, wingi mkubwa wa watumishi wa huduma wameoa na karibu asilimia 62 ni wazazi. Kwao, hatari ya mioyo yao kulemewa na “masumbufu ya maisha” ni kubwa kuliko ilivyo kwa ndugu waseja. (Luka 21:34-36) Hivyo, katika kupendekeza useja, Paulo alisema: “Nataka mwe huru bila usumbufu. Mwanamume asiyeoa anasumbukia mambo ya Bwana, namna anavyoweza kupata kibali ya Bwana. Lakini mwanamume aliyeoa anasumbukia mambo ya ulimwengu, namna anavyoweza kupata kibali ya mke wake, na anakuwa amegawanyika. . . . Yeye pia anayetoa ubikira wake katika ndoa anafanya vizuri, lakini yeye asiyeutoa katika ndoa atafanya vizuri zaidi.”​—1 Wakorintho 7:32-38, NW.

6. Watumishi wa huduma waliooa wanahitaji kufanya nini, na ni nani wanaoweza kutoa maoni yenye msaada?

6 Ingawa watu wa Yehova hawaamini kwamba ‘ndoa za watu zinatayarishiwa mbinguni wanajua kwamba hekima ya kimbingu inahitajiwa ili kutatua matatizo ya ndoa. (Zaburi 19:7; Mithali 3:5,6) Kwa hiyo watumishi wa huduma waliooa wanahitaji kufuata shauri la Neno la Mungu kwa ukaribu kama inavyowezekana. Ni lazima wajitahidi kuwa na usawaziko unaofaa katika kutimiza madaraka ya jamaa, na bado wasiyatumie kamwe kama udhuru wa kupuuza wajibu wao wa kitheokrasi katika kundi. Kati ya mambo mengine, ratiba iliyofikiriwa vizuri inahitajiwa kabisa. Wenzi ambao wamekuwa katika ndoa kwa muda mrefu na wenye ujuzi zaidi wanaweza kutolea walio wachanga maoni yenye mafaa katika jambo hilo, wakiombwa wafanye hivyo.

7. (a) Jamaa ya mtumishi wa huduma aliyeoa inaweza kuwa na matokeo gani juu ya jitihada na maendeleo yake ya kiroho? (b) Ingefaa watumishi wa huduma wanaopanga kuoa wakumbuke nini?

7 Mtumishi wa huduma aliyeoa anapata msaada mkubwa akiungwa mkono na jamaa yake. Bila shaka, washiriki wa jamaa wanaomdai wakati na uangalifu kupita kiasi au kudai kupita kiasi mambo ya kimwili wanaweza kuzuia maendeleo yake ya kiroho. Lakini ni haraka wakati jamaa yao nzima inapounga mkono jitihada zake za ‘kuhudumu kwa njia nzuri.’ (1 Timotheo 3:13, NW) Kwa hiyo kabla mtumishi wa huduma asiyeoa hajahusisha maoni ya moyoni na anayetazamiwa kuwa mwenzi wa ndoa ni jambo la maana kama nini kwamba ajaribu kuamua kama huyo ataelekea kuendeleza maendeleo yao ya kiroho!

Kazi ya Kuajiriwa na Kupenda Mno Vitu vya Kimwili

8. (a) Watumishi wa huduma wanaelekeana na hatari gani inayoweza kutokea kuhusiana na kazi ya kuajiriwa kimwili? (b) Ni kutafakari juu ya maandiko gani kunakoweza kusaidia mtu ashindane na kupenda mno vitu vya kimwili?

8 Wanane kati ya kila watumishi wa huduma 10 waliochunguzwa walikuwa chini ya umri wa miaka 60. Kwa hiyo katika visa vingi wao wangali wakifanya kazi ya kimwili ili kujiruzuku wao wenyewe na jamaa zao. Karibu watano kati ya kila 10 kati yao wana umri wa kuanzia miaka 20 mpaka 40—na huo ndio muda ambao kwa kawaida wanaume wa ulimwengu wanajiimarisha katika kazi au shughuli ya maisha yote na kujitahidi kupanda ngazi na kuwa salama kifedha. Ikiwa wewe ni mtumishi wa huduma aliye kati ya umri huo, usiipuuze hatari ya kukuza nia ya kilimwengu ya kupenda mno vitu vya kimwili ambayo inaweza kukudhoofisha kiroho. Bali, kumbuka kwamba Paulo alisema: “Tukiwa na chakula na nguo tutaridhika na vitu hivyo.” (1 Timotheo 6:8) Yesu, pia, alitoa shauri zuri linaloweza kutusaidia sisi sote tushindane na hali ya kupenda mno vitu vya kimwili. Jisomee mwenyewe shauri hilo kwenye Mathayo 6:19-34.

