Sanduku La Swali
◼ Je, sala inapaswa kutolewa kwenye funzo la Biblia mlangoni?
Kwa kuwa hali hutofautiana, yule anayeongoza funzo atahitaji kutumia busara ili kuamua kama atatoa sala kwenye funzo la Biblia mlangoni. Jambo moja linalopaswa kufikiriwa ni malezi ya mwanafunzi. Huduma Yetu ya Ufalme ya Machi 2005, ukurasa wa 4, inasema: “Inafaa kuanza na kumalizia funzo kwa sala. Nyakati nyingine tunaweza kutoa sala hata tunapojifunza kwa mara ya kwanza pamoja na wanadini. Lakini tunapoongoza funzo pamoja na wanafunzi wengine huenda tukahitaji kutumia busara ili tutambue wakati unaofaa wa kuanza kutoa sala.”
Jambo lingine linalopaswa kufikiriwa ni mahali ambapo funzo linafanyiwa. Ikiwa ni mahali pa faragha, sala fupi ya kufungua na kufunga funzo inaweza kutolewa kwa busara. Hata hivyo, ikiwa kutoa sala kutavutia uangalifu wa watazamaji au kutamfanya mwanafunzi asijihisi huru, basi ingefaa kusubiri hadi wakati ambapo funzo litafanyiwa mahali pa faragha zaidi.
◼ Je, dada anapaswa kujifunika kichwa ikiwa anaandamana na mhubiri wa kiume kwenye funzo la Biblia mlangoni?
Ndiyo. Dada anapoongoza funzo la Biblia linalofanywa kwa ukawaida akiandamana na mhubiri wa kiume, anapaswa kujifunika kichwa. (1 Kor. 11:3-10) Anapaswa kujifunika kichwa iwe funzo hilo linafanyiwa nyumbani, mlangoni, au mahali pengine. Gazeti Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 2002, ukurasa wa 27, linasema: “Kwa kuwa funzo hilo huwa limepangwa kimbele, mwenye kuongoza anafundisha na kusimamia. Chini ya hali hizi, funzo hilo ni kama mkutano wa ziada. Dada akiongoza funzo hilo akiwa pamoja na ndugu aliyebatizwa, anapaswa kufunga kitambaa kichwani.” Anapaswa kujifunika kichwa pia iwapo anaandamana na mhubiri wa kiume ambaye hajabatizwa.
Kwa upande mwingine, ikiwa funzo la Biblia mlangoni halijaanzishwa bado, si lazima dada ajifunike kichwa akiwa pamoja na mhubiri wa kiume, hata ikiwa kusudi la ziara hiyo ni kuonyesha jinsi funzo huongozwa au kuzungumzia habari katika mojawapo ya vichapo tunavyotumia kuongoza mafunzo. Kwa kuwa mara nyingi mafunzo ya Biblia mlangoni huanzishwa hatua kwa hatua, baada ya kufanya ziara kadhaa za kurudia, wahubiri wanahitaji kufikiria hali na kuwa wenye busara wanapoamua wakati ambapo dada anapaswa kujifunika kichwa.