9. Kupatana na Mathayo 16:26, ni mwendo gani wa hekima unaopasa kufuatwa na watumishi wa huduma walio vijana hasa?

9 Na sana-sana ninyi watumishi wa huduma wenye umri wa chini kidogo, watazameni wanaume wanaosemwa ati ni ‘wenye mafanikio’ wanaofuatia kazi za maisha yote za kilimwengu, au wanaojirundikia utajiri lakini wakimweka Yehova nje ya mipango yao. (Linganisha Mithali 16:3; 19:21.) Je! kwa kweli ingekuwa hekima gani mkijifuatisha kwa kiolezo cha watu mmoja mmoja wasiofikiria mambo ya kiroho, wenye kupenda mno vitu vya kimwili, ambao maisha zao zitafyekwa karibuni wakati wa ile “dhiki kubwa”? (Mathayo 24:21) Ni mtumishi gani wa Yehova angebadilishana cheo chake na watu hao! “kwani atafaidiwa nini mtu akiupata ulimwengu wote, na kupata hasara ya nafsi yake?” akasema Yesu. (Mathayo 16:26) Kwa uhakika, mwendo wa hekima ni kujenga wakati ujao salama pamoja na tengenezo la Yehova badala ya wakati ujao mfupi wenye kupungukiwa sana na usalama pamoja na ulimwengu huu unaokufa ulio katika uwezo wa Shetani.​—1 Yohana 5:19

Utii Kamili kwa Ufalme wa Mungu

10. Kwa habari ya mambo ya kisiasa, ni msimamo gani unaochukuliwa na “shirika la wanaume vijana” linaloongezeka, kutia na watumishi wa huduma?

10 Ilisemwa hivi kwa unabii juu ya Mfalme wa Kimasihi wa Yehova: “Watu wako watajitoa wenyewe kwa moyo wa kupenda siku ya jeshi lako la vita. Katika fahari za utakatifu, kutoka tumbo la uzazi la mapambazuko, unalo shirika la wanaume vijana kama matone ya umande.” (Zaburi 110:3, NW) Unabii huo umekuwa ukitimizwa tangu mwaka wa 1914 W.K., na wale walio wa “shirika la wanaume vijana” linaloongezeka wanajua kwamba utii wao kamili ni lazima utolewe kwanza kwa Ufalme wa Mungu ambao Mfalme wao ni Yesu Kristo aliyetukuzwa. Kwa hiyo ingawa wanaume hao walio wakfu, kutia na watumishi wa huduma, wanatii kwa kiasi “mamlaka zilizo kuu” za kiserikali, mapendezi ya pande hizo mbili yakipingana ni lazima wao ‘watii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.’ (Warumi 13:1; Matendo 5:29, NW) Kama vile Yesu alivyosema, wafuasi wake “si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:19; 18:36, NW) Wanaendelea bila kutokuwamo katika mambo ya kisiasa ya mataifa, wakitambua kwamba kutenda tofauti na hivyo kungewafanya wawe mahaini wa Ufalme wa Mungu.

11. Ndugu wanaotaabika kwa sababu ya kudumisha kutokuwamo kwa Kikristo wanaweza kuwa na uhakika juu ya jambo gani?

11 Namna gani watumishi wa huduma au wengine wakipoteza kazi yao ya kuajiriwa au hata uhuru wao kwa sababu ya kudumisha kutokuwamo kwa Kikristo? (Isaya 2:2-4; Yohana 17:16) Basi hapo wanajua kwamba ndugu na dada zao wa kiroho watawaunga mkono kiroho kwa njia yo yote wanayoweza, hata kimwili, ikiwa lazima. Hivyo ndivyo ilivyo kwa sababu watu wa Yehova wanatunzana wao kwa wao kwa upendo.​—Linganisha Yohana 13:34, 35; 1 Wakorintho 12:24, 25.

Uhitaji wa Kuwa na Ujuzi Mkubwa Zaidi

12. [Swahili halitafsiriwa]

12 Karibu theluthi moja (1/3) ya watumishi wa huduma waliochunguzwa wamekuwa Mashahidi wa Yehova kwa muda unaopungua miaka kumi. Kwa wazi, wanaume hao wamekubali msaada na uongozi wa washiriki wa kundi wenye ujuzi zaidi. Lakini ‘kujipatia msimamo mzuri’ kungehusu kuendelea kujifunza kutokana na wengine na kuongeza ujuzi. Kungemaanisha pia kuweka daima miradi ya kibinafsi na kudhamiria kujitahidi kuifikia. Kwa hiyo ikiwa wewe unataka kwa hamu nyingi utimize makusudi yenye faida ukiwa mtumishi wa huduma au ikiwa unajitahidi ukafikie pendeleo hilo, je! umejiwekea miradi fulani ya kibinafsi? Kwa mfano, mbona usiamue uwe umemaliza kusoma Biblia nzima ifikapo tarehe fulani au uwe painia msaidizi wakati wa miezi fulani?

13. Ni shauri gani alilopewa Timotheo ambalo lingefaidi ndugu anayetaka kuwa mtumishi wa huduma au ambaye sasa anatumikia katika cheo hicho?

13 Ikiwa wewe ni kijana kwa umri au ujuzi, unaweza kufaidika kutokana na yanayosemwa kwenye 1 Timotheo 4:12-15. Ingawa mwangalizi kijana Timotheo ndiye aliyeambiwa maneno hayo, mengi ya aliyosema Paulo humo juu ya usemi na mwenendo yangefaidi ndugu ye yote anayetaka kuwa mtumishi wa huduma au ambaye tayari anatumikia katika cheo hicho. Mtume aliandika: “Mtu awaye yote asiudharau ujana wako, bali uwe kielelezo kwao waaminio, katika usemi na mwenendo, na katika upendo na imani na usafi. Hata nitakapokuja, ufanye bidii katika kusoma na kuonya na kufundisha. Usiache kutumia karama ile iliyomo ndani yako, uliyopewa kwa unabii na kwa kuwekewa mikono ya wazee. Uyatafakari hayo; ukae katika hayo; ili kuendelea kwako kuwe dhahiri kwa watu wote.” Ni jambo gani hasa unalohitaji kutengeneza ili “kuendelea kwako kuwe dhahiri kwa watu wote?” Sali ujue unahitaji kufanya jambo halafu ulifanye kwa msaada wa Yehova!

Kupambana na Hali ya Kuvunjika Moyo

14, 15. (a) Kuna kitia-moyo gani cha Kimaandiko kwa watumishi wa huduma wanaolazimika kuvumilia hali ya uzee au afya mbaya? (b) Wanaume hao wanaweza kuwatiaje moyo wengine kundini?

14 Watumishi wa huduma wengi hawalazimiki kushindana na matatizo yanayopatikana sana kati ya vijana wa kiume. Wao wanaelekeana na uzee au afya mbaya, na mambo hayo yanaweza kuvunja moyo. Lakini wale wanaoendelea kuwa na nguvu kiroho wanaweza kujipatia faraja kutokana na maneno haya ambayo Paulo aliwaambia Wakristo wenzake waliopakwa mafuta: “Hatulegei; bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa; lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku. Maana dhiki yetu nyepesi, iliyo ya muda wa kitambo tu, yatufanyia utukufu wa milele uzidio kuwa mwingi sana; tusiviangalie vinavyoonekana, bali visivyoonekana. Kwa maana vinavyoonekana ni vya muda tu; bali visivyoonekana ni vya milele.” (2 Wakorintho 4:16-18) Pia watumishi wa Yehova walio na matumaini ya kidunia wana mataraja yenye kutia sana moyo​—yale ya kupata uzima wa milele katika paradiso ya kidunia.​—Luka 23:43; Yohana 17:3.

15 Kwa hiyo watumishi wa huduma wasioweza kutimiza mengi kama wengine kwa sababu ya afya mbaya au uzee wana sababu nzuri ya kudumisha nia yenye furaha na uhakika wa kutazamia mazuri. Kufanya hivyo kunaonyesha wanathamaini ukweli na wana imani yenye kina kirefu katika mambo ambayo ni ya milele. Roho nzuri namna hiyo, pamoja na utumishi wa unyenyekevu, itakuwa faida kubwa na kitia-moyo kwa kila mtu kundini.

16. Ni kwa sababu gani mtumishi wa huduma hapaswi kuvunjika moyo asipowekwa rasmi kuwa mzee?

16 Ikiwa wewe ni mtumishi wa huduma, endelea kujitahidi ‘ufikie cheo cha mwangalizi’ kwa kuendeleza uwezo wako wa kufundisha na sifa za kiroho. (1 Timotheo 3:1, NW) Lakini usivunjike moyo usipowekwa haraka uwe mzee. Kumbuka kwamba unapokuwa mtumishi wa huduma mwenye kutunza kazi zako “kwa njia nzuri” unatimiza makusudi yenye faida na wewe ni msaada mkubwa kwa kundi. Ni pendeleo kubwa kutumikia kwa njia yo yote ndani ya tengenezo la Yehova na kusaidia waamini wenzako watende kulingana na agizo la kuuhubiri Ufalme.​—Mathayo 24:14; 28:19, 20.

Namna Wengine Wanavyoweza Kusaidia

17. Mtumishi wa huduma anaweza kusaidiwaje na mkeye na watoto?

17 Wakitambua kwamba watumishi wa huduma wanatimiza makusudi yenye faida, watu wote wa Yehova wanapaswa watake kuunga mkono jitihada zao. Kwa mfano, litakuwa jambo jepesi zaidi kwa mwanamume kama huyo kuendelea ‘kuhudumu kwa njia nzuri’ ikiwa mke na watoto wake wanaridhika na mambo yale ya lazima maishani wala hawadai mambo mengi ya raha ambayo yangetaka mwanamume huyo afanye jitihada ya ziada katika kazi ya kimwili.-—1 Timotheo 6:6-8.

18. (a) Wazee wanaweza kusaidiaje watumishi wa huduma? (b) Kwa sababu gani kupashana habari kuzuri kunahitajiwa kabisa kati ya wazee na watumishi wa huduma?

18 Wazee wanaweza kusaidia watumishi wa huduma kwa kuwapa mwelekezo na mashauri yo yote yanayohitajiwa. Na maendeleo yakiisha kufanywa, wamepaswa wawapongeze kwa weupe wa moyo. Kati ya mambo mengine, wazee wanaweza kuambatana na watumishi wa huduma katika huduma ya shambani, wawasaidie kutayarisha hotuba, na kushiriki pamoja nao utajiri walio nao wa ujuzi wa Kikristo. Inaonekana kwamba kupendezwa nao na kupashana habari nao kwa njia hiyo kumeachiliwa nyakati nyingine. Kwa mfano, wakati alipoulizwa juu ya ripoti yake ya utumishi wa shambani ulio chini, mtumishi wa huduma mmoja alimwambia mwangalizi wa mzunguko hivi: “Mbona una uliza? Umekuwa chini kwa miaka mingi, lakini wewe ndiwe wa kwanza kabisa kusema lo lote juu ya jambo hilo.” Mara nyingi wazee wanaowatolea watumishi wa huduma mashauri yenye kuwajenga na ya upendo kisha kuwasaidia matatizo yao kwa subira wanapata furaha ya kuona matokeo ya kutokeza.

19. Ni kwa njia gani kila mshiriki wa kundi anaweza kusaidia watumishi wa huduma wadumishe “msimamo mzuri”?

19 Kwa kweli, kila mshiriki wa kundi anaweza kusaidia watumishi wa huduma wadumishe “msimamo mzuri” wao. Namna gani? Kwa kufanya ushirikiano pamoja nao na kuonyesha uthamini wa kutoka moyoni juu ya kazi yao. Sawasawa na vile ilivyo kawaida sehemu zote za mwili wa kibinadamu kufanya kazi pamoja ili kudumisha afya ya kimwili, ndivyo ilivyo lazima washiriki wote wa kundi wafanye ushirikiano kuhakikisha kwamba kundi lina afya nzuri ya kiroho. (Linganisha 1 Wakorintho 12:24, 25.) Kwa kusudi hilo, mengi yanafanywa na watumishi wa huduma wenye bidii ambao wanatimiza makusudi yenye faida na kudumisha msimamo mzuri. Acheni wao na mashahidi wote washikamanifu wa Yehova, watazamie wakati ujao wenye furaha ya milele, kisha waendelee kwa umoja kuufurahisha moyo wa yule “Mungu mwenye furaha.”​—Mithali 27:11, UV; 1 Timotheo 1:11, NW.

Tafadhali Eleza

◻ Ni matatizo gani huenda yakakabiliwa na watumishi wa huduma?

◻ Wake na watoto wa watumishi wa huduma wanaweza kufanya nini wawasaidie?

◻ Wazee wanaweza kufanya nini wasaidie watumishi wa huduma?

◻ Kila mshiriki wa kundi anaweza kufanya nini asaidie watumishi wa huduma?

[Picha katika ukurasa wa 16]

Ni lazima watumishi wa huduma watimize madaraka yao kwa uaminifu katika kazi ya kufanya wanafunzi na ndani ya kundi

[Picha katika ukurasa wa 19]

Watumishi wa huduma wa zamani Zaidi wanaweza kusaidia sana kundi na kulitia moyo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki